Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nami nianze kwa kumpongeza sana Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri pamoja na timu yake yote kwa kazi nzuri ambayo wanaifanya katika Wizara hii, pamoja na ukubwa na majukumu mengi lakini wanaonekana kuweza kuyamudu na kuimudu Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza napenda nipongeze kazi ya upanuzi wa Bandari ya Mtwara ambao tayari umekwishaanza. Ni imani yangu kwamba upanuzi ule wa bandari utasaidia sana katika kuharakisha maendeleo ya Mkoa wa Mtwara, Lindi na Ruvuma hasa ukizingatia kwamba sisi ni wakulima wakubwa wa korosho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kupanua bandari ile sasa hivi hakutakuwa na sababu hata kilo moja kusafirishiwa mizigo katika Bandari ya Dar es Salaam hasa inayozalishwa katika Mikoa ile. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia suala la Liganga na Mchuchuma kwamba kule kuna uzalishaji wa makaa ya mawe, kuna chuma, tuna kiwanda kikubwa sana cha Dangote ambacho kinategemea hiyo bandari pia tunategemea chuma itakayozalishwa kule, makaa ya mawe na yenyewe pia yasafirishwe kupitia Bandari ya Mtwara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namwomba Mheshimiwa Waziri suala la upanuzi wa Bandari ya Mtwara basi liende sambamba na ujenzi wa reli kutoka Mtwara hadi Mbamba Bay na Liganga na Mchuchuma. Suala la upembuzi yakinifu limekamilika, tathmini ya mimea pamoja na nyumba maeneo ambapo reli itapita imeshakamilika. Kwa hiyo, namwomba sana suala hilo nalo liende pamoja ili ile bandari isije ikaleta mzigo mkubwa ukalazimika tena kusafiri kwa magari ambao utaharibu barabara ambayo kwa kweli tumekaa muda mrefu sana baina ya Mtwara na Ruvuma hatujawa na barabara ya kueleweka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine napenda kumpongeza sana Waziri na Serikali pamoja na Mheshimiwa Rais kwa kuanza kujenga reli ya kati. Reli ya kati ni sawa na mifumo ya damu au mifumo ya fahamu ndani ya mwili wa binadamu, reli hiyo ndiyo itakayoifanya bandari ya Dar es Salaam iweze kufanya kazi yake vizuri. Kwa hiyo, namwomba tu waharakishe hicho kipande cha kutoka Dar es Salaam kwenda Morogoro ambayo ni reli ya kisasa sana. Vipande vinavyobaki basi watangaze kwa haraka ili ujenzi huo ikiwezekana uweze kukamilika kwa muda mfupi sana, kwa sababu huo ndiyo ukombozi wa nchi yetu na maendeleo yetu kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine napongeza pia ndege ya Bombardier kuanza kutua Mtwara na Songea. Tarehe 30 imeenda kwa mara ya kwanza, nimeambiwa kwamba kutakuwa na ratiba nzuri tu zinazoeleweka. Ushauri wangu naomba ile ndege ya kwenda Mtwara inaunganisha pamoja na Ruvuma, unatoka Mtwara unaenda Ruvuma saa nzima, unatoka Ruvuma kwenda Mtwara dakika hamsini karibu na tano, halafu ndiyo utoke pale kwenda Dar es Salaam karibu tena dakika 50. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba route ya Ruvuma ikiwezekana iwe ni ya Ruvuma peke yake ili mtu akitoka Dar es Salaam anafika Ruvuma na akitoka Ruvuma anafika Dar es Salaam. Kutoka Mtwara mpaka ufike Ruvuma upite tena Mtwara kwa kweli inachukua muda mrefu sana na kama shirika kweli linataka kushindana na mashirika mengine ambayo yanaenda Mtwara hapo hamtaweza kushindana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu ni kwamba route ya Mtwara iunganishwe na ya Comoro kwa sababu kutoka Mtwara kwenda Comoro ni saa moja na kutoka Comoro kwenda Mtwara ni dakika kama 25 au nusu saa. Kwa hiyo, hapo utaweza ushindani. Huo ndiyo ushauri wangu kwamba hiyo route ya Dar es Salaam – Ruvuma – Mtwara waiangalie tena ikiwezekana Mtwara iambatanishwe na ya Comoro. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo nataka nilichangie ni suala la barabara ya kutoka Mtwara – Newala kwenda Masasi. Niishukuru Serikali kazi inaonekana kwamba inakaribia kuanza, Mkandarasi amepatikana na ameshaanza kukusanya vifaa tuna imani muda wowote ataanza ujenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika bajeti iliyotengwa mwaka huu ambao tunaenda nayo ni bilioni 21 na bajeti ambayo ipo sasa hivi ni bilioni saba. Kwa mujibu wa mkataba ule ni zaidi ya bilioni 90 na mkataba ni wa miaka miwili, sasa kwa pamoja tumetenga kwa miaka miwili bilioni 29, mkataba unataka bilioni karibu 90 na kitu. Sasa huyo Mkandarasi atajenga kwa fedha zipi? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naiomba Serikali iangalie hilo, vinginevyo tutakuwa tunamfanya Mkandarasi anakuwa site anaondoka. Mheshimiwa Waziri tunashukuru kwa sababu lazima ushukuru kidogo ulichokipata, tunashukuru kwamba sasa hivi ile ndoto imeanza kutimia, lakini pia iangaliwe bajeti ili barabara ijengwe kwa ubora unaokusudiwa, kwa sababu kama pesa zitakuwepo mkandarasi hana kazi ya kuondoka site na kwenda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho ni suala la Uwanja wa Ndege wa Mtwara. Uwanja ule umejengwa kabla sijaanza hata darasa la kwanza na hata sijui umejengwa lini kwa sababu nimepata akili nimeukuta ule uwanja upo tayari. Tangu kipindi hicho sidhani kama kuna ukarabati wowote
wa uhakika uliofanywa na sasa hivi ndege zikitua pamoja na kwamba ni uwanja wa lami lakini utafikiri umetua kwenye matuta. Kwa hiyo, nawaomba Wizara wauangalie uwanja ule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tuna masuala ya utafiti wa gesi yanakuwa yakifanyika pamoja na kwamba sasa hivi yamesimama. Kule kazi zinafanyika usiku baharini, uwanja hauna taa na kama mnavyofahamu Mtwara jua linaanza kutoka na linawahi kuchwa. Sasa siku nyingine mnaondoka abiria mnakaribia uwanja mnaambiwa uwanja umeshaingia giza mnarudi tena Dar es Salaam. Nawaomba waukarabati uwanja ule pia wauweke taa. Taa zinazotumika pale ni za wachimbaji wa gesi na hawaruhusu taa zao kwa sababu ni mobile wanaziweka pale tu panapokuwa na dharura na kwa maombi maalum. Kwa hali, ambayo tumefikia sasa hivi Mtwara kwa kweli tunaomba uwanja ule ukarabatiwe na uwekwe taa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine kwa wale ambao wameenda Mtwara, lile jengo la abiria lipo ndani ya uwanja, nalo waliangalie waone uwezekano wa lile jengo kuliweka kama majengo mengine yalivyoojengwa. Haiwezekani jengo yaani unashuka kwenye ndege unaingia moja kwa moja kwenye jengo la abiria kwa sababu kwanza ni hatari kwa abiria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudie tena kumpongeza Waziri pamoja na timu yake, niombe tu yale ambayo nimeuombea Mkoa wangu na kuiombea nchi yangu basi yafanyiwe kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.