Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Leonidas Tutubert Gama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na wenzangu kumpongeza sana Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri sana aliyoianza ambayo imetupa matumaini Watanzania wote ya kuona kwamba sasa tunakwenda kule tunakokuhitaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nichukue nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa maelezo yake mazuri sana. Sisi sote tuna imani mno na yeye binafsi na tuna imani sana na timu yake ya Mawaziri ambao nashukuru wote wanakwenda kwa kasi ile aliyoanza nayo Mheshimiwa Rais. Tunaomba basi Mheshimiwa Waziri Mkuu kama ulivyoanza uendelee hivyo kuhakikisha unasimamia yale yote ambayo umewasilisha katika Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa mwenyekiti, nina maeneo machache ya kushauri. Eneo la kwanza, naomba nishauri juu ya wastaafu. Kwenye Majimbo yetu tuna wastaafu wengi sana. Mimi kuanzia nilipochaguliwa kuwa Mbunge moja kati ya watu wengi sana waliokuja kwa malalamiko mbalimbali ni wale ambao wamestaafu kutoka maeneo mbalimbali kwenye taasisi za umma na binafsi. Imeonekana dhahiri kwamba wastaafu wengi wanachelewa kupata malipo yao au wengine wanalipwa malipo kwa kupunjwa au wengine hawapati kabisa malipo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali ifanye zoezi la makusudi la kuwatambua wastaafu wote na jinsi walivyoshughulikiwa na taasisi zao ili tuweze kuona namna ya kupunguza na kuiondoa kero hii na matatizo ya wastaafu. Wastaafu hawa wamefanya kazi kubwa sana ya kutumikia nchi hii, kwa hiyo, wanapoteseka maana yake hatuwatendei haki. Ni imani yangu tukifanya zoezi la kuwatambua wote na maeneo ambayo wamestaafu na kile wanachokidai itakuwa rahisi zaidi kutoa maelekezo na miongozo ili kuhakikisha wastaafu wote wanapata haki zao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama Ilani yetu ya Uchaguzi ya CCM ilivyosema, tunao wastaafu kutoka kwenye taasisi mbalimbali za umma, lakini vile vile tunao wazee ambao hawakuwa watumishi katika maeneo mbalimbali, nafikiri sasa ni muda muafaka wa Serikali kujenga utaratibu wa namna ya kuwalipa pensheni wazee wote, kwa wale ambao walikuwa watumishi wa umma na wale ambao wamezeeka wakiwa wanafanya kazi za kujenga nchi yetu hasa kwenye eneo la kilimo na mifugo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wote tunafahamu kwamba wazee hawa waliokuwa wanafanya kazi kwenye taasisi za umma na wale waliokuwa wanafanya kazi za kujenga nchi kwa kutumia sekta binafsi, wote wamesaidia sana kuichangia nchi hii kufika hapa tulipofika. Kwa hiyo, kama ilivyosema Ilani yetu ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ni vizuri ukatayarishwa utaratibu ili pensheni iwe kwa wazee wote waliostaafu kwenye mashirika ya umma na wale waliostaafu kwenye shughuli binafsi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini ukiangalia maeneo mengi ya wastaafu ni zile taasisi au Mifuko ya Jamii ndiyo wengi wanatoka huko. Ukienda kwenye historia ya Mifuko ya Jamii unakuta tuna Mifuko ya amii mingi sana kiasi kwamba hata watumishi wamekuwa wanayumba, wengine hawajui waende Mfuko gani, wengine wanakwenda kwenye Mifuko kwa sababu ya kushawishiwa bila kuijua vizuri Mifuko hiyo na kuna utitiri wa Mifuko ya Jamii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri hebu tuangalie uwezekano wa kuwa na Mifuko ya Jamii michache ambayo inaweza kuwafanya wafanyakazi na vikundi mbalimbali vikajiunga na Mifuko michache na tukaweza kuisimamia vizuri zaidi. Nashauri tuwe na Mifuko ya Jamii katika sekta kama nne hivi. Tunaweza kuwa na Mfuko wa Jamii kwa ajili kuhudumia sekta binafsi, tunaweza kuwa na Mfuko wa Jamii kuhudumia sekta ya umma, tunaweza kuwa na Mfuko wa Jamii kuhudumia sekta ya afya na tunaweza kuwa na Mfuko wa Jamii kwa ajili ya kuhudumia sekta ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali ifanye kazi ya ziada ili kutoa elimu ya kuhakikisha kwamba watu wote wanaelewa na wanajiunga na Mifuko hii ya Jamii kwa maana ya watu katika makundi yao. Kuna akinamama lishe au mama ntilie, bodaboda, wafanyabiashara ndogondogo, wakijiunga na Mifuko hii itasaidia sana kuweza kujiwekea akiba ya uhakika wa maisha yao baada ya kufikia umri wa utu uzima. Tunajua tatizo la ajira lilivyo pamoja na juhudi zinazofanywa na Serikali bado vikundi vya wajasiriamali ni sehemu moja muhimu sana ya ajira binafsi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba tuna Baraza la Taifa la Uwezeshaji, Baraza hili lingeweza kabisa kuona namna gani tunaweza kuwezesha vikundi hivi vya akinamama wajasiriamali, vijana wajasiriamali na bodaboda, tuone namna gani Mfuko huu au Baraza hili linaweza kujikita katika suala hili kuona namna gani tunawasaidia ili kuondoka kwenye umaskini. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali kuwa na maamuzi thabiti. Hivi sasa wote tunajua vijana wa bodaboda au vijana kwa ujumla. Kulikuwa na kundi kubwa sana ambalo lilikuwa halina mwelekeo. Katika Bunge hilihili kipindi kilichopita tumeruhusu kuanzisha usafiri wa bodaboda. Usafiri wa bodaboda ndiyo msaada mkubwa sana kwa shughuli mbalimbali za kimaendeleo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na watu wa bodaboda kusaidia sana kupunguza kundi kubwa la wazururaji lakini mpaka sasa haieleweki, hivi tuna tatizo la kutokuwataka bodaboda? Maana kila ukisikia habari unasikia Dar-es-Salaam wamekamatwa, pikipiki 100 zimekamatwa, Songea wamekamatwa wako Polisi, mahali fulani wamekamatwa. Kwa nini hatufiki mahali tukaweka utaratibu mzuri wa kuyashughulikia matatizo katika uendeshaji wa bodaboda badala ya kuwanyanyasa hawa vijana bila kujua sababu za msingi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nina hofu kubwa sana kwamba kama tutaendelea kuwanyanyasa hawa vijana, tunakamata pikipiki zao zinakaa Polisi, maana yake tutatengeneza kundi lingine ambalo litakuwa kundi kubwa tusiloweza kulimudu wakiingia mitaani kwa nia mbaya. Kwa hiyo, nashauri Serikali hii ijipange vizuri kuona namna gani tunashughulikia kundi hili na makundi mengine ili yaweze kujitegemea na vijana waweze kuendesha maisha yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine nataka nishauri. Tuna mahusiano mazuri sana kati ya Tanzania na nchi nyingine. Sote tunajua kwamba tuna mahusiano mazuri na jirani zetu wa Kenya, Uganda, Burundi, Rwanda, Zambia, Msumbiji, Kongo na kadhalika. Hata hivyo, naona mwelekeo wa Serikali umebana sana Kaskazini, upande wa Kusini kasi siyo nzuri sana. Sisi tutakumbuka mahusiano yetu mazuri yalivyo kati ya sisi na ndugu zetu wa Msumbiji. Tuna mahusiano mazuri sana ya kihistoria lakini tumewasahau ndugu zetu wa Msumbiji kwa maana ya kufungua mpaka kati ya Tanzania na Msumbiji kupitia Kijiji kile cha Mkenda kule Songea.
Mheshimiwa Spika, kama tutafungua mahusiano yale tutaimarisha sana mahusiano ya kibiashara kati ya Tanzania na wenzetu wa Msumbiji kwa upande wa Mkoa wa Ruvuma, lakini vilevile wananchi wetu wataweza wakafanya kazi nzuri ya biashara kati ya sisi na Msumbiji na hivyo kuinua kipato cha wananchi. Kwa hiyo, naomba Ofisi ya Waziri Mkuu ione namna gani inafanya utaratibu wa kufungua mpaka ambao upo na kuna barabara ambayo ipo lakini haishughulikiwi. Barabara ile Ikishughulikiwa inaweza kutusaidia sana katika shughuli nzima za kuongeza na kupanua uchumi wa wafanyabiashara wa eneo lile la Songea na Mkoa wa Ruvuma kwa jumla. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa na mengine lakini naona muda wangu hauniruhusu, basi nichukue nafasi hii niunge mkono hoja kwa asilimia mia moja. Niitakie Serikali yangu ya Awamu ya Tano utekelezaji mzuri wa Ilani ya CCM.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuwasilisha.