Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Hotuba ya Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018.

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya kuchangia Wizara hii muhimu. Kwanza nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye amenipa afya na nguvu na kuweza kuendelea kuwatumikia wananchi wangu wa Jimbo la Kyerwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii kipekee kumpongeza Rais wetu, kwa kazi nzuri anayoifanya, hakika imeonekana mbele ya Watanzania kuwa huyu ni Rais mtetezi wa wanyonge. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi hii pia kumpongeza Waziri wetu Mheshimiwa Ummy, Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na watendaji wote kwa kweli kazi mnayoifanya ni nzuri, Mheshimiwa Ummy na timu yako ninasema msonge mbele na Mungu atawafanikisha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kuchangia bajeti. Kwanza niipongeze Wizara ya Afya kwa kuboresha kituo chetu cha afya cha Nkwenda. Kituo hiki sasa hivi akina mama wanapata huduma nzuri, kituo hiki kimeboreshwa, Mheshimiwa Ummy nakushukuru sana umetupatia ambulance, tulikuwa na hali mbaya. Sasa hivi kile kituo kwa kweli ni cha kisasa ingawa bado wananchi wanahitaji huduma zaidi kwa sababu ukilinganisha na jiografia ya jimbo langu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee kwa upande wa dawa. Kwa kweli Serikali inajitahidi lakini bado mahitaji ni mengi na dawa bado haziwafikii wananchi wetu. Niombe Serikali iongeze nguvu na tumeona kwenye bajeti imetenga hela nyingi lakini bado. Niiombe Serikali, Mheshimiwa Waziri hizi dawa mnazopeleka hebu zisimamiwe vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna maeneo mengine mimi bado ninaamini pesa inayotengwa dawa zinanunuliwa lakini zile dawa zinachakachuliwa zinauzwa mitaani. Mimi nitoe mfano kama kule kwangu Kyerwa. Ukimuuliza DMO atakwambia dawa zipo, lakini unapooenda kwa wananchi wanakwambia kila tunapoenda kituo cha afya hatupati dawa za uhakika. Kwa hiyo, mimi niombe Mheshimiwa Waziri uweke utaratibu ambao tunaweza kufuatilia hizo dawa tukajua kwa siku ni watu wangapi, ikiwezekana hata majina yale waliotibiwa na kupewa dawa yawe yanabandikwa ili tupate uhakika hizi dawa zinaenda vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuiomba Serikali yangu, bado wananchi wanahitaji sana kwa upande wa vituo vya afya, Serikali inajitahidi kuboresha, lakini bado kuna maboma ambayo wananchi wameanzisha wao wenyewe, mengine yamekaa muda mrefu miaka mitano mpaka kumi. Niiombe sana Serikali, hawa wananchi tusije tukawakatisha tamaa, tujitahidi kumalizia haya maboma ili wananchi wetu waweze kupata huduma. Lakini kuna jambo ambalo mimi nishauri, kwenye ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi tunasema kituo cha afya kila kata na zahanati kila kijiji. Hili jambo ni zuri lakini mimi niishauri Serikali, kwa kipindi hiki ambacho bado hatujaweza kufikia hapo hebu tupeleke nguvu yetu kila kituo cha afya kila tarafa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano mimi nina tarafa nne, katika tarafa nne nilizonazo mimi nina kituo cha afya kimoja ambacho kina uhakika. Tunaposema tunapeleka kwenye kila kata nina uhakika hatutaweza kufikia hayo malengo kwa wakati tulioupanga; lakini tukipeleka kwenye kila tarafa ikapata kituo cha afya mimi ninaamini wananchi wetu tutaweza kuwasogezea huduma kwa ukaribu. Kwa hiyo, huo ni ushauri Mheshimiwa Waziri uuchukue na iwe kwa Waheshimiwa Wabunge wote kwenye majimbo yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la watumishi. Mheshimiwa Waziri bado watumishi ni wachache, wananchi wanakosa huduma kwa sababu ya watumishi. Kwa mfano mimi kwenye kituo changu pale Nkwenda tuna watumishi wachache sana. Nimuombe Mheshimiwa Waziri Ummy, mmetangaza ajira kwa ajili ya madaktari, hebu tuangalie haya majimbo ambayo yako pembezoni kama kwetu Kyerwa, kwa kweli hali ni mbaya sana. Tusiangalie maeneo ya mijini hebu tuangalie na huku pembezoni ili Watanzania wote waweze kupata huduma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie suala la bima ya afya. Suala la bima ya afya ni zuri sana, niombe sana Serikali tuendelee kuwahamasisha wananchi ili kila mwananchi aweze kupata bima ya afya. Vilevile tuangalie hawa wazee wetu ambao tumesema wapate matibabu bure, bado huduma hii ni ngumu, wazee wetu bado hawapati huduma bure. Wanapokwenda kwenye zahanati au hospitali wanahudumiwa na daktari lakini mwisho wanaambiwa waende kununua pharmacy.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawa wazee kama tumesema wapate huduma bure, Mheshimiwa Waziri hebu tuweke utaratibu ili waweze kupata huduma bure ili na wao wafurahie matunda ya taifa lao wakati wanaelekea jioni kuaga dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi michango yangu sehemu kubwa ni hiyo, lakini niombe sana Mheshimiwa Ummy, kwa kweli umekuwa ukitoa ushirikiano pale tunapokuja kwako kuleta matatizo ya wananchi wetu. Nikuombe sana Mheshimiwa Ummy na Mheshimiwa Kigwangalla moyo huo uendelee bado wananchi wetu wanayo mahitaji mengi, bado huduma za afya hazijaweza kukidhi viwango vinavyotakiwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ninaunga mkono hoja, ninaishukuru sana Serikali yetu kwa kazi zinazofanyika, ahsanteni sana.