Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria

Hon. Mohamed Omary Mchengerwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Rufiji

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Katiba na Sheria

MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya wana Rufiji wote duniani, nasimama hapa nami kuwasilisha ya kwangu lakini kwa kuzingatia maelekezo yaliyowahi kutolewa katika kitabu chake Paul Flynn, mmoja wa Wabunge wazoefu nchini Uingereza kinachozungumzia how to be an MP. Pia Profesa Phillip Collin naye katika kitabu chake aliwahi kuzungumzia mambo ya msingi kabisa ambayo Mbunge anapaswa kuyafanya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nianze kumshauri dada yangu Mheshimiwa Sabreena atambue kwamba BAKWATA sasa ina uongozi ulio imara na wachapakazi sana. (Makofi).
Shekhe Mkuu wa sasa, Shekhe Zuberi ni mchapakazi sana na mambo haya ya dini tusiyalete kwenye Bunge hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu mmoja anaitwa K. Sachiarith mmoja kati ya wa washindi wa Global Award, katika Mkutano wa 136 wa Bunge wa Dunia uliofanyika kule Bangladesh, aliwahi kuzungumza maneno ambayo napenda niyazungumze katika Bunge lako hili Tukufu. Ndugu Sachiarith aliwahi kusema kwamba kama akinamama wangewezeshwa miaka 50 iliyopita basi dunia tungekuwa na Taifa jema sana (if women were empowered in the last fifty years we could have a better world).
Mheshimiwa Mwenyekiti, aliendelea kwa kusisitiza kwamba iwapo vijana wangezaliwa na akinamama waliowezeshwa miaka 50 iliyopita basi tungekuwa na vijana wazalendo wa Taifa, waadilifu na tungekuwa na Taifa lenye nguvu sana, Tanzania ingekuwa ni Taifa lenye nguvu sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona niseme maneno haya kwa sababu tunaona kabisa kwamba vijana waadilifu utawakuta upande huu tuliokaa wengi. Hapa nataka nimtofautishe ndugu yangu Bwana Tundu Lissu ni miongoni mwa ignorant pan-politician. Nimeona niseme hivi kwa sababu Tundu Lissu hana uzalendo wa Taifa hili, anaendekeza harakati, yeye ni mwanaharakati lakini si mwanasiasa. Kwa hiyo, tunawaomba Watanzania kumuepuka na kuepukana naye kwani dhamira yake ni kuligawa Taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jukumu la Bunge kwa mujibu wa Ibara ya 63 na 64 ni kutunga sheria na kuisimamia Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasheria wote duniani wanatambua kwamba nchi hii inaendeshwa na Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.
Taarifa......
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii naikataa kwa sababu Shekhe Zuberi ni Shekhe ambaye anatambua elimu ya dunia pamoja na ya akhera. Ni mtu muadilifu na mchapakazi sana na ameweza kui-transform BAKWATA kuwa ni chombo kizuri sana kwa Waislam. Niwaombe Waislam wote kuendelea kuiamini BAKWATA. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, wanasheria wote duniani wanatambua kwamba nchi inaongozwa na katiba, sheria, kanuni na taratibu. Vilevile inaongozwa na taratibu za Chama Tawala ambacho ndicho kimeiweka Serikali madarakani. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimeona niseme hili kwa sababu upo upotoshaji mkubwa uliozungumzwa na Tundu Lindu kuhusu Rais kwamba haitaki Katiba Mpya. Naomba nikumbushe Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015 ambayo katika ukurasa wake wa nne (4) inazungumzia mambo yatakayotekelezwa na Serikali ya Chama cha Mapinduzi. Katika Sura ya Saba ya Ilani ya Uchaguzi wa Chama cha Mapinduzi pamoja na maneno mengine ukurasa 163 katika aya ya 144 inazungumzia mambo yafuatayo ambayo naomba niyanukuu hapa.
“Mchakato wa kutunga Katiba Mpya umeendeshwa na umefikia hatua ya Katiba Inayopendekezwa iliyopitishwa na Bunge Maalum la Katiba ambayo itapigiwa kura ya maoni”.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hii ni Ilani ya Chama cha Mapinduzi ambayo nchi hii inaongozwa kwa mujibu wa taratibu kama ambavyo nimezisema.
T A A R I F A...
