Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Hamoud Abuu Jumaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa uwezo wake mkubwa na upendo alionao juu yetu sisi sote kwa kutuwezesha kuwa mahali hapa katika kutimiza majukumu yetu ya kila siku, pia kuniwezesha nami kuchangia hotuba hii ya bajeti iliyo mbele yetu ya mwaka wa fedha 2017/2018. Vilevile nimpongeze Mheshimiwa Waziri pamoja na Wizara kwa ujumla wake kwa kuandaa bajeti nzuri yenye mlengo chanya, bajeti hii inaenda kutekeleza Ilani ya Chama cha Mapinduzi, mahsusi kuleta maendeleo kwa wananchi wake na Taifa kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilio changu cha muda mrefu ni miundombinu ya barabara na mambo mengine mengi, ila kuna hii barabara ya Makofia - Mlandizi - Mzenga, ni miaka sita (6) sasa tunazungumzia ujenzi wa barabara hii, wananchi wamekuwa wakipata shida sana katika shughuli zao za kila siku. Kutokana na hii barabara kuwa mbovu shughuli zao za kiuchumi zimekuwa zikizorota. Naiomba Serikali hii sikivu katika bajeti hii wakamilishe ujenzi wa barabara hii ili wananchi wale na wao waone faraja na kuanza kutumia barabara nzuri. Katika bajeti hii tunaomba fedha zitengwe na barabara hiyo iweze kukamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, niipongeze Serikali kwa jitihada kubwa inazoendelea kuzifanya kwa kuleta miradi mikubwa ya barabara za juu makutano ya TAZARA, daraja jipya la Selander, ujenzi wa barabara ya Dar es Salaam - Chalinze kwa kiwango cha expressway na bila kusahau ujenzi wa barabara za juu (interchange) kwenye makutano ya barabara ya Ubungo. Hizi ni hatua muhimu za kimaendeleo katika kukabiliana na changamoto ya msongamano wa magari. Vilevile Mji wa Mlandizi kutokana na kukua kwa kasi, kuna uhitaji wa makutano ya barabara ili kurahisisha watumiaji na kuufanya uwe wa kisasa zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda mrefu sasa umepita tangu kuomba kuwekewa kivuko cha kuvukia watu pamoja na vyombo vya moto, Ruvu Station, Soga, Mpiji, Kwala na Magindu. Kukosekana kwa vivuko hivyo kunapelekea wananchi kuwa katika hali ya hatari sana kwani maeneo hayo hayana alama yoyote na kuwa kikwazo kwa wananchi kufanya shughuli zao za kila siku pindi wanapotaka kuvuka ama kuvusha vitu mbalimbali. Naomba katika bajeti hii sasa tupewe kipaumbele kwa maeneo hayo kuwekewa vivuko. Vilevile kuna uhitaji mkubwa sana kwa maeneo tajwa hapo juu kuwa na vituo vya treni ili kuwarahisishia wananchi hawa, pindi kukiwa na vituo kutakuwepo na fursa mbalimbali katika maeneo hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya mawasiliano bado imekuwa kubwa hapa nchini kwetu. Jimboni kwangu Kibaha Vijijini ni wahanga wa changamoto hii kwani kuna maeneo mengi hakuna kabisa mawasiliano ya simu. Kwa kuwa hakuna hata kampuni moja ya simu inayopatikana maeneo hayo ya Dutumi, Mpelamumbi, Miyombo, Gwata na Msua. Tunaomba minara ya Tigo, Vodacom na Airtel maana hakuna mawasiliano kabisa. Hakika kwa wananchi wangu hii imekuwa ni kero ya muda mrefu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, naipongeza Serikali kwa hatua yake nzuri ya kukamilisha Kituo Kimoja cha Kuhifadhia Taarifa na Mifumo ya Serikali (Government Data Centre) na Serikali haina budi kuzihamasisha Ofisi zote za Serikali kutumia mfumo huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa sijatenda haki kama nisipoipongeza Serikali kwa hatua yake iliyoichukua siku si nyingi ya kuanza mradi mkubwa kabisa wa treni ya umeme ama treni iendayo kasi kama wengi walivyozoea. Huu ni mradi mkubwa na wa kihistoria katika nchi yetu. Mradi huu utarahisisha sana usafirishaji kwenye sekta ya reli, utapunguza muda wa kusafirisha mizigo na abiria kwani treni hii itakuwa inatumia muda mfupi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ushauri wangu na maombi kwa Wizara, naomba mradi huu usiache kuwajali vijana wetu katika kutoa ajira kwa hatua hii ya awali ya ujenzi wa reli kwa (standard gauge), kwa maeneo yote reli itakapopita basi watu wa maeneo yale wasiachwe nyuma, wachukuliwe na kupewa ajira kwa mujibu wa taratibu na sheria kama zinavyosema. Haitapendeza kuona vijana wanatoka maeneo tofauti kuja kufanya kazi katika eneo ambalo nalo lina vijana wasiokuwa na ajira. Mradi huu uwe chachu na mfano kwa miradi mingine hata na nchi jirani ziweze kuiga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bandari yetu hasa ya Dar es Salaam imekuwa lango kuu na tegemeo kwa nchi mbalimbali zilizotuzunguka. Naipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa mageuzi makubwa ya kimkakati katika kuiboresha bandari yetu hii pia na bandari nyingine zilizopo ndani ya nchi yetu. Bandari ni chanzo kizuri cha mapato kama tu kikitumiwa vizuri na kwa uadilifu mkubwa. Hivyo basi hatua hizi zilizochukuliwa ziwe endelevu ili ziendelee kuleta tija kwa Taifa letu

