Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Leah Jeremiah Komanya

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi hii kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu jioni hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa vile ni mara yangu ya kwanza kuchangia, naomba niwashukuru akinamama wa Mkoa wa Simiyu walioniwezesha kuingia katika Bunge hili. Pia, naomba niwashukuru wananchi wote wa Mkoa wa Simiyu waliokichagua Chama cha Mapinduzi nafasi ya Ubunge kwa asilimia mia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda niipongeze Serikali ya Awamu ya Tano kwa namna inavyofanya kazi ya kutumbua majipu. Wananchi wa Simiyu wana imani na Serikali na wanaiunga mkono. Hii imejidhihirisha katika ziara ya Waziri Mkuu aliyoifanya mapema mwezi wa Tatu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo naomba niombe yafuatayo katika bajeti ya mwaka huu. Mkoa wa Simiyu ni mpya una changamoto nyingi na changamoto moja ni ukosefu wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa. Wananchi wanalazimika kusafiri umbali wa kilomita zaidi ya 100 wakifuata huduma hiyo Mkoa wa Shinyanga ama Mwanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishukuru Serikali katika bajeti yake ya mwaka 2015/2016, ilitoa fedha kidogo kwa ajili ya uanzishaji wa jengo la mapokezi. Naomba katika bajeti hii pia Serikali itenge fedha za kutosha ziweze kujenga hospitali hiyo na iweze kukamilika na kuanza kutumika. Hospitali hii itasaidia kuondokana na tatizo la mama wajawazito wanapopata dharura za kujifungua kusafiri zaidi ya kilometa 100 na hali barabara zetu zikiwa na ubovu hasa katika kipindi cha mvua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali katika kuharakisha maendeleo katika uchumi wa viwanda pamoja na maandalizi mengine ni vyema Serikali ikaona haja sasa ya kuandaa mafundi mchundo wa kutosha ambao watahitajika kwa wingi katika viwanda vyetu. Mafundi hao wanaandaliwa na VETA zilizopo katika wilaya na mikoa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kutoa masikitiko yangu, Mkoa wa Simiyu hauna Chuo cha VETA hata kimoja katika wilaya ama mkoa kwa ujumla. Naomba Serikali kupitia bajeti hii iweze kuuona Mkoa wa Simiyu ili hata vijana wetu waweze kupata mafunzo ya ufundi stadi ambayo pia yatawasaidia kujiajiri wenyewe. Pia chuo hicho kitaweza kusaidia kutoa ushindani katika kazi ambazo sasa halmashauri zinapaswa kutenga 30% ya kazi za zabuni kwa ajili ya vijana wetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile naiomba Serikali katika kufanya uchaguzi wa wanafunzi wanaoenda kidato cha tano kuwepo pia na uchaguzi wa wanafunzi watakaokwenda katika vyuo vya VETA. Hii itasaidia kuwepo na uhakika na wanafunzi katika vyuo vya VETA, pia itasaidia kuondoa ile dhana kwamba wanaoenda VETA ni wale waliofeli kuendelea na kidato cha tano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichangie upande wa nishati ya umeme. Ni dhamira ya Serikali kuwezesha upatikanaji wa umeme wa uhakika unaokidhi mahitaji na wenye gharama nafuu ili kusukuma mapinduzi ya viwanda kwa kasi zaidi. Wilaya ya Meatu iko nyuma sana katika usambazaji wa umeme wa vijijini wa REA ukilinganisha na maeneo mengine. Wilaya ya Meatu ina vijiji 109 na Majimbo mawili, lakini ni asilimia 19 tu ya vijiji vilivyopata umeme. Niiombe Serikali yangu sikivu iangalie kwa jicho moja Wilaya ya Meatu iweze kusambaziwa umeme huo wa REA. Umeme huo utawasaidia wanafunzi wetu tunaowaandaa kuweza kujisomea vizuri na kuepukana na vibatari wanavyotumia. Umeme pia utawasaidia wananchi wetu waweze kununua mashine za kukamua alizeti na kuweza kujipatia kipato na kujikwamua kutoka katika umaskini tulionao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba pia nichangie kuhusu upatikanaji wa maji salama. Natambua Serikali katika Mpango huu wa Miaka Mitano imepanga kuleta maji kutoka Ziwa Viktoria kwa kupitia Wilaya ya Busega, Bariadi, Itilima, Maswa na Meatu lakini maji haya yata-cover vijiji vilivyo ndani ya umbali wa kilomita 12. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mkoa wa Simiyu una changamoto ya upatikanaji wa maji. Kuna ukanda ambao unahitaji mabwawa kama vile ukanda wa Meatu. Tunaomba Serikali kwa maeneo ambayo hayatafikiwa na Mradi wa Maji toka Ziwa Victoria, ichimbe mabwawa zaidi katika Wilaya ya Meatu kuliko visima vya maji ambavyo vinakauka wakati wa kiangazi. Hata maji hayo yakipatikana huwa ni ya chumvi. Kanda zingine kama za Itilima, Kisesa, Bariadi, Busega, Maswa Serikali iendelee kuchimba visima virefu kwa ajili ya upatikanaji wa maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono sana hoja kwa asilimia mia moja. Ahsante