Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Prof. Palamagamba John Aidan Mwaluko Kabudi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kilosa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria

WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kuniwezesha kutoa hotuba yangu leo asubuhi na kuwawezesha Waheshimiwa Wabunge kuchangia hotuba ya Wizara yangu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna ya pekee, nachukua fursa hii kukushukuru wewe binafsi, kwanza kwa mchango wako mkubwa kwangu katika taaluma ya sheria. Mimi na Dkt. Harrison George Mwakyembe baada ya kuhitimu Shahada ya Sheria wakati wa mafunzo ya sheria, tukiwa State Attorney grade III Mheshimiwa Chenge ulikuwa Mkurugenzi wa Mambo ya Kimataifa na ulitusaidia sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru pia, kwa miaka mitano niliyoazimwa katika Ofisi ya Makamu wa Rais kushughulikia mambo ya mazingira, ambapo tulifika tukatunga Sheria ya Mazingira ya mwaka 2004, wewe ulikuwa msaada kwangu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakumbuka, naomba niliseme ndani ya Bunge hili, kazi ya Muswada ule haikuwa rahisi, ilinizulia watu wengi na maadui wengi, wengine walioona husuda ya fedha niliyolipwa; na wengine ambao hawakuelewa kwa nini sheria ile itungwe. Kwenye kikao kimoja unakumbuka nilitolewa kwa hali iliyokuwa haikunifurahisha. Hata hivyo, wewe uliniambia jambo moja na leo nataka niliseme; “In public service, learn to swallow your pride. In public service learn to suppress your eagle.” Kweli mambo hayo sasa naona umuhimu wake ndani ya jengo hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mheshimiwa George Masaju, Mwanasheria Mkuu wa Serikali kwa ushirikiano alionipa katika kutekeleza majukumu yangu na kwa kuungana na mimi katika kujibu baadhi ya hoja zilizotolewa na Waheshimiwa Wabunge. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mara nyingine, naishukuru Kamati ya Kudumu ya Bunge la Katiba, Sheria na Utawala pamoja na Kamati ya Bajeti kwa maoni na ushauri wao ambao wameipatia Wizara na Taasisi zake katika kutekeleza majukumu yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nizihakikishie Kamati na Waheshimiwa Wabunge wote kuwa tumepokea maoni, hoja na ushauri mliotupa katika mjadala wa Bajeti yetu na tunaahidi kufanyia kazi masuala yote yaliyojitokeza katika mjadala huu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Kambi ya Upinzani, nashukuru pia kwa maoni yenu yaliyotolewa na kukubaliwa na Bunge hili kutoka kwa Msemaji wa Kambi ya Upinzani wa mambo ya Katiba na Sheria; ni mdogo wangu, kaka yake Mheshimiwa Tundu Lissu, Ndugu Alute Mughwai na mimi tumesoma pamoja Milambo. Kwa sababu hayupo, sipendi kuleta mambo ya mila hapa ndani, lakini wale wote tunaotoka Singida mnajua mila yetu na heshima kwa watu, eeh, kwa neno lililokataliwa jana, waliotangulia kwa ngariba kabla ya wewe. (Makofi/Kicheko)
