Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni hii ya leo na mimi nitoe mchango wangu kwenye Wizara hii ya Mawasiliano na Ujenzi.

Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote napenda nitangulize maneno yale ambayo umetuasa jana hapa, ukatutahadharisha kwamba tusitumie maneno mengine tukaonekana ni wahaini baada ya baadhi ya Wabunge kutoka Mikoa ya Kusini wanapoeleza habari hizi kwa uchungu.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo siwezi kuyarudia hayo maneno usije ukanitoa njiani, lakini nataka niwape hadithi moja, hadithi hii nimeipata miaka ya 1980. Rafiki yangu mmoja aliniambia ukijenga nyumba yako usiweke master bedroom Kusini; ukiweka master bedroom Kusini kuna


uwezekano hata ndoa yako isiwe vizuri na familia yako inaweza kubaki maskini. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, akanieleza yafuatayo; anasema ukiangalia ramani ya ulimwengu hebu angalia Visiwa vya Caribbean vinaona jua labda kwa wiki mara moja, mara mbili. Ukirudi kwenye ramani ya Afrika hebu angalia Afrika ya Kusini mpaka leo hawajapata uhuru, Rhodesia, Msumbiji hawajapata uhuru ni kwa sababu wapo Kusini. Ramani ya Tanzania, angalia Mkoa wa Lindi na Mtwara, wakati ule Mkoa wa Mkoa wa Lindi na Mtwara ndiyo adhabu ya wafanyakazi, ukipelekwa kule wewe ni adhabu. Akaniambia hii yote ni kwa sababu tuko Kusini. Kwa hiyo, ukichora ramani ya Tanzania angalia Mkoa wa Lindi na Mtwara ilivyo nyuma ni kwa sababu tuko Kusini. Akasema njoo uchore ramani ya Dar es Salaam hebu angalia Wilaya ya Temeke na Kinondoni, ana maana kwamba ukiweka master bedroom Kusini utabaki kuwa maskini, ndiyo maana leo mtu wa Kusini akisema anasema kwa uchungu hayo tunayoyasema. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, reli inayoongelewa ya Tanga
- Moshi, Mjerumani aliijenga ile reli kutoka Mtwara kwenda Nachingwea. Wakati ule Mtwara na Lindi tulikuwa na pamba, katani, korosho na karanga ndiyo maana akajenga ile reli. Sisi tulipopata uhuru, tukaihamisha ile reli ikaenda Tanga na mkonge ukahamia Tanga, pamba ikahamia Tanga tukabaki maskini. Tunaposema hamtuhitaji nchi hii tunamaanisha. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mkitaka kuona hilo, je, watu wa Kusini kosa letu kwenye nchi hii ni nini? Hiyo barabara ambayo inaongelewa ya Kibiti - Lindi, mimi wakati nasoma nikiwa form four ndiyo barabara ya Kibiti- Lindi imeanza kuletewa pesa. Mwaka 1984, vifaa vilikuja na Nangurukuru vya kumaliza hiyo barabara, hiyo barabara imeshajengwa na Marais wangapi? Wanne, hiyo iko Kusini.(Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 1987 natoka Dodoma nakwenda Singida, barabara ni ya vumbi, lakini barabara ya Singida na ya Kibiti - Lindi ipi imeanza kuisha? Mnataka tuseme nini? Naomba Serikali ya Awamu ya Tano mfungue Mikoa ya Lindi na Mtwara. Muufungue Mkoa wa Lindi na Mtwara kwa barabara na kwa mawasiliano, hapo mtakuwa mmetutendea haki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, barabara ya Nangurukuru- Liwale; Nachingwea - Liwale na Liwale - Morogoro zimeshaongelewa sana sina haja ya kuzirudia, lakini kwa sababu mimi ndiyo mwenye hizo barabara wanasema chereko chereko na mwenye ngoma. Wabunge wengi hapa mmesema tuende kwenye sera, Mbunge aliyepita amesema tuende kwenye sera, kama tumeamua kuunganisha Mkoa hadi Mkoa basi nasi mtuunganishe na Morogoro mtungaanishe na Ruvuma. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze kwenye Wilaya ya Liwale. Walio wengi hapa wakisimama wanasema Wilaya zao mpya, mikoa mipya, Wilaya ya Liwale ina miaka 42. Sasa kama kuna mtu Wilaya yake mpya anadai barabara na sisi ambao tuna miaka 42 hatuna barabara tuseme nini? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, Wilaya ya Liwale haina mawasiliano ya simu, haina mawasiliano ya barabara na leo hii Liwale hapa ninapoongea siwezi kwenda, barabara hakuna na nikienda kule wanaweza wakanipiga hata mawe. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu upande wa mawasiliano ya simu. Namuomba Waziri atuletee mawasiliano, kata zifuatazo ili kuweza kupata mawasiliano ya simu ni lazima uende zaidi ya kilometa tano, 10 mpaka
12. Kata ya Mpigamiti, Kikulyungu, Kimambi, Lilombe, Mlembwe, Mkutano, Ngunja, Ngongowele, Ngorongopa, Pengere, Makinda, Mirui, Mikunya, Naujombo, Nahoro, Mtawango, Makololo na Gongowele hizi zote hazina mawasiliano.

