Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa afya njema na pia nitoe shukrani zangu za dhati kwa Rais, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kusaini ujenzi wa gati moja la Bandari ya Mtwara ambayo ndiyo chachu ya uchumi Kanda yote ya Kusini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, Mtwara Corridor inategemea kwa kiasi kikubwa ujenzi huu wa bandari ulioanza kwa kusafisha maeneo ya ujenzi huo. Ombi langu kwa Mheshimiwa Waziri ni kwamba, ahakikishe mara tu baada ya kumalizika ujenzi huo, basi magati mengine yawekwe kwenye orodha ya kujengwa ambayo ni matatu. Gati moja halitoshi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba utanuzi wa bandari uendane na ujenzi wa reli ya Kusini ambayo itaanzia Mtwara – Liganga – Mchuchuma – Mbamba Bay na nchi nyingine za Kusini mwa Afrika. Ujenzi wa reli hii utasaidia sana kufungua uchumi na Bandari yetu ya Mtwara itapata mizigo ya kutosha, hivyo kuliingizia Taifa pato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mitandao ya simu kwa baadhi ya maeneo ya Mtwara Mjini haipo. Mfano, Mbawala Chini, Mkangala, Naulongo, Namayanga, Dimbuzi; maeneo haya network hakuna kabisa na yapo Mtwara Mjini. Sambamba na hilo, Mtwara Mjini hakuna network ya TBC kabisa. Hii inafanya Wanamtwara wakose huduma ya taarifa mbalimbali hivyo kuwa nyuma ya wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Ulinzi; mwaka 2016 tuliongea sana juu ya umuhimu wa barabara hii ambayo inaanzia Mtwara Mjini mpaka Ruvuma. Tunaomba iwekwe kwenye bajeti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna Viwanja vya Ndege ambavyo havimilikiwi na Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Tanzania, naomba kujua, kwa nini Serikali imeruhusu hili? Haioni kama ni hatari kwa Taifa letu na uchumi? Naomba Wizara itoe tamko juu ya hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hakuna eneo ambalo hivi sasa Jijini Dar es Salaam ambalo lina msongamano mkubwa kama Mbagala hasa njia panda ya Charambe. Hapa kuna ulazima wa kujenga flyover haraka sana. Naomba bajeti ieleze, ujenzi wake utaanza lini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya Kilwa Road hasa eneo la Somanga - Nangurukuru imeharibika sana na ina mashimo na mabonde makubwa na sioni ujenzi au ukarabati kabambe unafanyika hasa eneo hili. Tunaomba majibu ya Waziri ili nayo ianze kujengwa kwa kiwango cha lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, barabara ya uchumi imesainiwa kwa kilomita 50. Tunaomba Mkandarasi asimamiwe kama alivyosema Mheshimiwa Rais alipokuja Mtwara Machi, 2017 na kusema kuwa Mkandarasi hayuko sharp, tunaomba asimamiwe barabara hii ijengwe haraka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa sasa kuna utanuzi wa bandari unaanza, tunaomba Wanamtwara Kusini tupatiwe usafiri wa meli hasa kwa ajili ya mizigo, kwa kuwa barabara inaharibika kwa cement kupitia barabara ya lami.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Uwanja wa Ndege wa Mtwara ni mbovu, hauna taa za kuongozea ndege; ndege hazitui usiku na inaleta usumbufu sana sambamba na kudumaza uchumi. Naomba bajeti hii ianze kukarabati na kuweka taa katika bajeti hii.