Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza namshukuru sana Mungu ambaye amenipa nafasi hii kuchangia bajeti hii ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ambayo ni muhimu kwa Taifa letu. Pia naipongeza Serikali yangu kwa kazi nzuri zinazofanyika. Nampongeza kipekee Rais wangu na timu yake kwa muda mfupi, wameonesha uwezo mkubwa kuwatumikia Watanzania hasa hasa wanyonge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile nampongeza Mheshimiwa Waziri wa Wizara hii, Naibu Waziri, Katibu Mkuu, Naibu Katibu Mkuu na Watendaji wote kwa kazi nzuri wanazozifanya. Kweli naiona Tanzania mpya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza kwa sababu sisi ni mashahidi, muda mfupi tumeona hostel za Chuo Kikuu Dar es Salaam zimekamilika, usafiri wa mwendo kasi, barabara za juu Dar es Salaam, tumeshuhudia reli ya standard gauge, zinaanza kujengwa na mengine mengi. Hakika hapa kazi tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Jimbo la Kyerwa, naongelea suala la mawasiliano siyo mazuri. Upande wa mawasiliano ya simu, maeneo mengine hakuna mtandao wa simu, mawasiliano yote yanaenda au yanaingiliwa na mitandao ya nchi jirani, yaani nchi ya Uganda na Rwanda. Naomba sana Wizara ishughulikie tatizo hili ili tupate mawasiliano ya uhakika ukilinganisha na umuhimu wa mawasiliano na ya kuwa tunapakana na nchi jirani jambo ambalo kiusalama siyo nzuri kabisa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee suala la barabara zangu za Wilaya ya Kyerwa. Nikumbushe ahadi ya ujenzi wa barabara ya Mgakorongo - Kigarama mpaka Murongo wa kiwango cha lami, ambapo Mheshimiwa Waziri akijibu swali nililouliza; ni lini ujenzi utaanza na ahadi ya Mheshimiwa Waziri alisema before June, 2017 ujenzi utakuwa umeanza. Namwomba Mheshimiwa Waziri ahadi hiyo itimizwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara iangalie kwa makini matengenezo ya barabara ya Murushaka mpaka Murongo ambapo barabara hii imekuwa ikisahaulika sana kufanyiwa matengenezo. Kwa sababu barabara ya Murushaka mpaka Murongo ni ya kiuchumi zaidi ya asilimia 75 ya magari yanayotumia barabara hiyo, ingawa imepewa kipaumbele cha pili kujengwa kwa kiwango cha lami. Naiomba Wizara barabara hii kwa sababu ya umuhimu wake katika kipindi hiki ambacho haijafikiwa kujengwa kiwango cha lami, Serikali iweke changarawe kuepusha usumbufu tunaoupata katika kipindi cha mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais alipokuja Kyerwa aliwaahidi Wanakyerwa kilometa tano zijengwe Kata ya Nkwenda; nimejaribu kufuatilia lakini mpaka sasa hakuna mwenye jibu kamili. Naomba sana Mheshimiwa Waziri atupatie lami, hizi kilometa tano zijengwe ili kutimiza ahadi ya Mheshimiwa Rais na lami hii ni muhimu kisiasa. Pia namwomba sana Mheshimiwa Waziri atukamilishie kuweka lami kwenye mlima Rubunuka pande zote kuondoa usumbufu wa magari kukwama kipindi cha Mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kuipunguzia mzigo Halmashauri, tunayo barabara ya Nkwenda mpaka Mabila ambayo imejengwa kwa kiwango cha changarawe. Tunaomba ipelekwe TANROADs kwa sababu ya umuhimu wake kwa Wanakyerwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuandika hayo, narudia kuipongeza Wizara kwa kazi nzuri inazofanya. Tunawaombea sana Mungu awafanikishe katika yote mpate fedha ili na sisi Kyerwa tuone lami halisi katika barabara ya Mugakorongo – Murongo - Murushaka na Murongo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.