Mheshimiwa Naibu Spika, kata ya Mpigamiti ndiyo kata anayotoka huyu anayeongea sasa hivi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, nakuomba sana Serikali ya Awamu ya Tano, hebu muifungue Liwale na Lindi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, juzi nikiwa kwenye Kamati, niliambiwa vigezo vya barabara kupata lami wakasema magari lazima yafike 300, nikawaambia kama kigezo ndiyo hicho, Liwale hatutapata barabara ya lami mpaka Yesu arudi. Kwa sababu karavati walizojenga kwenye hiyo barabara magari makubwa hayaendi na tayari wameshapunguza magari. Mfano, masika kama sasa hivi watu wanazunguka kupitia Lindi, hiyo barabara itafikia magari 300 lini? Siyo kweli kwamba hii barabara haiwezi kufikia magari 300.

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri naomba nikuambie barabara ya Nangurukuru – Liwale ukiipa lami, hakuna msafiri atayekwenda Masasi na Tunduru, atakayepitia Lindi au Mtwara lazima wapitie Liwale kwa sababu ndiyo shortcut, lakini leo hii Liwale inaonekana iko kisiwani kwa sababu hatuna barabara.

Kwa hiyo, barabara hii ni barabara ya kiuchumi siyo kweli kwamba ni barabara ya huduma. Liwale tunalima korosho, Mkoa wa Lindi ndiyo tunaongoza, tunalima ufuta, tunalima viazi. Sasa kama siyo uchumi huu ni kitu gani? (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nirejee kwenye ubora wa barabara, juzi tulipokuwa kwenye Kamati tulikagua barabara. Mimi nilisikitika sana yule engineer alinieleza barabara ile haina hata mwaka imeanza kuweka crack, namuuliza anasema unajua hapa wali-estimate vibaya kumbe level ya maji (water table) ile kwamba walikadiria iko juu kumbe iko chini sana, kwa hiyo, barabara imebomoka wanarudia. Nikamwambia hawa wanaofanya feasibility study, sijui upembezi wa kina, wanafanyaje?

Mheshimiwa Naibu Spika, mimi ninavyofahamu kila mita 50 panachukuliwa udongo wanafanya sampling, wanapeleka maabara kupata historia ya hiyo barabara. Ndiyo maana tunashindwa kuwakamata wakandarasi mara nyingi makosa yanakuwa siyo yao. Haya mambo ya upembuzi yakinifu, upembezi wa kina, mtu yuko ofisini anapiga simu tu, eeh bwana hiyo barabara kutoka mahali fulani, kuna mto gani hapo? Huo mto ukoje? Anachora tu, eeh, jamani tuende kwenye field! (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, haingii akilini mtu aniambie kwamba ile barabara pale maji yanafoka ndiyo maana barabara haidumu, hukuyaona? Hapa tunapoteza pesa bure, lakini tatizo siyo wakandarasi, tatizo kubwa liko kwa upembuzi yakinifu na usanifu wa kina, wataalamu wanabaki ofisini wanafanya upembuzi yakinifu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho kabisa tunazungumzia upande wa bandari. Nchi hii ni ya ajabu sana, leo hii hatuna hata lengo kusema kwamba kwenye nchi yetu hii ni mizigo tani ngapi tupitishe majini na mingapi tupitishe kwenye reli. Leo hii Mtwara kuna bandari lakini hii bandari haitumiki. Juzi hapa tumepata shida na mazao ya korosho, Mtwara kumejaa korosho maghala yote, meli hakuna, hii bandari mbona hatuitumii? Tumerogwa na nani sisi? Tatizo liko wapi? Hakuna nchi ya ajabu kama hii. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, leo hii nchi hii bado inasafirisha mizigo mikubwa kwa malori, halafu bado tunawalaumu wakandarasi wanajenga barabara chini ya kiwango, hii si kweli, haiwezekani! Tunayo bandari ya Tanga mwambao wote ule Mtwara, Lindi, Dar es Salaam, Tanga, Bagamoyo bado tunasafirisha mizigo kwa magari, hii ni aibu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri kwamba umefika wakati Serikali wapange kwamba tunataka tusafirishe mizigo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.