Mhesimiwa Mwenyekiti, niseme hili, nimeshangaa sana kuwa watu katika jengo hili kubagazana. Waheshimiwa Wabunge kama ni kawaida, ni kawaida mbaya. Hatuwezi kubagazana. Jengo hili siyo la kubagazana; na tunabagazana kwa sababu kwa bahati mbaya tumepoteza pia uelewa mzuri wa lugha ya Kiswahili. Tunazungumza Kiswahili kikavu kama alivyosema Mheshimiwa, Riziki Shahari Mngwali, tumepoteza uelewa wa Kiswahili wa kutumia lugha ya kumfanya mtu mpuuzi ajue ni mpuuzi bila kumwambia mpuuzi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ukimsikia muingereza anakwambia your stupid, siyo muingereza. Muingereza mstaarabu ndani ya Bunge, atakwambia I am sorry, your level of appreciation of issues is diminishing, which means you are stupid! Yes. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ugeni una faida wa kusema mambo ambayo hayakufurahishi. Nimefundisha wanasheria, na mimi nimefundishwa. Mwanasheria yeyote worth being called a lawyer, he must have sense of respect and more so, as officer of the court to the judiciary. Ndiyo maana naanza kuelewa kwa nini nchi nyingine Bajeti ya Mahakama hailetwi Bungeni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa vitu ambavyo vinanisumbua na nilisema siku ya hotuba ya Mheshimiwa Mbowe na ninamheshimu sana kwa maturity yake, niliomba tusii-drag judiciary in our mucky politics. It is abominable! It is flabbergasting! Tusii-drag Mahakama katika mazungumzo yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nitaanza na suala la uteuzi wa Majaji, ikiwa ni pamoja na Jaji Mkuu na naomba mnisikilize; na kama hamniheshimu kwa umri wangu, I am above 60, mniheshimu kwa utu wangu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, unajua nafasi ya Rais inagombewa, anachaguliwa…
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafasi ambayo ndiye mkuu wa nchi, naomba mnisikilize.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nafasi ya Rais tunayempigia kura, Rais wa Tanzania, Rais wa South Africa hapigiwi kura, anachaguliwa na Wabunge kama alivyo Waziri Mkuu. Ndiyo maana South Africa chama ni juu. Rais Zuma, chama kinaweza kikamwondoa leo, ndiyo kama kilivyomwondoa Mbeki. Hapigiwi kura. Lakini Rais wa Jamhuri ya Muungano Tanzania, anapigiwa kura. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Spika wa Bunge, anapigiwa kura. Mtu pekee wa mhimili ambaye hapigiwi kura, anateuliwa, ni Jaji Mkuu. Mnajua kwa nini?
Ni msingi wa kuhakikisha mtu huyu anayeteuliwa kushika nafasi hiyo, aachwe bila laumu ya mpumbavu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme hivi, katika uteuzi wa Jaji, nafasi ya Jaji katika hili, kwanza siyo kweli kwamba hapajawahi kuwa na Kaimu Jaji Mkuu kwa kipindi. Mara baada ya Jaji wa mwisho wa Tanzania, muingereza Windham kumaliza muda wake, Tanzania 1965, Mwalimu hakuona sababu ya kuwa tena na Jaji Mzungu. Ndipo jitihada zilianza za kutafuta Jaji mwafrika na huyo Jaji alipatikana kutoka nchi ya Trinidad and Tobago Telford Philip Georgies. Ilichukua muda kwa sababu Majaji walikuwa wanasita kuja kwa sababu ya elimu ya watoto wao. Ni mwafrika, tena alikuwa mweusi kuliko wewe.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa vitu nawasifu waafrika, wamekaa kule miaka 500, wengine ni weusi kuliko sisi; na ni Waafrika kuliko sisi kwa sababu wameishi ugenini. Ndipo nafasi ile ilikaa kwa kipindi kirefu ikisubiri Jaji Telford Philip Georgies afike nchini aapishwe. These are facts. