Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi hii kutoa mchango wangu katika Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Muungano wetu ni muhimu sana na fahari ya kujivunia kwa nchi yetu sababu una manufaa kwa pande zote mbili za Muungano wetu na Watanzania walio wengi hatujui nchi nyingine zaidi ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya utangulizi huo, naomba kutoa mchango wangu kama ushauri kwa Serikali yangu ya Chama cha Mapinduzi kama ifuatavyo:-
Utunzaji wa mazingira ni muhimu sana hasa mustakabali wa nchi yetu kwa kizazi cha sasa na cha baadaye ukizingatia na mabadiliko ya tabianchi na uharibifu unaotokana na shughuli za binadamu katika vyanzo vya maji, misitu na mbuga zetu za wanyama ambazo ni urithi wetu na zawadi toka kwa Mwenyezi Mungu kama zawadi kwa Watanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na umuhimu wa hilo la utunzaji wa mazingira na kutokana na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi, kuna umuhimu mkubwa wa kuwa na mikakati ya kuvuna na kuhifadhi maji kwa ajili ya matumizi ya binadamu, mifugo na kwa matumizi ya kilimo cha umwagiliaji ili kukabiliana na kuondokana na kilimo cha kubahatisha na kutegemea mvua ambazo kwa sasa hazina uhakika kutokana na ukame unaosababishwa na mabadiliko ya tabianchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kutoa ushauri kwa Serikali kuwa; tuwekeze katika kujenga mabwawa zaidi ili kuvuna na kuhifadhi maji kwa ajili ya kutunza mazingira na kulinda vyanzo vya maji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja ya mabwawa hayo ni bwawa la Kidunda ambalo andiko lake la kwanza lilikuwa mwaka 1955 kabla ya uhuru na la pili ni mwaka 1962 na la tatu ni mwaka 1994 ambalo lilibadilisha wazo la awali la matumizi ya bwawa kwa uzalishaji wa umeme, ufugaji wa samaki, kilimo cha umwagiliaji pamoja na uzalishaji wa maji safi na salama kwa Mikoa ya Morogoro, Pwani na Dar es Salaam.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kushauri Serikali kurudi kwenye mipango ya awali ya Mwalimu Nyerere ya kujenga bwawa kwa ajili ya matumizi yote kwa ajili ya kukabiliana na uzalishaji wenye tija katika kilimo na kuwa na uhakika wa chakula na malighafi ya kiwanda ukizingatia kuna shamba kubwa la miwa na kiwanda cha sukari kinachojengwa kule Mkulazi ambao nao watahitaji maji kutoka katika bwawa hilo. Katika hili tutapata changamoto lakini tutangulize maslahi mapana ya Tanzania kwanza.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.