Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii nichangie Wizara hii ya Afya.

Awali ya yote nitoe shukrani zangu za dhati kwa Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu wa Wizara hii kwa haki walioyonitendea katika kipindi hiki. Mwaka jana nilisimama hapa nikalalamika sana, nikalia sana, kwamba hospitali yangu ile ya Wilaya ya Liwale haina wafanyakazi kwa maana ya madaktari lakini nashukuru Alhamdulillah Mheshimiwa Waziri ameisikia kilio changu amenipa madaktari wawili namshukuru sana nasema ahsante sana. (Makofi)

Pamoja na hilo bado nitaendelea kukuomba kwamba katika zahanati 31 za Wilaya ya Liwale zinaongozwa na enrolled nursing, kwa maana ya kwamba hatuna clinical officers. Wilaya mzima ile ina clinical officer wanne tu. Kwa hiyo, bado tunaendelea kulia pengine kama utapata nafasi hiyo utuongezee hao clinical officers.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile hospitali ile ya Wilaya ya Liwale ina x-ray haina mtaalamu wa hiyo x-ray.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nijielekeze kwenye taasisi moja muhumu sana ambayo ni taasisi ya Mirembe. Taasisi ya Mirembe kama ilivyo umuhimu wake, nimefanya utafiti huu kwa muda wa miezi sita, taasisi ya Mirembe inakabiliwa na matatizo lukuki. Kwanza kabisa ni Ikama ya wafanyakazi, posho ya mazingira magumu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninapoongea posho ya mazingira magumu Hospitali ya Mirembe inafahamika. Pia madai ya watumishi mbalimbali waliopandishwa madaraja pamoja likizo. Kikubwa zaidi katika taasisi ile ya hospitali ya Mirembe sasa hivi imegubikwa na tatizo kubwa la rushwa. Kwa utafiti nilioufanya, tatizo hili na matatizo mengine yote lukuki niliyoyaorodhesha hapa, tatizo kubwa liko kwenye uongozi wa Hospitali ya Mirembe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiongea na wafanyakazi wa Hospitali ya Mirembe morali ya kufanyakazi imeshuka. Hawana ushirikiano kutoka ngazi ya juu mpaka kwa mtu wa chini. Naomba Mheshimiwa Waziri ufanye utafiti, nenda Hospitali ya Mirembe, Mkurugenzi wa Hospitali Mirembe siyo rafiki kwa wafanyakazi wa Mirembe, na hii inashusha hadhi na morali ya wafanyakazi ya Hospitali ya Mirembe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna wafanyakazi ambao wameshushwa madaraja na wanashushwa na mshahara, hivi mfanyakazi aliyeshushwa daraja, mkashusha na mshahara halafu unamuacha kituo hicho hicho, huo ufanisi wa kazi atautoa wapi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nijielekeze sasa kwenye Hospitali ya Wilaya ya Liwale. Hospitali ya Wilaya ya Liwale aina hadhi ya kuitwa Hospitali ya Wilaya, kama ambavyo Katibu wa Wizara ya TAMISEMI anayeshughulikia mambo ya afya alivyosema. Halmashauri pamoja na kwamba tumeambiwa sisi wenyewe ndiyo tuanzishe vipaumbe, kweli sasa hivi tumeshatafuta kiwanja tumeshapata kiwanja, na Inshaallah bajeti inayokuja tunaweza tukaanza ujenzi. Tunaomba Mheshimiwa Waziri support yako tujengee Hospitali ya Wilaya ya Liwale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kama nilivyosema awali Wilaya ya Liwale ina zahanati 31, ina kata 20 lakini tuna kituo kimoja tu cha afya. Hapa napenda kutoa shukrani zangu za dhati kwa Naibu Waziri wa TAMISEMI ameweza kutusaidia pesa kidogo kwa ajili ya kuboresha kile kituo chetu kidogo cha afya, naye nasema Alhamdulillah Mwenyezi Mungu ampe umri mrefu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa bado naendelea kusisitiza takwimu za ...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana, ninaunga mkono hotuba ya upinzani.