Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Martin Alexander Mtonda Msuha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kupatiwa nafasi ya kuweza kuchangia hoja iliyopo mezani ya Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.

Nichukue fursa hii kuungana na Waheshimiwa wenzangu wote waliotangulia kwa kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi kubwa wanayoifanya, ni kazi ambazo zinaonekana, sitahitaji kurudia. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia niipongeze Serikali kwa kutupatia mradi wa barabara ya kutoka Longa hadi Kipololo, pia awamu nyingine Kipololo hadi Litowo kwa kiwango cha lami kupitia ufadhili wa Umoja wa Ulaya (European Union).

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii inazo changamoto nyingi sana, barabara hii haiendi kwa speed ambazo zilioneshwa kwenye mikataba na makubaliano. Kipande cha kwanza cha kutoka Longa hadi Bagamoyo, ambayo iko kata ya Kipololo mkataba wake ulitakiwa ukamilike tarehe 30 Septemba, 2016 bahati mbaya hadi ninavyosema hakuna hata futi moja iliyoweza kutiwa lami mpaka sasa hivi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kipande cha pili cha kutoka hapo kijiji cha Bagamoyo kwenda Litowo baada ya kufanya mabadiliko ya mkataba walitakiwa Wakandarasi wamalize kazi ile tarehe 31 Januari, 2017, bahati mbaya hadi nasimama hapa leo hii, barabara hii katika vipande vyote viliwili haijaweza kuwekewa hata nukta moja ya lami.

Mheshimiwa Naibu Spika, kikubwa barabara hii sijaiona kwenye kitabu cha mawasilisho ya Mheshimiwa Waziri, sasa sijajua iko mpango wa nje ya hii programu iliyoletwa ya 2017/2018 kwa mwendelezo au vinginevyo nitaomba tupate ufafanuzi baadaye ili iturahisishe pia ufuatiliaji wa ujenzi wa barabara hii.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wenzangu walitangulia pia kuchangia asubuhi Mheshimiwa Jacqueline Ngonyani Msongozi lakini pia kupitia swali la nyongeza Mheshimiwa Mpakate juu ya barabara inayotoka Kitahi kwenda Lituhi kupitia kwenye Mgodi wa Makaa Ngaka.

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara hii ni muhimu sana kwa uchumi si tu wa Mbinga lakini pia uchumi wa Taifa letu kwa ujumla. Barabara hii ya Kitahi - Lituhi ni barabara kubwa sana ikizingatia na upanuzi unaoendelea kufanyika kule kwenye makaa ya mawe Ngaka. Jambo linalofanyika sasa hivi kwa sababu madaraja ya ile barabara kutoka Kitahi kwenda Ngaka, kata ya Ruanda ni membamba wametengeneza bandari kavu karibu na Kitahi. Kwa hiyo, utakuta pana msururu mkubwa sana wa malori yanayotakiwa sasa kwenda kuchukua mzigo unaotoka machimboni na kuletwa kwenye bandari kavu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tuiombe Serikali iangalie, mwaka jana nilikuwa na swali juu ya barabara hii, niliambiwa kuwa upembuzi yakinifu ulikwisha fanyika. Bado kwenye kitabu cha mawasilisho ya Mheshimiwa Waziri barabara hii sioni kama inapewa kipaumbele cha kujengwa kwa lami. Kwa hiyo, ombi langu ni kwamba barabara hii ni ya kitega uchumi na bahati nzuri lazima niwe muwazi kwamba Mkuu wa Mkoa jana alinipigia simu baada ya kupata taarifa kwamba barabara hii haijatengewa fedha kuweza kujengwa kwa kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati Mheshimiwa Waziri Mkuu akiwa ziarani Mkoani Ruvuma, mwezi Januari 2017; tukiwa kwenye makaa ya mawe ilionekana kwamba katika mkataba wa mwekezaji TANCOAL component mojawapo ya mkataba wake ni kujenga barabara hii kwa kipande cha kutoka Kitahi mpaka pale machimboni Ngaka. Kwa hiyo, ninaiomba Serikali ifanye mapitio ya mkataba huu kama ilikuwa ni makubaliano ya yule mwekezaji atujengee barabara kwa kiwango cha lami, basi kazi hii aweze kufuatiliwa na atimize wajibu wake.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na barabara hizi ambazo nimezitaja pia tulikuwa na ombi, ile barabara ambayo ilikuwa inatoka Kitai kupitia Ruanda kwenye makaa ya mawe Lituhi kipaumbele sasa kisogezwe mpaka Ndumbi ambako tunajenga bandari mpya kando ya Ziwa Nyasa kwa Mheshimiwa Stella Manyanya. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo pia barabara ya kimkakati pia kiulinzi pia ambayo inatoka Lituhi mpaka Mbamba bay. Barabara hii ni muhimu sana siyo tu kwa uchumi ni kwa watu wa Nyasa na Mbinga pia ile barabara ndiyo ulinzi wa Ziwa Nyasa ukizingatia tunapakana na Malawi ambao hatuwaamini sana mpaka sasa hivi.(Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunazo barabara zingine muhimu ambazo tungeomba pia Wizara ingalie namna gani ya kuzipeleka kwenye ujenzi wa kiwango cha lami. Tunayo hospitali moja ambayo tunaitumia kama hospitali ya Rufaa ya Litembo, ili kufika kwenye ile hospitali tunazo barabara mbili, hii inayotoka Mbinga inapita Myangayanga kwenda Litembo tunayo inayotoka Nyoni - Mbuji kwenda Litembo. Barabara hii bahati mbaya sana kipindi cha masika haipitiki. Wiki iliyopita tu Diwani alinipigia simu kwa sababu ya barabara hii ile hospitali imeshindwa kubeba supplies kutoka Mbinga Mjini kupeleka kule Litembo ili watu waweze kupata huduma.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia nikiri nilimpigia simu Meneja wa TANROADS na alikuwa ameshamtuma mhandisi kwenda kukagua maeneo ambayo ni korofi ili watu waendelee kupata huduma, niiombe Wizara walau barabara mojawapo kati ya hizi mbili ifikiriwe kwenye kiwango cha lami. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, tunayo barabara nyingine iliongelewa pia hapo awali ipo chini ya Mtwara corridor, barabara ya kipande cha Mbinga kwenda Mbamba bay. Barabara hii kwa majibu ya mwaka jana upembuzi yakinifu umekwishafanyika lakini pia uzinduzi wa barabara hii ulifanyika Katavi mwezi wa tatu mwaka jana kwa barabara inatoka Sikonge - Mpanda na hii ya Mbinga Mbamba bay. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwenye mawasilisho ya kitabu cha Wizara ukurasa 28, item namba 50 inaongelea hii ya Katavi, ukienda kwenye ukurasa 244 inapoongelea sasa barabara ya Mbinga - Mbamba bay msimamo wa wizara unatofautiana. Kwenye kipande cha Mbinga - Mbamba bay kitabu kinaeleza kwamba upembuzi yakinifu zimeshafanyika zinatafutwa fedha kwa ajili ya ujenzi. Kwa kipande kile cha kutoka Sikonge - Mpanda unasema kwamba fedha zilikwishapatikana kupitia African Development Bank. Ninachofahamu miradi hii inatekelezwa kwa pamoja kwa nini huku kuwe na status tofauti na huku status tofauti? Mara ya mwisho wakati nafuatilia kwa Meneja wa TANROADS Songea walichoniambia mwezi wa kwanza mwaka huu walikuwa wanarekebisha design ya barabara ya Mbinga - Mbamba bay na hapakuwa na suala la fedha.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri wakati tutakapokuja kufanya Windup utuambie status ya upatikanaji wa fedha hizi, kwa sababu wananchi walishapisha maeneo ili ujenzi wa barabara hii uweze kufanyika mara moja.

Mheshimiwa Naibu Spika, zipo barabara zingine ambazo ni za ngazi ya Mkoa ambazo TANROADS hawakuwahi kupita tangu zipandishwe hadhi …...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, muda wako umekwisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante na naunga mkono hoja.