Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. Martin Alexander Mtonda Msuha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kuchukua nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango, kwa maandalizi mazuri ya Mpango wa Pili wa Maendeleo ya Taifa letu, kwa kipindi tajwa hapo juu. Mpango huu ni muhimu sana kwani ndiyo dira ya mwelekeo wa Taifa kwa miaka mitano ijayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya utangulizi huu, naomba sasa nichukue nafasi hii kuchangia kisekta kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Kilimo; naipongeza Serikali kwa juhudi ambazo imezifanya hadi saa katika kuboresha kilimo nchini. Hata hivyo, katika Mpango huu wa Maendeleo siajona mkakati wa kuendelea kuyaboresha mazao makuu ya biashara kwa maana ya zao la kahawa, tumbaku, korosho na pamba.
Mheshimiwa Naibu Spika, wakulima wa kahawa hususani wanazo kero nyingi sana ambazo zinawakatisha tamaa katika kuliendeleza zao hilo. Kero hizo ni pamoja na:-
(i) Bei kubwa ya pembejeo na utaratibu usiofaa wa kugawa mbolea kwa mtindo wa vocha ambazo zinakwenda kwa package ya mbegu, mbolea ya kupandia na kukuzia. Mkulima wa kawaha hahitaji mbegu wala mbolea ya kupandia. Vocha zinazotolewa hazitoshelezi badala yake imekuwa ni lawama kwa Serikali.
Mheshimiwa Naibu Spika, maoni yangu ni kuwa, Serikali ifuate mfumo wa kupeleka mbolea kwa mtindo wa vocha na itengeneze mfumo mwingine na kwamba mbolea hizo zipelekwe mapema kabla ya msimu.
(ii) Mfumo wa soko la kahawa hususani Mbinga ni mbovu sana. Walanguzi wa soko huria hudiriki hata kununua kahawa kwa wakulima ikiwa shambani kabla haijakomaa na kuvunwa. Wanaingia mikataba ya kuwaumiza sana wakulima. Endapo mavuno ya msimu huo hayatoshi kulipa deni basi walanguzi hao hunyang‟anya mashamba ya wakulima.
(iii) Kutokana na kuwa na soko huria wakulima wamekuwa wakilipwa bei tofauti tofauti ndani ya wilaya moja. Hii inakatisha tamaa sana kiasi kwamba wakulima wameanza kususia utunzaji wa mashamba hayo ya kahawa na ndiyo maana zao hilo limeporomoka kwenye orodha ya mazao makuu ya biashara nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maoni yangu ni kuwa Serikali ichukue hatua za makusudi kupiga marufuku ununuzi wa kahawa mbichi ikiwa shambani. Mfumo huu kule Mbinga unajulikana kama “MAGOMA”. Lakini pia serikali ichukue hatua za makusudi kuimarisha Chama Kikuu cha Ushirika cha Mbinga kiitwacho MBIFACU na kuhakikisha mali ya chama kikuu cha zamani zinarejeshwa kwa chama hiki kipya.
Mheshimiwa Naibu Spika, Sekta ya Elimu; wananchi wa Wilaya ya Mbinga kwa ujumla wake wanaipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa Sera ya Elimu Bure. Hata hivyo, kuna changamoto zifuatazo ambazo zinahitaji utatuzi wa haraka sana:-
(i) Utatuzi wa uhaba wa Walimu. Zipo shule zenye wanafunzi zaidi ya 300 darasa la I hadi IV na kuna Mwalimu mmoja tu.
(ii) Vyumba vya madarasa havitoshi kabisa. Zipo shule ambazo wanafuzi wanasoma zaidi ya darasa moja kwa chumba kimoja cha darasa kwa wakati mmoja kwa kugeuziana migongo.
(iii) Suala la vyoo vya kisasa ni tatizo kubwa sana katika shule zetu za msingi.
(iv) Nyumba za Walimu nazo ziangaliwe. Watumishi hao wanaishi katika mazingira magumu sana tena sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, Nishati na Madini. Tunashukuru Serikali kwa kutekeleza Mradi wa Umeme Vijijini kupitia mpango wake wa REA. Hata hivyo, bado kuna vijiji vingi sana katika Wilaya ya Mbinga havikupata umeme kwenye REA II. Naomba Serikali sasa ipeleke umeme kwenye vijiji vilivyobaki ambavyo ni zaidi ya 150 kwenye mpango wa mwaka ujao.
Kwenye maeneo yanayotarajiwa kuzalisha umeme sijaona machimbo ya makaa ya mawe katika Kijiji cha Ntunduwalo, Kata ya Ruanda, Wilayani Mbinga yakitajwa kwenye mipango yote miwili wa mwaka mmoja wala ya miaka mitano. Eneo hili yupo mwekezaji anayechimba makaa ya mawe, naiomba Serikali imwangalie mwekezaji huyu na machimbo haya kwa namna ya pekee ili wananchi weweze kunufaika na uwekezaji wake. Kwa ujumla mwekezaji huyu na machimbo haya kwa namna ya pekee ili wananchi waweze kunufaika na uwekezaji wake. Kwa ujumla mwekezaji huyu hana mwelekeo wa kuzalisha umeme hivi karibuni. Mgodi huu uangalie upya kwani pia umekuwa kero kwa wananchi wa kata hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, maoni ya ujumla; kwa kuwa kwa miaka kadhaa ya nyuma Serikali haikuwa na uwezo wa kutoa fedha za kutosha kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya maendeleo, wakati sasa umefika, ningeishauri Serikali iangalie upya namna ya upangaji wa vipaumbele vya Kitaifa.
Vipaumbele hivyo vingepangwa kisekta badala ya kimiradi kama inavyofanyika kwa sasa. Mfano, miaka mitatu ya kwanza fedha zote za maendeleo zingepelekwa Elimu; miaka mitatu inayofuata fedha zote za maendeleo zipelekwe kwenye Afya na kadhalika. Uwekezaji katika miradi ungeweza kuonekana kwa macho na kwa tija.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuwasilisha na naunga mkono hoja.