Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. AMINA S. MOLLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, mojawapo ya malengo ya milenia ilikuwa ni kupunguza vifo vya wanawake wajawazito, watoto wachanga pamoja na watoto walio chini ya umri wa miaka mitano. Pamoja na kuwepo lengo hili, Tanzania bado tuna changamoto kubwa ya vifo vya wanawake na wajawazito pamoja na watoto wachanga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri, ukurasa wa 16 ameeleza na kuthibitisha kuwa vifo hivi bado ni changamoto kubwa, ambapo kwa mwaka 2015 idadi ya vifo ilikuwa 556 kwa kila vizazi hai 100,000. Hili ni tatizo kubwa ambalo linahitaji nguvu ya pamoja kati ya wanawake na wanaume. Wanaume wakielimishwa na wakawa karibu na wake zao kuna uwezekano mkubwa wa kupunguza vifo hivi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mila potofu katika jamii zetu ni tatizo. Kwa mfano katika baadhi ya makabila mwanamke mjamzito hawezi kwenda kujifungulia hospitali mpaka apate ruhusa ya mama mkwe au wifi ndipo aende hospitali au kwa waganga wa kienyeji. Hili ni tatizo na elimu ni muhimu kutolewa kwa jamii hizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Mkoa wa Arusha takwimu zinaonesha kuwa vifo vya wajawazito vimeongezeka kwa asilimia 31 kutoka vifo 49 kwa mwaka 2015 na kufikia vifo 72 kwa mwaka 2016. Kwa upande wa vifo vya watoto kwa mwaka wa jana kulikuwa na vifo 978 waliopoteza maisha sawa na kifo kimoja kwa kila vizazi hai 1,000.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya vifo hivi ni kutokana na upungufu wa vituo vya afya katika Halmashauri za Mkoa wa Arusha ambapo kwa jamii za wafugaji kama inavyoeleweka wanaishi mbali na miji, hivyo naomba Wizara isaidie kwa kutimiza Ilani ya Chama cha Mapinduzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa WHO duniani kote hasa nchi zinazoendelea wanawake 300,000 hufa wakati wa ujauzito na wakati wa kujifungua, na zaidi ya watoto milioni mbili hufa katika siku 28 za mwanzo na wengine zaidi ya milioni mbili wakiwa si riziki. Kwa upande wa watoto takwimu za WHO zinasema kuwa watoto wachanga na wale wanaozaliwa wanakufa. Vifo hivi vinaweza kuzuilika kwa kuwa na huduma bora za afya wakati wa ujauzito na kujifungua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa bahati mbaya sana vifo vinavyorekodiwa ni kwa wale tu wanaofika hospitali na wengi hujifungua majumbani kutokana na umbali pamoja na mila na desturi.