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto ya kuamini na kuzikubali bandari kavu ila bandari kavu kama tukizipa kipaumbele zitakuwa na msaada mkubwa sana. Hapa nazungumzia bandari kavu za pembezoni mwa miji kama Jimboni kwangu Kibaha Vijijini tumetenga maeneo maalum kwa ajili ya bandari kavu na kama mpango huu ukifanikiwa ina maana utapunguza msongamano ambao uko mjini. Mfano niliwahi kuishauri Serikali humu humu Bungeni kuhusu suala la bandari kavu iliyopo Kwala, bandari hii iwe maalum kwa kuegesha magari yote (used), kwa maana kuziondoa yard za kuuzia magari (used) ambazo zimezagaa kila kona Jijini Dar es Salaam na hivyo kuwepo sehemu maalum ya mtu akitaka magari (used) anajua wapi pa kwenda. Hili limefanyika katika nchi nyingi sana zilizoendelea kama Dubai na kadhalika huwezi kukuta kila kona ya mji kuna yard ya kuuzia magari. Hizi yard zimekuwa zikiharibu mandhari ya miji yetu na uchafuzi wa mazingira.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hilo pia la bandari kavu kuwepo na upatikanaji wa spea tofauti tofauti za magari pamoja na mashine mbalimbali. Hiyo itapelekea kuondokana na maeneo ya mijini kutapakaa hovyo maduka ya spea kama ilivyo hivi sasa katika Mtaa wa Shauri Moyo. Hatua hii ikikamilika watu watajua wakitaka magari yaliyotumika yote ama spea zote basi wanakwenda Kwala Kibaha Vijijini na kufanya manunuzi. Itasaidia kuwa na sehemu moja tu ambayo utapata hitaji lako ama gari au spea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili Serikali tayari imeshaonesha nia kwa kutenga maeneo kama ilivyo jimboni kwangu, kilichobaki ni utolewaji wa elimu na uhamasishaji kwa sekta binafsi kuziona fursa hizi na kuzifanyia kazi. Hatua hii ikishakamilika, Serikali itapata fursa ya kuanzisha njia ya treni kutoka Dar es Salaam mpaka Kibaha ili kuwarahisishia wananchi watakaokuwa wakienda katika bandari kavu hiyo na Serikali kupata fedha za uendeshaji. Vilevile Mkoa wa Pwani hivi sasa umekuwa na watu wengi sana, kupatikana kwa usafiri wa treni hiyo kutawasaidia watu wengi sana na kutatua changamoto ya usafiri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo ya teknolojia yamekuwa yakikua siku hadi siku na Taifa hatuwezi kukwepa ukuaji huo. Ndio maana takwimu za watumiaji wa mawasiliano zimezidi kukua siku hadi siku. Serikali imejaribu sana na inaendelea kujitahidi kuimarisha miundombinu yake na kuwasisitiza wadau wa mawasiliano pia kuzidi kuongeza jitihada mahsusi kwa ajili ya kuleta tija. Leo tunaona Serikali imezitaka kampuni zote za simu za mikono kutoa hisa kwa wananchi na wao kuwa ni wamojawapo wa wamiliki wa haya makampuni lakini bado kuna changamoto katika hili kwani uhamasishaji wa kununua hisa hizo umebaki kwa makampuni yenyewe na si Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali nayo kutilia mkazo juu ya kuhamasisha wananchi ili kuleta nguvu na imani kubwa kwa wananchi wetu. Vilevile naishauri Serikali kuzidi kuchukua hatua stahiki kwa wale wote wanaokiuka sheria na taratibu zilizowekwa kisheria ili kuzifanya sekta hizi kufanya kazi zake kwa kufuata taratibu, sheria na misingi iliyopo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho lakini si kwa umuhimu, naipongeza Serikali kwa juhudi ilizozifanya na inazoendelea kuzifanya kwa shirika letu la ndege. Shirika hili lina historia yake kubwa sana lakini hapa miaka ya karibuni historia hii ilitaka kufutika lakini sasa tuna ndege zetu na nyingine zimeagizwa zinakuja muda wowote. Hatua hii ni ya kujivunia sana na ya kihistoria. Ushirikiano na makubaliano waliyokubaliana kati ya nchi mbili za Ethiopia na Tanzania katika nyaja mbalimbali hususani ya ushirikiano wa mashirika yetu haya ya ndege ni hatua nzuri ukizingatia wenzetu shirika lao ni kubwa na lina historia ndefu. Hatua hizi zote si za kubezwa kwani zitasaidia kuliimarisha shirika letu la ndege.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.