Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante, ninaomba tena nitumie Kanuni Na. 60 (11) nichangie nikiwa nimekaa.
NAIBU SPIKA: Tafadhali endelea,
MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Naibu Spika ahsante, moja kwa moja nitaenda kwenye pongezi, napenda kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa utendaji wake mahiri, chini ya Rais wetu mpendwa John Joseph Pombe Magufuli. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, yaliyofanyika ni mengi siwezi kueleza moja moja, pia ninapenda nimshukuru Rais wetu kwa kusikia kilio cha watu wenye ulemavu kwa kutuhamishia Ofisi ya Waziri Mkuu, kilikuwa ni kilio chetu cha muda mrefu, tunashukuru kwamba alisikia ombi letu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaomba nijikite moja kwa moja kwenye masuala ya watu wenye ulemavu kwa sababu mengi yemeongelewa mambo ya maji watu wanaongelea, barabara, umeme na kadhalika.
Moja kwa moja ninaomba niongelee suala la elimu kwa watu wenye ulemavu. Katika sehemu hii ya elimu ninaiomba Serikali iangalie ni kwa jinsi gani ambavyo inaweza ikawasaidia watu wenye ulemavu hasa katika suala zima la kuongeza shule ambazo ni maalum na ambazo watu wenye ulemavu wanaweza wakapata elimu pasipo kipingamizi chochote. Ukiangalia suala zima la kusema kwamba majengo yaongezwe inaweza ikawa ni ngumu, lakini naiomba Serikali iboreshe majengo yaliyopo kwa upande wa miundombinu pamoja na walimu ili watu wenye ulemavu waweze kupata elimu pasipo vikwazo vyovyote.
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia ninaomba nizungumzie suala la mikopo kwa watu wenye ulemavu vyuoni. Mimi pendekeza kwa Serikali kwamba kusiwe kuna vipingamizi kwa mtu mwenye ulemavu kupata mkopo ambaye tayari amechaguliwa na chuo fulani kujiunga hapo. Ninaomba sana Serikali iliangalie hili suala la mikopo ili kusiwe kunakuwa kuna vikwazo kwa watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ninaomba niongelee suala la ajira. Katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri Mkuu, ukurasa wa 18 ameongelea suala la ajira lakini ametoa takwimu za vijana. Katika sehemu hii haioneshi kwamba Serikali inatekeleza vipi ile Sheria Na. 9 ya mwaka 2010 kwa upande wa ajira kwa watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, ninaiomba Serikali iangalie ni kwa jinsi gani ambavyo Sheria hii ya mwaka 2010 inatekelezwa hasa katika suala zima la ile asilimia tatu kwamba kila mwajiri awe na asilimia tatu ya watu wenye ulemavu katika wafanyakazi wake.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia ninaomba niongelee suala la mauaji kwa wenzetu wenye ulemavu wa ngozi. Suala hili kwanza napenda niishukuru Serikali na kuipongeza kwa jinsi ambavyo mauaji haya yamepungua kwa kiasi kikubwa, lakini bado kuna taarifa ambazo zinaendele kuripotiwa za kupotea kimya kimya kwa hawa wenzetu wenye ulemavu wa ngozi. Ninaiomba Serikali pamoja na ulinzi ambao inatupatia, pia ijikite katika suala nzima la elimu kwa jamii yetu. Pia niwaombe Waheshimiwa Wabunge katika Majimbo yao wanapopata fursa ya kukaa na wapiga kura wao watoe elimu hii kwa jamii kuhusiana na suala zima la mauaji kwa watu wenye albinism.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niongelee suala la kodi kwenye mishahara ya waajiriwa ambao wana ulemavu. Tumeona kwamba mishahara ya waajiriwa wenye ulemavu imekuwa ikikatwa kodi ninaiomba Serikali iondoe suala zima la kodi kwenye mishahara ya watu wenye ulemavu. Kama tunavyofahamu kwamba ulemavu ni kikwazo, sasa unapokata tena ile kodi ina maana kwamba unampunguzia huyu mtu uwezo wa hata kumwezesha kumpa posho mtu ambaye ni msaidizi wake. Kwa hiyo, ninaiomba Serikali iondoe kodi kabisa kwenye mishahara ya waajiriwa ambao ni walemavu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie suala zima la vyombo vya usafiri ambavyo vinaagizwa na watu wenye ulemavu. Kumekuwa kuna sheria kwamba ili mlemavu asamehewe kodi ya chombo alichokiagiza ni mpaka kile chombo kiwe kina vifaa maalum kwa ajili ya watu wenye ulemavu. Binafsi ni mlemavu, lakini mimi huwa naweza kuendesha gari yoyote ambayo ni automatic, kwa hiyo, ninaomba sheria hii irekebishwe mradi tu kwamba mtu aliyeagiza kile chombo ni mlemavu basi ile kodi asamehewe siyo mpaka kile chombo kiwe na vifaa maalum kwa watu wenye ulemavu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la malipo ya road license kwa vyombo vya watu wenye ulemavu. Naomba Serikali itusamehe kodi hii ya barabara katika vyombo ambavyo tunavitumia sisi watu wenye ulemavu, kwa sababu hili suala lipo ndani ya uwezo wa Serikali ninaamini kabisa kwamba inaweza ikaondolewa na vyombo hivi tukawa hatulipi hii road license badala yake tukawa tunalipa tu insurance.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la Mfuko wa Watu Wenye Ulemavu. Mfuko huu ninajua kwamba upo na ulishaanzishwa, ninaiomba Serikali kama vile ambavyo imekuwa ikitenga pesa kwa ajili ya barabara, pesa kwa ajili ya umeme, pia Serikali itutengee fungu maalumu kwenye huu mfuko ili huu mfuko uweze kutusaidia sisi watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nizungumzie suala zima la Halmashauri na Manispaa hasa kwa wale watu wenye ulemavu ambao hawana kipato chao kujitosheleza.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika eneo hili Wakurugenzi wa Halmashauri na Manispaa wafanye utambuzi wa watu wenye ulemavu ambao hawajiwezi na baada ya kufanya utambuzi huu waweze kuwapatia zile shughuli ambazo zinapatikana kwenye Halmashauri zao ikiwemo shughuli mbalimbali kama kuzoa takataka, vyoo vya city, hili limefanyika katika Halmashauri ya Ilala kuna choo kimoja ambacho walitengewa watu wenye ulemavu, kwa hiyo hawa watu wenye ulemavu ambao walikuwa wanaomba barabarani, walikuwa wanapita pale kila asubuhi mtu anachukua shilingi 1,000 kwa sababu kile choo kilikuwa kina uwezo wa kupata shilingi 250,000 kwa siku, hivyo ilipunguza kwa kiasi kikubwa wimbi la ombaomba wenye ulemavu katika eneo lile.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika Halmashauri kuna ile asilimia ambayo inawataja wanawake na vijana tu, nilikuwa ninaomba asilimia hii iweze pia kuwataja na watu wenye ulemavu ili weweze kunufaika isiwe general, iwataje na wao kama vile ambavyo inataja vijana na wanawake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema haya ninaunga mkono bajeti hii ambayo ipo mbele yetu, ahsante.