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, alichaguliwa mwingine akaimu kwa sababu daima nafasi ya Jaji Mkuu haiwezi kuwa wazi hata kwa dakika moja. Ndiyo maana hata Jaji Mkuu akisafiri, akiteuliwa mwingine kukaimu, anaapishwa. Hakuna Kaimu Jaji Mkuu ambaye haapishwi, hata kama atakuwa Kaimu Jaji Mkuu kwa siku mbili, ataapishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ukiangalia Katiba, iko wazi kabisa, inamruhusu Rais kuteua Kaimu Jaji Mkuu na haiweki mipaka. Haiweki, haiweki.Ukienda kwenye Katiba mpaka mwaka 2000 wakati Mwenyekiti akiwa Attorney General kabla ya hii 2005 kufanya marekebisho kupunguza maneno, niwasomee tafsiri ya Jaji Mkuu ilikuwa inasemaje. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Jaji Mkuu maana yake ni Jaji Mkuu wa Mahakama ya Rufani aliyetajwa katika Ibara 115(1) ambayo sasa ni 118 ya Ibara hii, ambaye ameteuliwa kwa mujibu wa masharti ya Ibara ndogo ya pili ya Ibara hiyo ya 118 au iwapo Jaji Mkuu hayupo au anashindwa kutekeleza kazi zake kwa sababu yoyote, Kaimu Jaji Mkuu aliyeteuliwa kwa mujibu wa masharti ya Ibara 118(4) ya Katiba hii na Kaimu Jaji Mkuu naye hayupo au anashindwa kutekeleza kazi yake, Jaji Mkuu, Jaji wa Mahakama ya Rufani aliyeko kazini kwa wakati huo na ambaye yuko kwenye daraja la juu zaidi la madaraka kupitia Majaji wote wa Mahakama waliopo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiisoma ya sasa inaeleza wazi kabisa Jaji Mkuu ni nani, maana yake ni Jaji Mkuu anayetajwa kuteuliwa na ambaye majukumu yake yameelekezwa katika Ibara ya 118 ya Katiba. Ukiisoma hiyo ni pamoja na Kaimu Jaji Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maana yake nini? Watu wengine wote wanaoteuliwa kukaimu, hawaapishwi. Ni Jaji Mkuu tu. Kaimu Jaji Mkuu anaapishwa, peke yake.Maana yake, kitendo cha kumwapisha kinampa mamlaka na ulinzi kamili wa cheo hicho. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu uteuzi wa Jaji Mkuu, mimi nalisihi Bunge liheshimu Mamlaka ya Uteuzi. Rais anayo mamlaka kamili ya uteuzi na Rais anavyo vigezo vingi vya uteuzi na Rais msidhani ni mtu anayetembea, ni taasisi. Hivyo, kwa sababu ni taasisi, haina macho mawili tu, ina zaidi ya macho mawili, tuiache ifanye kazi yake. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwasihi sana Waheshimiwa Wabunge, tuache Kaimu Jaji Mkuu afanye kazi yake. Tusimfikishe mahali tukamtweza. Kwa sisi wanasheria, tuheshimu sana mhimili huo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo napenda nilizungumzie ni kuhusu Rais. Ndiyo maana dada yangu Mheshimiwa Riziki Shahari Mngwali ametoa, ni kweli alichokisema. Kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba tulikuwa na Kamati tatu; Kamati ya Maadili na Haki za Binadamu chini ya Mzee Ussi, Mwenyekiti; Kamati ya Muungano, chini ya Mzee Butiku, Mwenyekiti na Kamati ya Mihimili, mimi nikiwa Mwenyekiti. Watu walionisaidia sana, nikiri ni Kibibi Mwinyi Hassan kutoka Unguja, Zanzibar na Mheshimiwa Riziki Shahari Mngwali kutoka Tanzania Bara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati wa kuzunguka kule tulikuta nafasi ya Rais watu hawaielewi. Nimekuja na maoni hapa na mengine nimeyaacha. Watu hawaelewi nafasi ya Rais, yaani kama kuna nafasi ilikuwa inazungumzwa mpaka tunashtuka, ni nafasi ya Rais, mpaka tukajiuliza hawa Watanzania kwa nini nafasi hii hawaielewi? Tukabaini, tunachanganya mambo mengi katika nafasi ya Rais. Ndiyo maana tukasema, ni vyema tukapambanua tuelewe nafasi ya