Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Waziri Mkuu kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017

MHE. SHABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nipende kumshukuru Mwenyezi Mungu ambaye ameniwezesha afya na nguvu kuweza kusimama mbele ya Bunge hili Tukufu. Kwa kuwa ni mara yangu ya kwanza basi niwashukuru wapigakura wangu wa Jimbo la Lushoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kushukuru hotuba hii ambayo imejaa maudhui mema, niendelee kumshukuru Waziri Mkuu kwa hotuba yake nzuri. Andiko linasema nimrudishie nini Bwana kwa wema wake alionitendea, kwani hotuba ya Waziri Mkuu imekuna wengi na inastahili kupongezwa hata Mwenyezi Mungu naamini ameibariki. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, waislamu tunasema; maa yashkuru-nnasa laa yashkuru-llah (usiposhukuru watu basi hata Mwenyezi Mungu hutamshukuru). Basi nishukuru hotuba hii na pia niwashukuru Watanzania wote kwa kumchagua Rais wetu John Pombe Magufuli Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja nijikite katika kuchangia hotuba ya Waziri Mkuu. Hakuna asiyefahamu kwamba Wilaya ya Lushoto ni Wilaya ya kilimo cha matunda na mboga mboga. Wilaya ile na wakulima wanalima kwa zana ambazo ni dhaifu mno, wanalima kwa mbolea ya samadi yaani kinyesi ng’ombe. Wakulima wanapovuna mazao yao huwa wanapata taabu sana, wanunuzi wakati wa mvua barabara hazipitiki na inapelekea mazao yale yanauzwa bei rahisi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika suala zima la ukusanyaji wa mazao wananchi wa Lushoto wanapata taabu sana. Mimi kama Mbunge wao ambaye wamenituma niwawakilishe kwao, kwani wakati wa kura za maoni walisema tunakutuma wewe mnyonge mwenzetu, mkulima mwenzetu ukatuwakilishe, basi na mimi ninawaahidi kutowaangusha na ndiyo maana mkulima mimi, mnyonge mimi nimesamama mbele ya Bunge hili Tukufu kwa ajili ya wananchi wa Lushoto hususani wakulima. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba hotuba ya Waziri Mkuu iangalie wakulima wangu wa Lushoto hususan katika suala zima la pembejeo, suala zima la masoko, suala zima la kujenga maghala na kujenga mabwawa kwa ajili ya kilimo cha kisasa cha umwagiliaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la maji. Lushoto imezungukwa na vyanzo vingi vya maji, lakini miundombinu ya maji hakuna katika Jimbo zima la Lushoto. Ukianzia Kata ya Ngwelo, Gare, Mlola, Ubili, Makanya, Kwemashai, Mbwei, Ngulwi, Malibwi, Kilole, Kwekanga na Lushoto Mjini. Nakuomba katika bajeti hii basi uwafikirie watu wa Lushoto hususan katika suala zima la maji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la afya, tunashukuru tuna Hospitali ya Wilaya ya Lushoto, lakini hospitali ile ina changamoto. Hospitali ya Lushoto hususani wodi ya akina mama wajawazito, ile wodi ni ndogo inastahili kuongezwa. Sambamba na hilo katika Kata za Ngwero, Gare, Magamba, Ubili, Kilole na Kwemashai tunahitaji kujengewa vituo vya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala zima la miundombinu, Lushoto wenyewe tunaita Lushoto ya wazungu, kwani Wazungu Wajerumani walikuwa wanaishi maeneo yale, miundombinu ya barabara imejengwa tangu kipindi cha mkoloni. Kwa hiyo, niiombe Serikali ituangali katika vipaumbele vya barabara, hususan barabara ya kutoka Lushoto kupitia Soni hadi Mombo. Barabara hii ni nyembamba na mvua zikinyesha huwa kuna mawe yanaporomoka yanazuia barabara. Hata juzi kati tarehe 17 zaidi ya siku tatu magari yalilala pale mpaka hata maiti zinatoka Dar es Salaam, Tanga na sehemu zingine basi zilishindwa kupita pale kwa sababu ya mawe yaliyoshuka pale na makalvati kuziba, maji yanatiririka katikati ya barabara ilichukua takribani ya siku tatu, naomba katika bajeti yako hii basi waifikirie barabara ya Lushoto.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo kuna barabara ya kutoka Mlalo kupitia Ngwelo, Mlola hadi Makanya kwenda kwa Mheshimiwa January, Mlingano kwa Mheshimiwa Majimarefu, Mashewa, barabara hii tunaomba sasa ipandishwe hadhi iwe ya Wakala wa Barabara TANROAD. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya kutoka Dochi kupitia Ngulwi hadi Mombo, kwa kuwa barabara hii ya Lushoto - Soni - Mombo, mara nyingi mvua zinaponyesha barabara ile mawe yanashuka yanaziba barabara ningeishauri Serikali iwe na barabara mbadala ya kutoka Dochi - Ngulwi hadi Mombo ijengwe kwa kiwango cha lami na iweze kupandishwa daraja ili iweze kuwa barabara mbadala kwa ajili ya matatizo yanapotokea na breakdown zinapotokea katika barabara ya Soni - Mombo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna hawa ndugu zangu, vijana wenzangu siyo vijana wa Lushoto tu ni Tanzania nzima, vijana wanaojihusisha na bodaboda. Vijana hawa inapaswa walindwe maana bodaboda ni ajira kama ajira nyingine. Bodaboda hawa naomba kama kuna uwezekano watengewe fungu katika bajeti hii kwa ajili ya kukidhi mahitaji yao kwani katika vipaumbele vinavyotoa ajira ni watu wa bodaboda. Wamepata ajira kwa kuwa watu hawa wana watoto, wanao wake zao na wanawasomesha watoto na bodaboda ndiyo kipato chao, ndiyo ajira yao, ninaomba askari wasiwanyanyase vijana wanaojishughulisha na bodaboda, siyo kwa Lushoto tu ni Tanzania tuwalinde vijana wetu wa bodaboda. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima la umeme. Nimshukuru Waziri Muhongo, alituma timu yake wakazunguka katika Wilaya nzima ya Lushoto siyo Jimbo la Lushoto tu, Wilaya nzima ya Lushoto alituma timu yake ikazunguka na kubaini maeneo ambayo hayana umeme na kuyaandika, kuyahakikisha kwamba ameyachukua then atayafanyia kazi. Kwa hiyo nampongeza sana Profesa Muhongo, Mungu akulinde na akuzidishie umri! (Makofi)
Kuna suala zima la michezo. Lushoto kuna vipaji vingi sana, kuna vijana wengi sana ni wanamichezo wazuri na hata timu za Simba na Yanga zinakuja Lushoto kwa ajili ya kufanya mazoezi. Kwa hiyo, niombe sasa, nimuombe Waziri wangu, mpendwa wangu Mheshimiwa Nape Nnauye katika bajeti hii aifikirie Lushoto kimichezo sasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga hoja asilimia mia moja.