Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutupa nafasi nyingine tena mchana huu ili tuweze kuitendea haki hotuba ya Waziri wa Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa namna ya pekee nakushukuru wewe mwenyewe kwa kunipatia nafasi hii ili niweze kutoa mchango wangu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza kabisa naanza kwa kuunga mkono hoja hotuba ya Mheshimiwa Waziri. Wizara hii ndiyo ambayo kwetu sisi Wakristo, kuna maneno fulani yamo kwenye vitabu vitukufu, yanasema: “Tazama nakwenda kufanya nchi mpya na mbingu mpya, ya kale yamepita na tazama yamekuwa mapya.” Nchi hii tunaiona inavyobadilika.
Mheshimiwa Naibu Spika, tunaona Tanzania mpya inakwenda kuzaliwa. Unaweza ukaona kuanzia Mwalimu Nyerere mpaka Rais Kikwete, makao makuu ya nchi hii yalikuwa Dar es Salaam; kuanzia kwa Rais Magufuli, makao makuu ni Dodoma sasa. Kuanzia mkoloni, Nyerere mpaka Rais Kikwete tulikuwa na meter gauge, kuanzia Mheshimiwa Magufuli na kuendelea tunakwenda kuwa na standard gauge. Hiyo ndiyo Tanzania mpya tunayoitaka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pale Rais wetu alipokuwa Mgombea, aliimbia Tanzania na Dunia nzima, watu wakataka kwenda mahakamani akasema, M for change, wakasema ameibia sera fulani, lakini alikuwa anasema Magufuli for Change na M4C hiyo kweli tunaiona. Hongera Rais wetu. Tunaweza tukasema hakika ya kwamba huyu anaweza akawa ni miongoni mwa Manabii wa kizazi kipya.
Anaitabiria Tanzania mambo mazuri na kila mmoja anaona. Kwa maana hiyo niseme, Wizara ya Miundombinu kwa maana ya Ujenzi, Uchukuzi na Mawasiliano ndiyo inakwenda kuifanya Tanzania hii iwe mpya ili hata Mataifa mengine watakapokuja hapa, watauona uso wa Tanzania ukiwa umepambwa na flyovers, ukiwa na madaraja ambayo yako kwenye viwango, ukiwa na treni ambazo zinakwenda kwa haraka. Kwa maana hiyo, hata uwekezaji katika Taifa hili utakuwa ni wa uhakika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, sekta nyingine muhimu za viwanda, uzalishaji, kilimo, zinategemea sana ni namna gani tunavyokuwa na mawasiliano ya haraka. Hata Mwekezaji akija hapa, atapenda sana kuona ni namna gani itakavyoweza kuwa anasafirisha bidhaa zake kama ata- import au ata-export, muda gani anautumia hapo? Ndipo tutaona kwamba watu hawa wanaweza wakaja kutusaidia na tukaenda kwenye Tanzania ya viwanda tunayoitaka. (Makofi)
Mheshimwa Naibu Spika, naomba niseme neno moja ambalo napenda Watanzania walisikie, kwamba kuna baadhi ya Watanzania wanafanya michango yao katika Taifa hili, wakati mwigine wasitambuliwe. Nichukue hata dakika chache kumsifu bwana mmoja anaitwa Engineer Patrick Mfugale. Amekuwa ni chachu katika TANROADS na hata sasa kwa wale wasiojua, ndiye anayeongoza timu inayojenga standard gauge ya Tanzania. Kwa maana hiyo, mtu huyu ni hazina ya nchi hii na hongera sana kwake. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika suala zima la miundombinu ya barabara hasa Jimboni kwangu. Namuomba Mheshimiwa Waziri, barabara yetu ya Mtengorumasa – Iparamasa - Mbogwe mpaka Masumbwe inayotuunganisha Watanzania na watu wa Uganda na Mikoa jirani ya Kagera, Geita, Shinyanga, Tabora mpaka Dar es Salaam, ijengwe kwa kiwango cha lami. Watanzania wa maeneo haya na wenyewe wangependa kufaidi keki ya nchi hii kwa kupata sehemu ya keki hiyo kupitia barabara ya lami kwenye barabara hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ipo barabara ya kutoka Kahama mpaka Geita, nashukuru ipo kwenye bajeti ya
mwaka huu, naomba utekelezaji wake ufanyike haraka iwezekanavyo. Pia, niende haraka sasa, niseme tu kwamba Bandari ya Dar es Salaam ndiyo lango kuu ambalo nchi nyingi zinategemea.
Mheshimiwa Naibu Spika, namwomba Mheshimiwa Waziri, wakati wa uongozi wake, ahakikishe yale magati namba moja mpaka saba, uchimbaji wake ufanyike kwa haraka; na gati namba 13 na 14 ambayo yalikuwa yakipigiwa kelele kila wakati katika Bunge hili, ujenzi wake ukamilike. Bandari za Tanga, Bagamoyo na Mtwara, nazo zipewe umuhimu wa pekee. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa standard gauge hatua ya kwanza umeanza, naomba na mchakato wa hatua zile nyingine zilizosalia ukamilike ili kwamba ile ndoto ambayo tumekuwa tukiiwaza kwa muda mrefu, Tanzania inayokwenda kuwa na barabara nzuri na treni inayokwenda kwa kasi inayotumia umeme, iweze kufikiwa kwa haraka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi hii inayo majaliwa ya kuwa na madini mengi; tuna Mchuchuma, Liganga, tuna nickel kule Kabanga na graphite kule Lindi. Maeneo haya yote uchimbaji wake utategemea sana miundombinu ya barabara na Reli zitakazojengwa na Wizara hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, niwatie moyo tu viongozi wa Wizara hii, wapige kazi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la ununuzi wa ndege mpya, nalo ni maono mapya ya Mheshimiwa Rais wetu, nayo yanafanyiwa kazi. Tumuombee Mungu ndoto yake hii iweze kutimia katika kipindi cha uongozi wake. Ndiyo Tanzania mpya hiyo itakayokuwa na Shirika la Ndege la Kimataifa na ndiyo tunayoitaka. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na niunge mkono hoja. Ahsante sana.