Rais na Rais ni nani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais anazo nafasi tatu; moja, ni Mkuu wa Nchi (Head of State); pili, ni Kiongozi wa Serikali na tatu ni Amiri Jeshi Mkuu. Sasa yako madaraka ya nafasi ya Rais kama Mkuu wa Nchi na kama Amiri Jeshi Mkuu yanayompa hadhi tofauti ambayo haistahili kubezwa na ndiyo maana Bunge kwa Kanuni limezuia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja, Rais ni taswira ya nchi. Kwa nafasi yake ya Mkuu wa Nchi Rais ni taswira ya nchi. Malkia wa Uingereza kwa nafasi yake ya ukuu wa nchi, ni taswira ya nchi (Head of State). Kwa maana hiyo, yeye ndiyo alama ya umoja, yeye ndio alama ya uhuru wa nchi na mamlaka yake. Kumuonesha kwamba yeye ni alama ya uhuru wa nchi, ndiyo maana Rais peke yake anafuatana na mtu ambaye tumezoea kumwita mpambe, ambaye amevaa mavazi ya kijeshi. Maana yake ni kwamba anawaonyesha kwamba huyu ndiye alama ya Serikali yenu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo Rais ana dhamana ya kukuza na kuhifadhi umoja wa kitaifa, ana dhamana hiyo. Sasa ukiangalia madaraka ya Mkuu wa Nchi, yale huwezi kuyapunguza; lakini ukiangalia mamlaka yake ya Amiri Jeshi Mkuu, huwezi kuyapunguza na ukiangalia mamlaka yake kama Mkuu wa Serikali, kwa mujibu wa Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania majukumu ya Rais kama Mkuu wa Serikali, akiwa Mkuu wa Serikali, hayo unaweza kuyapunguza. Unaweza kuyasimamia, unaweza kuyadhibiti. (Makofi)
Mdogo wangu Tundu Lissu asubuhi ameeleza zile makala ya mimi na Mlimuka na ya Mheshimiwa Dkt. Harrison Mwakyembe tuliyoandika wakati wa mfumo wa chama kimoja, tena tukielekea mabadiliko makubwa ya Katiba ya mwaka 1985. Niseme hivi, mwaka 1985 hii Katiba, Mzee Chenge yuko hapa, kwa maudhui hii siyo Katiba ya mwaka 1977, ni Katiba ya mwaka 1985. Iliandikwa yote upya. Kwa nini ilitwa Katiba ya mwaka 1977, ni kwa sababu The Constituent Assembly haikuwa convened. (Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwa sababu Constituent Assembly haikuwa convened na kwa nini Mwalimu haku-convene Constituent Assembly?
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni kwa sababu wapo watu wanaoamini the Constituent Assembly is only convened once. Only convened once. Ndiyo maana nilipokuwa amidi, Kiswahili cha dini ni amidi. Nilipokuwa amidi wa Shule Kuu ya Sheria, nimeanzisha course mpya ya Legal History na nimeifundisha mwenyewe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini nilianza course ya Legal History? Ni kwa sababu niligundua vijana wetu wengi wanaidhani Tanzania ni hii ilivyo leo. Hii ilivyo leo haikuwa hivi. Kabla ya mabadiliko yale, Bunge hili Wabunge wengi humu ndani walikuwa ni wa kuteuliwa na siyo wa kuchaguliwa, ndiyo! Tena nina fahari sana ya kuwa Mbunge wa Kuteuliwa, ndiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitawaambia kuwa sisi wasomi hakuna Doctorate unayoiheshimu kama Honorary (Honoris Causa), ndiyo. Unapokuwa Doctor Honoris Causa, tena ukiwa multi…
Kwa hiyo, wakati huo Waziri Mkuu yuko hapa hakuwa Mbunge wa kuchaguliwa, walikuwa ni Wabunge wa kuteuliwa. Ndiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo, Bunge lilikuwa ni Kamati ya Halmashauri Kuu ya Chama. Sasa mtu asiyejua historia atabeza mafanikio yaliyofikiwa.
