Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Amina Saleh Athuman Mollel

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. AMINA S. MOLEL: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi nami niweze kuchangia Hotuba ya Waziri Mkuu kuhusu mapitio na mwelekeo wa Serikali na Makadirio ya mapato na matumizi kwa Wizara husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, naomba nitoe shukrani zangu za dhati kwa Ofisi yako wewe mwenyewe, kwa maana ya Ofisi ya Spika, kwa jitihada zake za kuhakikisha kwamba masuala ya watu wenye ulemavu yanafanyiwa kazi. Pia pongezi za kipekee kabisa zimwendee Mheshimiwa Waziri Mkuu ambapo amekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kwamba haki za watu wenye ulemavu zinatimizwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue nafasi hii nitoe pongezi za dhati kabisa kwa Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Rais amefungua milango na kuthamini haki za watu wenye ulemavu kwa kuona kwamba kuwa na ulemavu siyo kulemaa na ndiyo maana leo hii katika Idara mbalimbali watu wenye ulemavu wamepewa nafasi kuonesha uwezo wao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nimpe pongezi za dhati kabisa kwa kuhakikisha kwamba Wizara yetu inahamishiwa Ofisi ya Waziri Mkuu. Hiki kilikuwa ni kilio cha watu wenye ulemavu kwa muda mrefu. Kana kwamba hiyo haitoshi ni furaha iliyoje kuwa na Naibu Waziri katika Wizara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba ya Waziri Mkuu imejitosheleza. Ni hotuba ambayo imegusa maeneo yote. Sisi watu wenye ulemavu tunaona ni fahari kubwa kwa sababu masuala yetu mengi yamezungumzwa na yameguswa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo, naomba tu nishauri mambo machache ambayo naamini kabisa kwa jitihada zilizoanza kutekelezwa na Serikali ya Awamu ya Tano mambo haya yatafanyiwa kazi hasa katika suala la elimu. Naomba nitoe mapendekezo yangu kwa Serikali hasa kipindi hiki ambapo Mheshimiwa Rais ametoa kipaumbele cha elimu na kuhakikisha kwamba watoto wa Kitanzania wanasoma bure, ni jambo muhimu sana kuhakikisha kwamba sasa ni wakati wa kuboresha miundombinu ili watoto wenye ulemavu waweze kupata elimu pasipo vikwazo vyovyote. Pia ni wakati muafaka sasa kuboresha vyuo vyetu ili kuhakikisha kwamba navyo mazingira yanakuwa rafiki kwa watu wenye ulemavu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa mambo mengi yameorodheshwa humu na kwa kuwa matarajio yetu katika Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ni pande zote mbili kugusia mambo haya ya watu wenye ulemavu ambayo siku zilizopita yalikuwa nyuma sana, lakini sasa tumeona yanapewa kipaumbele. Tulitarajia Kambi ya Upinzani pamoja na vyama vingine vyote ambavyo vinawakilishwa hapa Bungeni vingekuwa mstari wa mbele kuunga mkono hotuba hii kwa kushauri ili kuboresha kwa namna moja au nyingine na kuhakikisha masuala ya watu wenye ulemavu yanasonga mbele na kuendana na kasi ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ya hapa kazi tu. Ni jambo la kuhuzunisha hasa tukizingatia kwamba tunapokuja hapa Bungeni tunategemea kupata mambo yenye msingi, matokeo yake upande wa pili unatoa vitu ambavyo haviendani na wakati uliopo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la vyombo vya habari kurusha moja kwa moja matangazo ya Bunge ndiyo hoja yao hivi sasa. Tunapozungumzia suala zima la habari, habari zinapatikana wakati wowote na katika matukio yoyote muhimu. Hatujaona vyombo vya habari kama vimekatazwa kurusha habari na matangazo yanaendelea kutolewa Mheshimiwa Mwenyekiti, kinacholiliwa hapa ni kule kurushwa habari moja kwa moja. Hata ukiangalia katika Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania hakuna sehemu ambayo imezuia kurusha matangazo ya Bunge na matangazo haya yanaendelea kurushwa. Hata kama hayajarushwa moja kwa moja lakini si yanaendelea kurushwa kwa wakati mwingine? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nafikiri ni wakati muafaka wa kujiuliza ni kwa nini wenzetu wanalilia matangazo haya kurushwa moja kwa moja. Pengine ni kutokana na ajenda zao kwa hivi sasa zimeweza kufanyiwa kazi kwa kiasi kikubwa na Serikali ya Awamu ya Tano na kujikuta hivi sasa hawana la kusema. Ndiyo maana hata wakati mwinginge wanaona kwamba ni bora wafanye yale ambayo yamefanyika na tumeshuhudia leo hii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, yale masuala ya ufisadi waliyokuwa wakiyapigia kelele hivi sasa mafisadi wanashughulikiwa. Wamekuja hapa na kuzungumzia kuhusiana na matumizi ya fedha ambazo hizi fedha Waziri mwenye mamlaka husika sheria inamruhusu. Ni kwa vipi sheria inamruhusu, hivi hata nyumbani baba anapotoa fedha na zikabaki zikatumika kwenye matumizi mengine kuna ubaya? Katika sheria hii ambayo tumewasikia leo wakizungumzia ya Appropriation Act ya mwaka 2016 iko wazi kuhusiana na Waziri kutoa Fedha na kwenda kutumika sehemu nyingine. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tumeona Sherehe za Uhuru fedha zile zimetumika kutengeneza barabara ya Mwenge, kuna ubaya gani? Vile vile tumeona fedha za Muungano zitatumika kufanyia ukarabati barabara ya kwenda uwanja wa ndege kule Mwanza. Katika hili Serikali inapoamua kutekeleza mambo muhimu ambayo yataleta unafuu kwa wananchi hivi tatizo liko wapi? Ajenda yao hapa ni nini? Tumeona jitihada za Rais katika kutumbua majipu. Nafikiri kwa upande mwingine hata hawa pia ni majipu ambayo yanapaswa kutumbuliwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine wanapozungumzia utawala bora hapa Tanzania ni Serikali ya Chama cha Mapinduzi imekuwa ikilivalia njuga suala hili na utawala bora upo, upo kwa maana gani? Hebu tuangalie hata katika vyama vyetu. Katika Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tumeshuhudia kabisa kwamba kila kipindi cha miaka mitano uchaguzi upo, miaka kumi uchaguzi upo na hata Rais anayekuwa Mwenyekiti katika chama husika anapomaliza muda wake unafanyika uchaguzi. Hata hivyo, tangu upinzani umeanza hapa nchini hebu tuangalie hawa Wenyeviti kwa muda wote wamekuwa Wenyeviti wa vyama hivyo na wao ndiyo wa kwanza kuzungumzia demokrasia, lakini ndiyo wavunjaji wa demokrasia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunapozungumzia Upinzani kwa chama cha CUF, tangu kimeanza Maalim Seif ndiye Mwenyekiti, hivi hakuna wengine ambao wana sifa za kuwa Wenyeviti?
MHE. AMINA S. MOLEL: Kuwa Katibu Mkuu, amekuwa Katibu Mkuu kwa muda wote kwani hakuna wengine wenye sifa?
Sasa mnazungumzia demokrasia ipi? Ni demokrasia ipi mnayoizungumzia wakati ninyi ndiyo wa kwanza kuivunja hiyo demokrasia?
Mheshimiwa Mwenyekiti, linapokuja suala la uongozi wakati mwingine Mwenyezi Mungu ndiye anayeteua viongozi…
MHE. AMINA S. MOLEL: Siyo kila mtu tu atakuwa kiongozi, siyo kila mtu tu atakuwa Rais, miaka yote hujawa Rais basi achia ngazi wapishe wengine. Mnafurahisha sana, mlisusa uchaguzi, uchaguzi umefanyika wa haki, halali kabisa mmewaumiza wengine ambao hivi sasa wanalia ambao kwa namna moja au nyingine wangeweza kuendeleza Taifa hili, lakini leo hii mmewazuia. Kwa maana hiyo ninyi ndiyo wa kwanza kuvunja demokrasia kwa sababu hamuitimizi hiyo demokrasia.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimwombe tu Rais wetu na tuzidi kumpa moyo, aendelee kufanya kazi, aendelee kuyatumbua majipu, Watanzania wanayaona. Wanaona jitihada za Rais, wanaona jitihada za Mawaziri wetu, kazi kubwa wanayoifanya na hicho ndicho tunachokihitaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati mwingine wanasema kelele za chura hazimzuii ng’ombe kunywa maji. Naomba kuwatia moyo muendelee kufanya kazi, kazi inaonekana na wananchi wanaifurahia, kila siku umaarufu wao unazidi kushuka. Tunapoelekea sasa mwaka 2020 ni dhahiri kabisa hizi row ambazo hivi sasa mmeongezeka zitapungua kwa sababu matarajio makubwa ya wananchi ni kufanyia kazi matatizo yao, lakini hivi sasa mmekwenda kinyume kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naomba kuunga mkono hoja, naomba kuwapa moyo Mawaziri wetu, naomba kumpa moyo Waziri Mkuu, naomba kumpa moyo Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na tunamwomba aendelee kufanya kazi kwa mwendo huo huo. Kauli mbiu ya hapa kazi tu iendelee isirudi nyuma, tunachotaka sisi ni maendeleo. Wananchi kwa muda mrefu walikuwa na kero nyingi hivi sasa basi hizo kero ziweze kufanyiwa kazi, ahsante sana.