Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Halima Ali Mohammed

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. HALIMA ALI MOHAMMED: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana. Awali ya yote nichukue nafasi hii nimshukuru Mwenyenzi Mungu mwingi wa rehema na utukufu kwa kutujalia afya njema. Ninakushukuru wewe kwa kunipatia nafasi hii ili na mimi niweze kutoa mchango wangu katika mada iliyoko mbele yetu. Namwomba Mwenyenzi Mungu amjalie maisha marefu Katibu Mkuu wa Chama cha CUF Maalim Seif Sharif Hamad ili aweze kuwatumikia Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuzungumzia kuhusu hoja ya haki za watoto. Tanzania tumekuwa tukiridhia mikataba mbalimbali inayohusiana na haki za watoto, kama Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa mwaka 1989, vilevile kuna Mkataba wa Haki za Mtoto wa Afrika ambao umeridhiwa mwaka 1979, lakini Tanzania tuna sheria inayomlenga mtoto wa Tanzania sheria hii imepitishwa katika mwaka 2009.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimekusudiaKuna watoto wengi wa Kitanzania watoto hawa aidha baba ama mama wamehukumiwa jela kifungo cha muda mrefu ama wazazi hawa wako rumande kwa muda mrefu. Sasa watoto hawa wanakosa haki zao za msingi kwa mujibu wa sheria ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimejaribu kuangalia sheria, sheria hii imekaa kimya kuhusiana na mtoto ambaye mzazi wake mmoja ma wote wawili wako gerezani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wetu wanasoma, watoto wetu tunawatibia vizuri, watoto wetu wanacheza wanafurahi lakini watoto wa Watanzania hawa wanakosa haki zao za msingi. Sasa nilikuwa naiuliza Serikali je, imefanya utafiti kwa kiasi gani kuhakikisha kwamba watoto hawa wa Kitanzania nao wanapatiwa haki zao za msingi kwa mujibu wa Katiba? (Makofi)

Je, kwa sasa Serikali watakubaliana na mimi ili watoto hawa waweze kupatiwa haki zao za msingi kwa mujibu wa sheria za nchi hii? Hilo ni jambo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, naomba nizungumzie suala la uzazi salama. Uzazi salama umeshazungumziwa hapa kwa Wabunge waliotangulia na mimi nazungumzia, nawaomba na Wabunge wengine walizungumzie suala la uzazi salama. Takwimu zinaonyesha wanawake wengi wanapoteza maisha wakati wakitimiza jukumu lao la kuleta watoto duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, takwimu za hivi karibu ni kwamba wazazi 30 wanapoteza maisha kila siku. Sasa idadi hii ni idadi kubwa na inawezekana kwamba idadi hii ni wale ambao wanajifungulia sehemu husika ambao ni zahanati, vituo vya afya na hospitali. Lakini kuna idadi kubwa ambayo wanajifungulia vijiji, huko ambako wanakosa huduma halisia. (Makofi)

Kwa hiyo, napendekeza kwa Serikali yenye kusikia kwamba bajeti basi ya Wizara ya Afya iweze kuongezwa kwa maksudi ili kuokoa vifo vya wajawazito wakati wa kujifungua, ahsante.