Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana nami kupata fursa hii ya kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Kwanza, kabla ya yote naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja, maana yake nisije nikatiririka mpaka nikajisahau kama ule upande wa pili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pili, nitoe pongezi kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa hotuba yake ya bajeti ambayo inagusa, inakidhi na inajibu changamoto nyingi za Watanzania mpaka imewaogopesha upande wa pili kwa sababu watachangia nini wakati Waziri Mkuu amemaliza kila kitu na ukija kuchanganya na utendaji wa Rais Dkt. John Pombe Magufuli amewamaliza kabisa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu hawa wamekuwa kigeugeu sana. Tuwaambie kabisa CCM imejaa viongozi wa kila aina. Awamu ya Nne hawa hawa walikuwa wanalalamika Serikali haichukui maamuzi, ikichukua maamuzi inachelewa, tukawaambia sasa tunaleta Rais ambaye anachukua maamuzi haraka. Sasa wameanza kulalamika, wanalalamika nini, ni kwa sababu ameshawapiga Dokta John Pombe Magufuli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, napongeza bajeti ya Waziri Mkuu kwa hali halisi, kuna Mbunge mmoja huku huwa anasema kwamba maneno yanadanganya lakini hesabu hazidanganyi. Nataka nimpeleke huko huko kwenye hesabu, hii bajeti imemaliza kila kitu, ukurasa wa mwisho kabisa kwenye fedha pale zilizopitishwa kwa sababu Waziri Mkuu ameonesha kwamba anaenda kutokana na maneno wanayozungumza Serikali ya Awamu ya Tano na vitendo vinaelekea vitakuwa hivyo hivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, twende tu kwenye fedha alizoomba tuzipitishe ni Sh. 236,759,874,706 wakati mwaka 2015/2016 fedha zilizopitishwa zilikuwa ni shilingi milioni 391.966 kwa kukaribisha, ni punguzo zaidi la asilimia 40 maana yake ni jinsi Serikali ilivyojipanga kubana matumizi na kuleta bajeti halisi ambayo inalingana na uwezo wa nchi yetu. Pia data hizo hizo, katika OC, mwaka 2015/2016 ilikuwa shilingi bilioni 349.288 mwaka huu OC imepunguzwa mpaka imekuwa shilingi bilioni 71.564, ni punguzo la asilimia zaidi ya 79.5, kujibana kwenye matumizi ya hovyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kupunguza pesa hizo katika bajeti halisi ameenda kuziongezea kwenye masuala ya maendeleo. Suala la maendeleo mwaka 2015/2016 ilikuwa ni shilingi bilioni 42.6 lakini bajeti ya Waziri Mkuu hii aliyoileta hapa ni shilingi bilioni 165.196, ni sawa na ongezeko la asilimia 122.5. Ndiyo maana nimesema naunga mkono hoja siyo kishabiki kwa uhalisia na namba halisi alizoleta Waziri Mkuu. Inaonesha ni jinsi gani bajeti hii inavyoenda kuwakomboa Watanzania walio wengi ambao kama anavyosema Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwamba waliteseka muda mrefu sasa nao ni zamu ya kuteseka upande wa pili.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema upande wa pili unaona wanavyolalamika ni baada ya hii kasi ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ya kutumbua majipu na hasa baada ya jipu kumfikia mkwe wao. Baada ya mkwe kuwekwa ndani ndiyo hawa wapambe wanaanza kulalamika na kujihami wanaona huu moto unakuja. Niwatoe shaka tu kwamba aliyekuwa msafi ataendelea kuwa msafi, wale wachafu mkono wa sheria utaendelea kuwafikia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya facts hizo, naomba nishauri Serikali katika mambo yafuatayo:-