Ndiyo maana Wangazija wana msemo, ukitaka kujua mafanikio ya mtu usiangalie kimo alichofika, angalia shimo alikotokea. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niseme mara baada ya kile kitabu kutoka, ndugu yangu Mheshimiwa Dkt. Harrison George Mwakyembe yupo, wako Mabalozi waliodhani Mwalimu angetutia kizuizini, yuko hapa. Leo ninyi mnaongea Sheria ya Kizuizini hayupo! Tuliongea wakati yupo. Don’t dare me, don’t dare me. We spoke when the law was law and when the President was President. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndiyo maana Katiba hii kwa mapendekezo ya wakati huo Mwalimu anaondoka ilikubaliwa kabisa, lazima madaraka ya Rais yapunguzwe. Someni mapendekezo ya Halmashauri Kuu ya Taifa ya mwaka 1983/1984 na yalipunguzwaje? Moja ya kuyapunguza ilikuwa ni kuanzisha cheo cha Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi Uwaziri Mkuu wetu huu, siyo kama wa Uingereza, huu ni kama wa Ufaransa. Kwa sababu ni kama wa Ufaransa ambapo Mzee Joseph Sinde Warioba alitumwa kwenda kujifunza, Mzee Msekwa alitumwa India na Canada, Waziri Mkuu wetu huyu mkisoma Katiba anatokana na chama chenye Wabunge wengi na anapigiwa kura ndani ya Bunge. (Kicheko/Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, aina hii ya Katiba yetu ambayo una Mkuu wa Nchi ambaye amechauguliwa na wananchi moja kwa moja, siyo kama wa Afrika Kusini na una Waziri Mkuu anayetokana na chama chenye Wabunge wengi au anayeungwa mkono na wengi, kinaweza kukupa aina ya government inayoitwa kwa Kifaransa kohavision.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa namna hiyo, madaraka ya Rais yakawa yamepunguzwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili kubwa lililofanyika mwaka huo, ilikuwa ni kuweka ukomo wa Rais. Mwalimu alitawala kama Rais miaka 23, anaondoka madarakani sisi ilikuwa ndiyo nchi ya kwanza Barani Afrika kuweka ukomo wa Rais kuwa ni vipindi viwili vya miaka mitano mitano. Eeh, kule Cameroon, Rais Ahidjo; Wafaransa walipomchoka Rais Ahidjo, wakamwambia anaumwa; alipoondoka akagundua haumwi, hawezi kurudi. Rais Sédar Senghor wa Senegal alikuwa ndiye Rais wa pili kung’atuka na yeye kuweka term limit. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la tatu muhimu ndani ya Katiba hii, lilikuwa ni kuweka sura ya haki za binadamu. Hazikuwepo wakati huo, hazikuwepo. Ndizo hizo leo, Ibara ya 12 mpaka ya 29, hazikuwemo. Hayo ndiyo maendeleo na mapito ambayo nchi hii imeyapitia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mabadiliko ya mwaka 2005 kuhusu haki za binadamu, yaliyondoa clawback clauses zote. Tena yalikwenda mbali, hayakuondoa tu clawback clauses, yaliondoa hata enabling clauses.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachotaka kusema katika mambo ya Katiba, eeh, lecture room, kwa sababu Waswahili wana msemo, mwana wa muhunzi asiposana hufukuta. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ndugu zangu, tumefika hapa tulipofika kwa sababu nchi hii imejaliwa kuchukua maamuzi kwa wakati, lakini maamuzi hayo ni lazima yajenge umoja wa Taifa, maamuzi hayo ni lazima yajenge mshikamano, ni lazima yajenge utu, ni lazima yalenge ustawi wa watu. Ndiyo maana katika Katiba hii kama kuna Ibara naisoma kila siku, ni Ibara ya nane. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, at the bottom line wananchi ndio source ya mamlaka yote, sio sisi. Kwa hali hiyo, nashauri sana tutunze heshima ya Rais akiwa Mkuu wa Nchi, tutunze heshima ya Rais akiwa Amiri Jeshi, lakini inapokuja kwenye nafasi ya ukuu wa Serikali, isimamiwe na ishauriwe. Hapa ndani ni kupitia kwa Waziri Mkuu na Baraza la Mawaziri lililomo humu ndani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja mbalimbali zimetolewa, jumla ya Waheshimiwa Wabunge 24 wamechangia hotuba yetu ambapo Wabunge 17 wamechangia kwa maandishi na Wabunge saba wamechangia kwa kuzungumza. Miongoni mwa mambo ambayo yamezungumzwa, yako ambayo yamegusa vyombo na mambo mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na hoja zilizotolewa kuhusu Mahakama; hoja kubwa iliyotolewa na Mahakama ni kuhusu ujenzi wa majengo ya Mahakama. Ujenzi wa majengo ya Mahakama Kuu, za Wilaya na za Mwanzo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kueleza kwa ujumla kwamba moja ya changamoto kubwa zinazoikabili Mahakama ya Tanzania ni uhaba na uchakavu wa miundombinu. Mathalani katika ngazo ya Mahakama za Wilaya, tuna majengo katika Wilaya 30 na Wilaya nyingine huduma zinatolewa katika majengo ya kuazima kutoka taasisi nyingine za Serikali. Aidha, tuna Wilaya 23 zinapata huduma za Mahakama katika Wilaya za jirani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwa upande wa Mahakama za Mwanzo kuna Mahakama 960 tu kati ya Mahakama 3,963 zilizopo nchini. Sasa katika kukabiliana na changamoto hii, Wizara kwa kushirikiana na Mahakama imeanza kutekeleza mpango wa ujenzi katika ngazi zote za Mahakama. Kwa hiyo, kupitia mpango huo, katika kipindi cha miaka mitano tumepanga kuhakikisha kwamba mikoa yote itakuwa na majengo ya Mahakama, ndani ya miaka mitano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika hiyo miaka mitano, imepangwa kujenga Mahakama za Wilaya 109 na Mahakama za Mwanzo 150 katika maeneo mbalimbali nchini. Kwa hiyo, kwa msingi huo ni matarajio yetu kuwa hadi mwaka 2021 Wilaya zote nchini ziwe na majengo ya Mahakama, huo ndiyo mpango. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika mpango huo yapo maeneo ambayo tunaomba msaada, moja likiwa Jimbo la Mheshimiwa John Mnyika, tusaidiwe kupata viwanja, mahali ambapo tunaweza tukajenga Mahakama na pia Wilaya nyingine. Nimetaja yako Mheshimiwa Mnyika kwa sababu nimeona umeleta mchango wako kwa maandishi na nimeu-note. Sasa tukishapata viwanja hivyo, itatusaidia sisi kuweza kujenga Mahakama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limeelezwa na michango ya Waheshimiwa Wabunge wengi ni kuhusu Mahakimu wa Mahakama ya Mwanzo kukaa muda mrefu katika kituo kimoja. Sasa hili limechangiwa na gharama za uhamisho na vituo vya kuhamishwa kwa watumishi wote wa Mahakama ambao ni pamoja na Mahakimu wa Mwanzo. Gharama ya zoezi hili inakwenda takriban shilingi bilioni 2.3.
Kwa hiyo, Wizara yangu kwa kuthamini kwamba ni vyema Mahakimu au Mahakama za Mwanzo wakawa wanapata uhamisho, kwa sababu kukaa mahali pamoja muda mrefu na wewe unakuwa sehemu ya ile jamii.