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii naikataa kutoka kwa layman huyu na naomba nimsaidie kwamba nchi inaongozwa na katiba, sheria na kanuni na taratibu ambazo Chama Tawala ndicho kilichosimamisha dola madarakani. Chama cha Mapinduzi kilikuwa na Ilani ya Uchaguzi ambayo wananchi walio wengi waliiona na kuisoma wenzetu walikuwa na tovuti ambayo ilikuwa ni vigumu kwa wananchi wa vijijini kuiona na kuisoma na kuikubali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 118 ya Katiba ambayo Tundu Lissu amepotosha hapa jamii kwa kusema kwamba Mheshimiwa Rais amevunja Katiba kwa kutomchagua Jaji Mkuu wa Tanzania. Ibara ya 118 haimlazimisha Rais kuchagua Jaji Mkuu wa Tanzania. Ibara ya 118 iko wazi kabisa. Mheshimiwa Tundu Lissu anaifahamu sheria na anaijua Ibara hii imezungumza vizuri lakini anachofanya ni kupotosha Watanzania na kuleta taharuki katika nchi yetu hii ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yamezungumzwa masuala mengi kuhusu demokrasia na utawala bora. Chama cha Mapinduzi kinaongozwa na Ilani na ukurasa wa 146 umezungumzia demokrasia na utawala bora. Nataka niseme hapa kwamba chama hiki kina demokrasia ya kutosha na unapomwona nyani anamtukana mwenzie ni vyema akajiangalia nyumani kwake. Chama hiki kimekuwa na Wenyeviti kadhaa kila baada ya miaka kumi wenzetu wamekuwa na Mwenyekiti amekaa madarakani zaidi ya miaka 20. Hauwezi kuzungumzia demokrasi wakati nyumbani kwako kunaungua. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi hii mwaka 1961 ilikuwa na Rais wa kwanza alikuwa Mzanaki, Mheshimiwa Mwalimu Julius Kambarage Nyerere. Baada ya Mwalimu Nyerere wananchi walimchagua Rais wa Awamu ya Pili, Mzee wetu Mheshimiwa Ally Hassan Mwinyi, alikuwa Mzaramo wa kutoka Zanzibar.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1995 baada ya kupitishwa mfumo wa vyama vingi 1992 tulimchagua Mheshimiwa Benjamin Mkapa, huyu alikuwa Mmakonde kutoka kule Kusini. Mwaka 2005 tulimchagua Mheshimiwa Dokta Jakaya Mrisho Kikwete huyu alikuwa Mkwere kutoka pale Pwani. Taifa letu leo hii tunashuhudia kuwa na Rais Msukuma kutoka Kanda ya Ziwa. Hii ni demokrasia ya hali ya juu ambayo wenzetu hawana.
MHE. MOHAMED O. MCHENGERWA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ni vyema nyani akawa anaona kundule kuliko kutukana wenzio wakati wewe mwenye una matatizo.Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa naomba nijielekeze katika kuishauri Serikali yangu njema ya Chama cha Mapinduzi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nianzie hapo kwenye uzalendo, miaka ya 90 Mwalimu Nyerere aliwahi kumthibitisha Kawawa katika moja ya mikutano yake pale Mnazi mmoja kusema kwamba Kawawa ni muadilifu sana na alikuwa tayari kutoa machozi kuthibitisha kwamba Kawawa alikuwa ni muadilifu. Nami ndani ya Bunge lako Tukufu naomba kuthibitisha kwamba iwapo siku moja Wabunge walio wengi wakasema kwamba mambo mazuri anayofanya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Joseph Magufuli kwa nchi hii si uzalendo, basi nitaliomba Bunge lako hili Tukufu kufuta hili neno uzalendo katika dictionary ya Kiswahili. Kwa sababu mambo makubwa anayoyafanya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli ni uzalendo wa hali ya juu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwa maneno mawili matatu ambayo nimeyaacha pembeni. Mheshimiwa Waziri nikuombe sana wakati unahitimisha hoja yako hapa...
Nikukumbushe jambo moja, kwanza, tuiangalie kada ya Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo ambao wamekuwa wakipata mishahara midogo. Zipo taarifa wako Mahakimu zaidi ya 118 ambao hawajapandishwa vyeo na hao ni Mahakimu wa Mahakama za Mwanzo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pili, kwa hali ya uchumi tuliyonayo ni vyema tukawaangalia Mahakimu pamoja na Wanasheria wa Serikali ili kuwawezesha fedha kidogo kwa ajili …
(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila mpangilio)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa napenda niseme kwamba Taifa hili linategemea Bunge na uzalendo wetu ndio utakaoliweka Bunge hili katika…
(Hapa baadhi ya Wabunge waliongea bila mpangilio)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niunge mkono hoja na nampongeza Mheshimiwa Waziri kwa kila jambo alilolifanya katika Bunge hili.
MWENYEKITI: Ahsante sana.