Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa, nampongeza Mheshimiwa Waziri pamoja na team yake yote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni muda mrefu sana naomba kupandishwa hadhi kwa barabara inayoanzia Mlalo - Ngwelo – Mlole – Makanya – Milingano hadi Mashewa. Kilio changu hiki mpaka sasa hakijapata ufumbuzi; na barabara hii ni barabara ya uchumi ambayo ikifunguka itakuwa inachangia pato kubwa katika Serikali pamoja na Halmashauri yangu. Pia kutoa ajira kwa vijana, maana vijana wangu wamejiajiri katika suala zima la kilimo. Mazao yao yanaharibikia mashambani kwa sababu ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mtaji huu, vijana wengi wanakata tamaa ya kulima na kukimbilia mjini. Barabara hii ina kilometa 58 tu ambayo inaunganisha Majimbo matano, yaani Jimbo la Mlalo, Lushoto, Bumbuli, Korogwe Vijijini mpaka Mkinga. Naiomba Serikali yangu sikivu itoshe sasa, naomba barabara hii ipandishwe hadhi. Pia siyo vizuri Mbunge kuwaahidi wananchi wake kuwa barabara hii itapandishwa hadhi, lakini mpaka sasa hakuna hata dalili. Kwa hiyo, naomba Serikali itoe majibu leo baada ya kuhitimisha taarifa hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna barabara ya kilometa 16 inayoanzia Dochi hadi Ngulwi mpaka Mombo. Nayo hii ni kilio cha muda mrefu sana na barabara hii ni muhimu sana. Kama unavyojua, Lushoto ina barabara moja tu ya kuingia Lushoto Mjini. Kwa hiyo, barabara hii ikipandishwa hadhi itasaidia sana Mji waLushoto, utakuwa unafikika kwa wakati wote. Kwa hiyo, naiomba Serikali yangu Tukufu ipandishe hadhi barabara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo, barabara inayoanzia Mombo, Soni hadi Lushoto. Alitokea kiongozi mmoja na kutoa tamko kuwa barabara hiyo ipite magari ya uzito wa tani 10 tu. Kauli hii imesababisha ugumu wa maisha kwa wananchi wa Wilaya ya Lushoto. Kwani biashara zilizo nyingi zinauza bidhaa kwa bei ya juu na wananchi wa Lushoto kununua bidhaa hizo kwa bei ya juu kutokana na kuingizwa kwa bidhaa hizo kwa bei ghali. Wakati huo huo magari yenye uzito wa tani 40 yanapita, bila kuathiri au kuharibu barabara hiyo. Kwa mfano, magreda, magari yanayobeba materials yanayoenda Mtwara kwenye kiwanda cha Sementi cha Dangote. Pamoja na hayo nilimuuliza Meneja wa TANROADs Mkoa wa Tanga na akaniambia barabara hiyo inaweza kubeba gari lenye uwezo wa tani 50.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Waziri atoe tamko la kuruhusu kupita magari yenye uzito usiozidi tani 40 kwani suala hili limesababisha uchumi wa Lushoto kushuka na kunilalamikia mimi Mbunge wao kila siku. Naomba Waziri atoe tamko leo hii zaidi ya hapo nitashika shilingi ya mshahara wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hotuba ya Mheshimiwa Waziri sijaona bajeti ya daraja la Mshizii pamoja na bajeti ya barabara yake ya kutoka Nyasa kupitia Gare hadi Magamba. Kwani barabara hii ni mbadala, kukitokea breakdown ya Magamba Lushoto, magari yanatoa huduma kupitia njia hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, maeneo mengi ya Wilaya ya Lushoto ni ya milima na mabonde, kwa hiyo, minara ya simu baadhi ya maeneo hakuna. Kwa hiyo, naiomba Serikali itujengee minara hasa katika Kata ya Makanya, Malibwi, Ubiri, Ngwelo, Kwekanga na Kilole.

Mheshimiwa Spika, kuhusu suala la upimaji wa barabara, yaani kutoa kilometa 30 kila upande, yaani jumla mita 60. Hili naomba niishauri Serikali yangu Tukufu kwamba iangalie maeneo mfano, maeneo ya Lushoto, Serikali ikisema itoe mita 60 itapata hasara kubwa. Ushauri wangu ni kwamba kuna baadhi ya maeneo kama Lushoto yajengewe kulingana na yalivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna ahadi ya Rais wa Awamu ya Nne ya kilometa nne za lami. Mpaka sasa hivi bado ahadi hiyo haijatekelezeka na ni takriban miaka minne sasa imepita. Naomba Serikali yangu itupatie ahadi hiyo ya Rais ili Mji wetu wa Lushoto angalau nao upendeze na tuwe tunajivunia na kumkumbuka Mstaafu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Naomba pia nipatiwe majibu haraka iwezekanavyo, maana wananchi mpaka sasa wanakosa uvumilivu kwangu, kwani wanadai nimewadanganya kwa muda mrefu sana.