Kwa hiyo, tunashirikiana Wizara na Mahakama kuhakikisha kwamba tunaongea na Hazina ili kulifanyia suala la upatikanaji wa fedha za uhamisho wa watumishi wakiwemo Mahakimu waliokaa kituo kimoja kwa muda mrefu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo limezungumzwa kuhusu Mahakama ni juhudi za kuondoa mlundikano wa mashauri katika ngazi zote za Mahakama. Sasa Mahakama ya Tanzania pia imeweka muda maalum wa mashauri kuwa mahakamani. Kwa Mahakama za Hakimu Mkazi na Mahakama za Wilaya, shauri linatakiwa kukaa mahakamani kwa muda wa miezi 12. Mahakama za Mwanzo, shauri linatakiwa kukaa muda wa miezi sita tu. Kwa Mahakama za Mwanzo hazina mashauri yanayozidi miezi sita. Sasa kama ambavyo tumeeleza katika hotuba yetu na maelezo ya Mahakama, Mahakama ya Tanzania imejiwekea mpango wa kuondoa mlundano wa mashauri katika ngazi zote za Mahakama, iwe ni Mahakama ya Hakimu Mkazi au ya Wilaya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia katika Mahakama ya Hakimu Mkazi na Mahakama ya Wilaya zina mashauri 2,912 yanayoangukia kwenye mlundikano. Mashauri hayo yako katika Programu Maalum ya Uondoaji wa Mlundikano wa Mashauri inayoendelea nchi nzima. Nachukua fursa hii tena kuipongeza Mahakama kwa kazi kubwa waliyoifanya katika kuhakikisha kwamba kesi zote za uchaguzi wa Wabunge na Madiwani zinamalizika ndani ya muda uliopangwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili ni la kihistoria na ni vyema tukaipongeza Mahakama, kwa sababu ni mara ya kwanza kesi za kupinga matokeo ya uchaguzi zimemalizika katika kipindi kifupi. Huko nyuma tunafahamu, mpaka kipindi cha Bunge kilikwisha kesi bado zinaendelea Mahakamani. Kwa hiyo, ni imani yangu kwangu kwamba rasilimali fedha ikiongezeka, uhamisho wa Mahakimu utafanyika, ajira zaidi zitapatikana na majengo ya Mahakama zaidi yatajengwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulizungumzia ingawa Mwanasheria Mkuu wa Serikali amelizungumzia na mimi pia napenda nilizungumzie. Suala lolote linamlohusu Mtanzania yeyote au mtu yeyote kufunguliwa mashtaka na kupelekwa Mahakamani au
kuwekwa mahabusu au rumande, siyo suala ambalo mtu yeyote angelifurahia. Tungependa uhalifu usiwepo, tungependa wahalifu wasiwepo, lakini hulka ya binadamu, tunatenda makosa. Makosa yakitendeka kwa mujibu wa sheria, lazima mtu aitwe, ahojiwe, kesi ifunguliwe. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, nimeanza na hilo, niliseme wazi. Serikali haifurahii kuona watu wako ndani. Ingetokea muujiza leo pakawa hakuna uhalifu na Magereza yakafungwa, lingekuwa ni jambo la furaha kubwa sana, lakini huo ni utashi na mapenzi ambayo ni vigumu kuyatekeleza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kama alivyosema Mwanasheria Mkuu wa Serikali, moja ya mambo ambayo yamezungumzwa sana humu ndani, ni suala la kesi inayohusu Mashehe wa Zanzibar ambao wameshitakiwa chini ya Sheria ya Kuzuia Ugaidi (Prevention of Terrorism Act) ambayo inatumika Tanzania Bara na Zanzibar. Sasa maadam suala hili liko mahakamani, kama alivyosema Mwanasheria Mkuu wa Serikali, sisi kazi yetu kubwa tuharakishe uchunguzi na kesi ikamilike mahakamani. Sasa uchunguzi unategemea mambo mengi ambayo pia siyo vyema kuanza kuyazungumza ndani ya Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Mwanasheria Mkuu wa Serikali kufanya hivyo tutakuwa badala ya kuisaidia kesi hii, labda tukaivuruga zaidi. Kwa hiyo, naomba tuendelee kuviachia vyombo vinavyofanya shughuli hiyo pamoja na Mahakama na wachunguzi lakini kwa kadri inavyowezekana kesi hii kama kesi nyingine zozote zile imalizwe mapema iwezekanavyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo limezungumziwa na Waheshimiwa Wabunge ni suala zima la Katiba mpya. Napenda nirudie maelezo yale yaliyotolewa. Katika jambo hili niseme kama nilivyoeleza katika maelezo yangu kwenye Kamati nilipoulizwa, Serikali inatambua umuhimu wa Katiba mpya, lakini Katiba siyo kitabu hiki tu. Ziko nchi hazina katiba iliyoandikwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Waingereza hawana Katiba iliyoandikwa. Ukiwauliza Waingereza leo Katiba yao ni nini? Ni mila na desturi. Israel haina Katiba iliyoandikwa; na kwa kuwakumbusha, Zanzibar toka mwaka 1964 baada ya Mapinduzi mpaka mwaka 1979 haikuwa na Katiba iliyoandikwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, mimi na Mheshimiwa Dkt. Harrison George Mwakyembe tutamkumbuka Mwalimu wetu wa Katiba, Profesa Srivatava aliyetuambia Katiba siyo hicho kitabu, ni ujumla wa maisha yenu yote, matamanio yenu, matarajio yenu na shida zenu. Hii ambapo Waingereza wenyewe hawakuwa na Katiba ya kuandika na mpaka leo hawataki, walituandikia sisi na sijui niliseme maana yake nimekuwa Waziri, wakiamini kwamba ninyi hamna uwezo wa kuwa na mila na desturi zinazostahili kuwa Katiba. Kwa hiyo, wawaandikie. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana Katiba yetu ya uhuru ya mwaka 1961, actually it was a schedule to an Act of Parliament which was passed by the House of Commons. The Tanganyika Order in council and accented by the Queen, not in Buckingham Palace, in St. George Chapel, Windsor . (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, maana yake kama alivyosema dada, Mheshimiwa Riziki Shahari Mngwali, Tume ya Mabadiliko ya Katiba ilitoa siyo Rasimu tu; tuliangalia Rasimu tu na nimekutaja kwa kazi kubwa uliyofanya. Tulitoa Juzuu hii, maoni ya wananchi kuhusu sera, sheria na utekelezaji, iwe sehemu ya hiyo Katiba inayoishi. Ndani ya mambo hayo, niwasomee moja tu ambalo wananchi walituambia, ni safari za viongozi, ukurasa wa 38 kwamba safari za viongozi ziwe na kikomo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa huyu anasafiri sana? Wakasema, malengo ya safari za nje za viongozi yawe wazi kwa wananchi. Niwaambie jambo moja walilolisema, na mimi ningetamani
liwe, matumizi ya neno mheshimiwa, mapendekezo ya wananchi. Mapendekezo ya wananchi kuhusu matumizi ya neno mheshimiwa yalikuwa kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, neno mheshimiwa lisitumike kwa Wabunge na viongozi wengine wa umma, badala yake neno ndugu litumike ili kuondoa matabaka na kuwakweza viongozi juu ya wananchi ambao kimsingi ndio waliowaweka madarakani. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sehemu kubwa kama alivyosema Mheshimiwa Shahari Mngwali…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKTI: Mheshimiwa Waziri, malizia tu.
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kama alivyosema Mheshimiwa Shahari Mngwali, kitu kikubwa kilichozungumzwa na wananchi humu, ni maadili ya viongozi. Moja, wananchi walipendekeza viongozi wote wakiapishwa, waape maadili ya viongozi. Tunaapa au hatuapi?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, mimi, mimi, mimi…
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi kitabu hiki nitakikisha tunakipa uzito unaostahili kwa sababu ndiyo maoni ya wananchi ya Katiba inayoishi. Kwa hiyo, tayari matashi ya wananchi yameanza kutekelezwa. Ndiyo maana kwa sasa kama nilivyosema kwenye Kamati, kazi tunayoifanya ni kazi ya kuzichambua sheria, ndiyo maana haina kasma. Si ni kazi za siku zote, ndiyo maana haikutengewa fedha, kwa sababu ni kazi tunayoifanya ndani ya Serikali. Ni kazi ya kila siku, tunaangalia sheria zote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, siyo hivyo tu, nawaambia mambo makubwa kama haya hayataki shinikizo. Mambo makubwa kama haya yanataka umuombe Mwenyezi Mungu akufanye uwe mwerevu kama nyoka na mpole kama hua ili ufikie unapotaka Taifa likiwa moja. (Makofi)
(Hapa kengele ya pili ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
WAZIRI WA KATIBA NA SHERIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, wananchi na Wabunge wametoa maoni mengi na ninataka niwahakikishie kwamba maoni yote tumeyapokea na kwa utaratibu uliopangwa na Bunge, tutahakikisha kila aliyetoa hoja yake, jibu lake linapatikana kwa utaratibu uliopo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutoa hoja.