Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Rose Cyprian Tweve

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kuchangia. (Makofi)

Awali ya yote naomba nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri Dada yangu Ummy na Mheshimiwa Kigwangalla, mmekuwa mabalozi wazuri, kweli hilo jina linawafaa. Ni matarajio yangu Watanzania hasa wanawake na watoto wanatambua na wanajivunia mchango mkubwa ambao mnautoa kwenye Wizara yenu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba niende moja kwa moja kwenye hotuba ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 55 anasema: “Maendeleo endelevu ya Taifa lolote yanategemea uwekezaji katika makuzi, malezi na maendeleo ya mtoto. Kwa mujibu wa sensa ya watu na makazi ya mwaka 2012 idadi ya watoto ni asilimia 51.6 ya Watanzania wote.”

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi ambazo zimepiga hatua, zilifanya jitihada za makusudi kuhakikisha zinawekeza kwenye hii rasilimali watu. Kwa hiyo, kwa hotuba hii Mheshimiwa Waziri naungana na wewe kabisa kuwa ni jukumu letu kama Taifa kuhakikisha kuwa tunawatengenezea mazingira mazuri hii asilimia 51.6, kwa sababu tunasema tunataka Tanzania iweze kufika uchumi wa kati na hii ndiyo nguvu kazi ambayo itatusaidia kuweza kufika hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na utafiti ambao umefanywa na World Health Organization wakishirikiana na World Bank wanasema, Taifa kama tunataka kuhakikisha tunawekeza kwenye watoto umri ambao unafaa ni kuanzia mwaka sifuri mpaka miaka miwili. Sasa Mheshimiwa Waziri nikupongeze kwa kuleta takwimu hizi, imetupa picha kamili kuwa sasa ni zaidi ya nusu ya Watanzania ni watoto. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu ningependa turudi nyuma kwa kutumia huu utafiti na ushauri ambao umetolewa na World Health Organisation. Turudi nyuma sasa tujue katika hii asilimia 51.2 ni watoto wangapi wako kwenye umri wa mwaka sifuri mpaka miaka miwili, kwa sababu hii ni critical age ndiyo maana wamesema kama Taifa tunatakiwa kuanza kuwekeza hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini tunasema ni critical? Kama hotuba yako ambavyo inaonesha mortality rate ya watoto wa mwaka sifuri mpaka miwili ni kubwa sana, tunapoteza watoto 21 kwa kila watoto 1,000 wanaozaliwa.

Pia umekiri kabisa kuwa udumavu ni tatizo kubwa sana kwa Taifa letu, tumekuwa na watoto ambao uelewa wao unakuwa ni mdogo sana. Tunajua kabisa tatizo la udumavu linafanya mtoto ashindwe kufikiri, kutunza kumbukumbu na hata kufanya maamuzi inawawia vigumu sana.
Kwa hiyo, Mheshimiwa Waziri tuna kazi kubwa kama taifa kuhakikisha tunalinda hawa watoto wetu ili tuweze kufikia malengo hayo ya uchumi wa kati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo kwa Serikali yatakuwa kama yafuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tulivyosema hii age ya mwaka sifuri mpaka miwili ni critical na tunataka tuwe na watoto ambao wataweza ku-grasp hizi concept, sasa hivi kumekuwa na frustration. Mtoto anakwenda shuleni, mwalimu ameandaliwa na tumetengeneza miundombinu mizuri lakini watoto hawa bado wanashindwa ku-grasp hizi concept zinazofundishwa shuleni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Serikali na kama wizara naomba tupitie hizi sheria, tuzilete hapa ili tuweze kufanya mabadiliko na tunaweza tukaanza kidogo tu, hizi maternity leaves tunazipuuzia, tunasema zipo vizuri, hazipo vizuri, ukiangalia nchi ambazo zimeendelea kwa mfano, Scandnavian countries wanatoa kipaumbele kikubwa sana kwa wamama wajawazito, si ndiyo. Wengine wanapewa hadi siku 480 sisi hapa bado ni siku 120, siku hizi hazitoshi kwa sababu tunatakiwa kumlinda huyu mama ili aweze kumlea mtoto wake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze juhudi za Serikali za kuhakikisha tunatoa elimu kwa mama mjamzito juu ya lishe ya motto, lakini hii haitoshi tunatakiwa kwenda mbali zaidi. Tumesema kuna viwanda…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ROSE C. TWEVE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja nitaleta mapendekezo yangu kwa maandishi. Ahsante sana.