Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niipongeze Wizara, Waziri Mheshimiwa Ummy pamoja na timu yake yote kwa taarifa iliyosheheni na kukidhi kiu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuipongeza Wizara ningeomba kujenga au kuboresha vituo vyetu vya afya nchini. Kwa mfano, Jimbo la Lushoto lina kituo cha afya kimoja tu ambacho kipo katika kata ya Mlola. Kituo cha afya hiki kiliahidiwa kupata huduma ya upasuaji lakini mpaka leo huduma ile haipo. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu ipeleke huduma hiyo mapema ili kuzuia vifo hasa vya akina mama na watoto.

Pia niiombe Serikali yangu tukufu ipandishe hadhi zahanati ya Makanya kuwa kituo cha afya, pamoja na kujenga kituo cha afya katika kata ya Ngwelo kwani maeneo yote haya yapo mbali sana na huduma za afya ukizingatia hata miundombinu ya barabara ni mtihani, hali hii inasababisha vifo vya wananchi walio wengi pamoja na vifo vya akina mama na watoto.

Sambamba na hayo wananchi wamehamasika kwa kujitolea nguvu zao kwa kushirikiana na Mbunge wao, wameanzisha ujenzi wa vituo vya afya viwili ambavyo vipo maeneo ya Ngwelo na Gare. Hiki cha Gare kina vyumba kumi bado wananchi wanaendelea kujenga. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu tukufu ichukue majengo yale ili iweze kuyamalizia na wananchi waweze kupata huduma kwa ukaribu zaidi kuliko hii adha wanayoipata sasa hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sabamba na hayo pia kuna zahanati zaidi ya 13, zipo kwenye hatua tofauti, nyingine zimeisha lakini hazina vifaa wala watumishi, nyingine zipo kwenye hatua za kufanyiwa usafi. Kwa hiyo, niendelee kuiomba Serikali yangu ipeleke watumishi katika zahanati zilizoisha na zile ambazo hazijaisha Serikali izichukue ili imalizie ili wananchi tusiwavunje moyo kwa kazi yao kubwa waliyoifanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama kauli ya Serikali inavyosema kila Jimbo itajenga kituo cha afya kimoja, mimi katika Jimbo langu kituo hicho kijengwe katika kata ya Ngwelo kwani wananchi hawa ndiyo wanaopata taabu zaidi hasa katika kipindi cha mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama unavyofahamu Wilaya ya Lushoto ina Majimbo matatu na yote hayo yanaangalia hospitali moja ya Wilaya na Hospitali ile ni ndogo inahitaji kupanuliwa hasa vyumba vya mama wajawazito, vyumba vya mama na watoto. Pamoja na hayo x-ray na ultra sound ni ndogo sana hazina uwezo, ndiyo maana inafanya kazi kwa muda mfupi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Serikali yangu sasa ipeleke vifaa hivi ili hospitali iweze kutoa huduma inayoendana na kazi ya hospitali ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma hii ya afya ya uzazi na mtoto naiomba ifike vijijini hasa katika Jimbo la Lushoto wananchi wengi wanaishi ndani sana yaani vijijini mno. Kwa hiyo, naomba huduma hii ifike huko. Huko ndiko kuna wapiga kura wenye imani kubwa sana na Serikali yao ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo niishauri pia Serikali yangu haya mafungu yapelekwe vijijini, mfano, hizi asilimia tano hazifiki kabisa vijijini. Pamoja na hayo katika Mikoa ambayo itapelekewa mafungu, Mkoa wa Tanga sijaiona, naiomba Serikali yangu iangalie Mkoa wa Tanga nao uwe kwenye list ya kupata fedha hizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali yangu iweze kutoa ajira hasa kwa hawa maendeleo ya jamii, kwani hawa ni watu muhimu sana, wanahamasisha maendeleo vijijini kuliko ilivyo kuwa sasa ni wachache sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia niongelee suala la magari katika vituo vya afya pamoja dawa, vitu hivi ni muhimu sana kuwa katika vituo vyetu vya afya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia elimu ya UKIMWI ipelekwe zaidi vijijini kwani bado mpaka sasa kuna maeneo ya vijijini hawajapata elimu hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja, Mungu ibariki Tanzania, Mungu ambariki Rais wetu wa Tanzania.