Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Susan Anselm Jerome Lyimo

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. SUSAN A. J. LYIMO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru sana kwa kunipatia fursa hii na mimi niweze kuchangia kwenye hoja muhimu sana ya afya za Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiri tu kwamba na mimi ni Mjumbe wa Kamati hii, kwa hiyo mambo mengi yanayozungumzwa kwa kweli yananifurahisha na niseme tu kwamba Wizara inajitahidi, lakini Serikali inashindwa kupeleka fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haiwezekani kwa Taifa kubwa kama Tanzania, lenye watu zaidi ya milioni 50, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto hii ndiyo ambayo imeshika jamii nzima nazungumzia hasa Fungu namba 53.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kusikitisha kwa mwaka unaoisha Wizara hii ya Maendeleo ya Jamii nikiondoa Fungu lile la Afya wametengewa fedha za maendeleo mpaka sasa hivi zilizoenda ni asilimia 2.3. Hii ni aibu kubwa mno, hivi tuaacha kuwaona watoto wa mitaani, tuaacha kuwaona watoto wadogo wenye mimba changa?(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara hii ni Wizara inayoshughulikia wazee, niseme tu labda ndiyo sababu mvua hazinyeshi na zikinyesha zinanyesha za mafuriko, kwa sababu nchi hii ni kwamba tumelaaniwa na wazee. (Makofi)

