Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, awali nampongeza Waziri kwa hotuba nzuri ya Bajeti yenye mwelekeo wa kuipeleka nchi yetu katika ngazi nyingine. Nawapongeza pia Naibu Waziri, Makatibu Wakuu na Watumishi wote wa Wizara kwa kujituma, hali inayopelekea utekelezaji mzuri wa Ilani ya Chama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa kuendelea na mkakati wa ujenzi wa Bandari ya Mbegani Bagamoyo kama inavyooneshwa katika hotuba ya Waziri ukurasa 90. Jambo ambalo naliomba kwa niaba ya wananchi wa Bagamoyo ni kuwa, Serikali ijitahidi kumaliza malipo ya fidia kwa wanaopisha Mradi wa Bandari, pia kuwalipa fidia sahihi wale ambao wamegundulika kupunjwa fidia zao. Hiki ni kilio kikubwa kwa wananchi wanaopisha ujenzi wa mradi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kaya zipatazo 2,000 katika Kijiji cha Pande na Mlingotini zitahamishwa kupisha mradi wa Bandari. Kijiji chote cha Pande katika Kata ya Zinga kinafutwa kwenye ramani ya nchi pamoja na sehemu ya Kijiji cha Mlingotini. Kaya hizi kupitia wafidiwa waliahidiwa eneo la kuhamia katika shamba la Kidogoni Bagamoyo ambalo lilitengwa na Mamlaka ya EPZA tangu 2008.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika makao hayo mapya ndiko kungehamishiwa miundombinu yao ya jamii ikiwemo Shule ya Msingi Pande, Zahanati ya Pande, Ofisi ya Kijiji Pande, Misikiti na Kanisa. Naomba Waziri aharakishe upatikanaji wa eneo la makazi mapya ya wananchi hawa wanaopisha mradi na pia Serikali iwajengee katika makazi mapya miundombinu yao ya huduma za jamii zikiwemo shule, zahanati na kadhalika ambavyo vitavunjwa kupisha mradi. Ni zoezi gumu kaya 2,000 kujitafutia zenyewe mahali pa kuishi. Kwa vile ilikuwa ni ahadi ya Serikali, naomba Mheshimiwa Waziri alisimamie jambo hili muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaofidiwa kwa ajili ya bandari jumla yao ni 2,211. Ukitoa taasisi na wananchi wasioishi Kijiji cha Pande na Mlingotini, kaya zinazohamishwa ni karibu 2,000. Kijiji kizima cha pande kinavunjwa na sehemu ya kijiji cha Mlingotini. Hizi ni kaya nyingi. Mwaka 2013 wananchi hawa waliahidiwa eneo la makazi mpya lililotengwa na EPZA, shamba la Kidagoni. Ila kwa sasa hakuna dalili ya utekelezaji wa ahadi hii na wananchi wamepatwa na wasiwasi mkubwa! Naomba Mheshimiwa Waziri atuambie: Je, kaya hizi 2,000 zinazopisha mradi, zitapatiwa eneo la makazi mapya? Lini? Kwa Bajeti ipi? Naomba Mheshimiwa Waziri atupe jibu lenye matumaini ili kaya hizi zisije kuishi kuwa ombaomba mitaani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kati ya fidia ya shilingi bilioni 57,670/= imelipwa shilingi bilioni 45. Balance ya fidia ya wanaopisha bandari haionekani katika vitabu vya bajeti. Je, fidia hii italipwa? Pia kuna wananchi 687 waliothibitika kupunjwa fidia zao na uhakiki umefanywa na Mthamini Mkuu. Wananchi hao wanategemea malipo halali ya fidia zao, lakini fedha hizo sizioni. Mheshimiwa Waziri atueleze kama wananchi hao watalipwa mapunjo yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mradi wa Bandari Bagamoyo ni mradi mkubwa na wenye manufaa makubwa kwa nchi yetu. Bandari hii ndiyo itakayoipa maana reli ya standard gauge inayojengwa. Hesabu za kiuchumi za reli mpya zitakuwa tofauti sana, reli hiyo ikiunganishwa na Bandari ya Bagamoyo. Naiomba Serikali yangu itenge fedha kwa ajili ya ujenzi wa bandari ya Bagamoyo badala ya kuwaachia wawekezaji peke yao. Katika mradi mkubwa kama huu, Serikali iwekeze fedha zake ili iweze kuwa mshiriki kikamilifu katika mradi huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba nzuri na kazi nzuri ya ujenzi wa miundombinu ya maendeleo ya nchi yetu. Katika ukurasa wa 90 wa hotuba ya Waziri ametaja maandalizi ya ujenzi wa Bandari ya Bagamoyo. Hili ni jambo zuri sana, bandari kubwa yenye uwezo wa kuhudumia shehena nyingi kwa nchi yetu na nchi jirani, ni nyenzo kubwa ya maendeleo ya uchumi wa nchi ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wasiwasi wangu, kauli hii ya ujenzi wa bandari haina bajeti. Maandalizi haya ya ujenzi wa bandari yatafanywa vipi? Waziri atueleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.