Kwanza suala la ajira, naiomba Serikali izingatie sana katika kuweka mipango thabiti kwa ajili ya SME kwa maana ya wafanyabiashara wadogo na wa kati na hasa ukizingatia nchi yetu watu wengi wamejiajiri kwenye kilimo na kilimo ndiyo kinatoa ajira nyingi kwa maana ya kilimo na wafanyabiashara wa kilimo na watu wa namna hiyo. Kuna mambo mengine ambayo yako kisheria kwa mfano mfumo stakabadhi ghalani upo kisheria lakini ni mfumo ambao unawatoa SME na wafanyabiashara wadogo kushiriki katika biashara ya mazao ya kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niiombe Serikali itafute namna yoyote inavyowezekana ku-accommodate kundi hili kubwa la SMEs jinsi ya kushiriki katika mfumo huo ili kuweza kukabiliana na tatizo kubwa la ajira na ukizingatia Serikalini ajira hamna hata huko sekta binafsi siyo nyingi kiasi hicho kama tunavyofikiria, nyingi tunategemea watu wajishughulishe katika ujasiriamali, mambo ya biashara na mambo mengine. Ndiyo maana Mheshimiwa Waziri Mkuu utaona hata kule anasema changamoto mojawapo ni urejeshaji wa mikopo kwa sababu vijana wanakwenda kujiajiri lakini wanakosa hizo fursa za kujiajiri kwa sababu fursa zimekuwa chache.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tukiwatengenezea vizuri namna ya kuwasaidia kwa ajili ya kushiriki katika ujasiriamali hata urejeshaji wa mikopo tutakuwa tumetatua tatizo hilo. Hata hizi fedha ambazo Serikali kwa nia nzuri inataka kuzi-allocate kwa ajili ya kukopeshana kwenye kila kijiji shilingi milioni 50, lakini lazima tuwatafutie kazi za kufanya la sivyo utawapa shilingi milioni 50 kama kazi hakuna watu watakula. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka kuishauri Serikali kwenye suala la maji hasa kwenye Bwawa la Kidunda. Bwawa la Kidunda nimeanza kulisikia hata shule sijaanza lakini mchakato wake umekuwa mrefu ukihusisha mambo ya mazingira na kadhalika. Tangu miaka 80 wazee wengine wananiambia tangu miaka ya 70 Kidunda inazungumziwa lakini sasa hivi Serikali imefika mahali pazuri naomba utekelezaji wake uende haraka sana. Kwa kumaliza utekelezaji wa mradi huu Jiji la Dar es Saalam ambalo linategemewa kiuchumi na Tanzania zaidi ya asilimia 70 utaweza kupata maji ya uhakika na viwanda vitaweza kwenda, lakini na sisi huku Morogoro tutaweza kuneemeka na fursa zinazokuja na Bwawa la Kidunda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nataka kuishauri Serikali kuhusiana na migororo ya ardhi. Serikali imekuja na mpango mzuri wa majaribio katika Wilaya za Mvomero, Ulanga na Kilombero, naipongeza sana. Naomba katika mpango huu kwa sababu sasa hivi Morogoro ndiyo tunaongoza kwa migogoro ya ardhi na sababu kubwa ni kwamba ndiyo ardhi ambayo ina rutuba lakini kuna mashamba pori mengi na pia tuko karibu na soko kubwa la nyama kwa maana ya Dar es Salaam na kwenda nje, lazima mtu apitie Morogoro kwenda ku-export.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nia nzuri ile ya majaribio kwa Wilaya tatu tu ningeomba ingefanyika kwa Mkoa mzima wa Morogoro ili kuondoa hili tatizo, ukiwabana huku wanahamia upande wa pili. Mtamaliza huku watatoka upande wa pili wataenda kule kwa sababu ilishatokea katika ile Operesheni Tokomeza walianza Kilombero wote wakaja kwetu Morogoro Vijijini, operesheni ilivyokwisha wakarudi upande ule ule. Ni vizuri jambo hili lingefanyika kwa mkoa mzima ili kuwadhibiti vizuri hasa wale wavamizi waliokuja bila utaratibu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka pia kushauri katika suala la afya. Wilaya ya Morogoro ni kongwe lakini mpaka leo haina Hospitali ya Wilaya. Wilaya hii ina Halmashauri mbili, Manispaa na Morogoro Vijijini lakini mpaka leo hii hatuna Hospitali ya Wilaya. Naomba katika mpango huu ingeingizwa pia na Hospitali ya Wilaya ili tuondoe adha ya watu wa Halmashauri hasa wa Morogoro Vijijini ambao wanatembea zaidi ya umbali wa kilometa 180 kufuata huduma hiyo katika Hospitali ya Mkoa wa Morogoro.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nataka niishauri Serikali katika suala la uhifadhi wa mazingira na utunzaji wa vyanzo vya maji. Wote tunakubaliana miongoni mwa vyanzo vya maji katika nchi yetu vipo katika milima ya Uluguru kwa maana ya kule Kinole na Tegetero mpaka Mgeta, lakini utunzaji wa vyanzo hivyo inaachiwa Halmashauri…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)