Nimepita hapo nje kuna bango la Wizara ya Afya linasema “Mzee Kwanza,” na linasema “Mzee alikuwa kama wewe na wewe utakuwa kama huyo mzee.” Ajabu ukiangalia hotuba nzima ya Waziri ameongelea kidogo sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kubwa zaidi hapa nina hotuba ya Waziri ya mwaka jana alizungumza na alisema mwaka huu wa wataleta Sheria ya Wazee. Mwaka huu hakuna chochote kinachozungumzwa kuhusu Sheria ya Wazee. Wakati Sera ya Wazee inapita toka mwaka 2003 leo ni mwaka wa 14, hakuna Sheria ya Wazee na ndiyo sababu leo wazee wanauawa kwa sababu hakuna sheria inayowasimamia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba kwa kuwa Mheshimiwa Waziri mwaka jana alisema na siyo mara moja, amekuwa akijibu maswali hapa kwamba sheria italetwa, leo kwenye kitabu chake chote hakuna jambo lolote linalozungumzia kuhusu sheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunajua wazee wa Taifa hili wamelitumikia Taifa hili wametusaida kuleta uhuru, lakini wazee hawa wametelekezwa. Makazi yao hayaeleweki, chakula wanachokula ni taabu, kubwa zaidi naomba Serikali sasa ituambie ni lini inaleta Sheria ya Wazee, ili wazee wa nchi hii waweze kujua haki zao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye Wizara ya Afya. Wizara ya Afya, afya ndiyo jambo la msingi, afya ndiyo utajiri kama ambavyo Mahatma Gandhi amesema. Utajiri namba moja ni afya zetu wananchi. Unapokuwa na afya njema ndiyo unaweze kujenga Taifa. Afya za Watanzania ziko mashakani na ninasema hivi kwa sababu fedha hazijaenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hospitali kama ya Muhimbili ni hospitali ya Taifa, ilikuwa inaomba shilingi bilioni tano kwa ajili ya vifaa tiba hawajapewa hata senti tano. Hospitali ya KCMC imeomba shilingi bilioni nne hawajapewa hata senti tano. Hospitali ya Bugando kwa ajili ya mashine ya Kansa haijapewa fedha, tunategemea nini? Kubwa zaidi Hospitali ya Jakaya Kikwete ambayo inafanya kazi kubwa sana ya kutibu wagonjwa wa moyo, ambayo inasaidia sana kupunguza gharama za kwenda nje, lakini taasisi ile haijapewa fedha. Pamoja na kwamba Mawaziri inawezekana wanajitahidi sana, lakini fedha hakuna. Tunafanyaje? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba kama mwaka jana tulitoa shilingi trilioni 28 zimeshindwa kwenda japo asilimia 50 za fedha za maendeleo, leo tunaongeza tunasema shilingi trilioni 33 hizo hela zinatoka wapi. Kwa hiyo, jambo ambalo linashangaza hata zile fedha zetu za ndani bado haziendi tatizo liko wapi? Au mnatudanganya kwamba mnakusanya sana lakini fedha hazipo. Hili jambo kwa kweli linatutia wasiwasi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo jingine ambalo ninapenda kuzungumza ni suala la madaktari walioajiriwa juzi. Hapa nina barua mbili kutoka TAMISEMI kwa ajili ya hawa madaktari. In fact, walikuwa waje Dodoma Chuo cha Mipango kwa ajili ya semina elekezi na wafike kabla ya tarehe nane, baadaye kuna barua nyingine inasema waende moja kwa moja. Hii imetoka juzi tarehe Mosi, waende moja kwa moja kwenye vituo, jana tena Dkt. Chaula ameandika barua nyingine waende moja kwa moja kwenye Halmashauri, huko kwenye Halmashauri watafutiwe sehemu za makazi na fedha. Hivi najiuliza hizo Halmashauri tayari zimetengewa hizo fedha au mnataka hawa madaktari waende huko kama ambavyo walimu wanateseka, wanafika wanaolewa na Wenyeviti wa Mitaa au viongozi wa kata. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vizuri sana tunahitaji kweli madaktari, kama ambavyo Kambi ya Upinzani imesema, sielewi inawezekanaje Rais tu ndiyo aseme baada ya hao madaktari kushindwa kupokelewa kule Kenya, leo anatoa kibali kwa hawa madaktari 258. Je, hawa 3,000 walioko mitaani wanakwenda wapi? Ndiyo sababu Kambi ya Upinzani inasema je, huu siyo ubaguzi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hawa wasingekuwa wamejiandikisha kwenda Kenya ina maana leo wasingeajiriwa, kwa hiyo kuna haja ya Serikali kuwa na mipango thabiti ya ajira ya watu wake na siyo kusubiri watu waende mahali fulani, wanatakiwa kwenda nchi fulani wakikosa ndiyo Serikali inawapa ajira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu ni kwamba hawa madaktari wamesomeshwa kwa gharama kubwa sana, kwa maana hiyo, ni lazima kama wanapelekwa mahali kwenda kufanya kazi maandalizi ya kina yawe yamefanyika ili wasije kuwa frustrated. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie nadhani hiyo ni bado dakika tano. Pamoja na kwamba nia njema haikuwepo ya kupeleka madaktari hawa, kwa sababu wote tunajua Kenya ina madaktari wengi kuliko Tanzania, World Health Organization inasema kwamba daktari mmoja Kenya anahudumia wagonjwa 16,000 wakati Tanzania daktari mmoja anahudumu watu 20,000. Kwa hiyo, hainiingii akilini ni sawa na mgonjwa yuko ICU halafu na mwingine ana nafuu unasema daktari ampe dawa yule mwenye nafuu amwache yule ambaye amezidiwa. Kwa hiyo, hili jambo halikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niongelee suala la ndoa za utotoni. Pamoja na kwamba sheria yetu inakinzana lakini hatuwezi kuvumilia watoto wa kike wakiendelea kupata mimba za utotoni, maana yake ni kwamba Serikali inaruhusu mimba za utotoni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kwamba tunajua kuna watoto wengi wako mitaani, rai yangu ni kwamba lazima tulete sheria hiyo, tuipitishe na nina hakika Mheshimiwa Ummy ulikuwa mstari wa mbele katika hili naomba usirudi nyuma. Suala la imani kweli lipo, lakini tuangalie madhara makubwa ambayo wanayapata watoto wa kike na yameshazungumzwa mengi na wewe unayafahamu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa kweli Serikali kupitia Wizara hii na Wizara ya Sheria na Katiba walete sheria hiyo ili tuibadilishe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa ni kuhusu Benki ya Wanawake. Ukiangalia katika randama benki hii ilikuwa inatakiwa kila mwaka ipewe shilingi bilioni moja, bado Serikali imetoa kwa mwaka huu shilingi milioni 69.

Jamani hivi kweli tunataka kuwawezesha wanawake mdogo wangu Mheshimiwa Ummy? Kama hii benki kwanza moja ipo Dar es Salaam na sehemu chache sana, tunataka benki hii iende maeneo yote. Wanawake ni wengi sana nchi hii na wanaume. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana naunga mkono hoja ya Kambi ya Upinzani pamoja na Kamati yangu ya Maendeleo ya Jamii.