Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

Hon. Shamsi Vuai Nahodha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano na Mazingira

MHE. SHAMSI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa
Mwenyekiti, kwanza napenda kuchukua nafasi hii kukushukuru sana kwa kunipa fursa hii ya kuchangia hotuba ya bajeti ya Ofisi ya Makamu wa Rais, Muungano.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo nimefarijika sana kutokana na mambo mawili. Kwanza, mwaka 2008 nilipokuwa Kiongozi wa Shughuli za Serikali katika Baraza la Wawakilishi, Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, lilipitisha Azimio la mapendekezo ya kuondolewa suala la mafuta na gesi katika orodha ya Muungano. Azimio hili, liliungwa mkono na Wajumbe wote wa Baraza la Wawakilishi. Wawakilishi, kutoka Chama cha Mapinduzi waliunga mkono na wawakilishi kutoka Chama cha CUF waliunga mkono Azimio hili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Uchaguzi Mkuu uliopita wa Oktoba, 2015, suala la mafuta na gesi lilikuwa ni ajenda muhimu sana katika uchaguzi huo. Chama cha CUF kililitumia suala hilo katika kuombea kura na Chama cha Mapinduzi kikafanya hivyo kule Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa miaka mingi Wazanzibari tumekuwa tukiiomba Serikali ya Muungano itafute njia ya uchumi itakayoisaidia Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar kupata fedha za kutosha kwa ajili ya kushughulikia masuala ya kupunguza umaskini na kuwaletea maendeleo wananchi wa Zanzibar. Kutokana na umuhimu wa sekta hii, kwa uchumi na maendeleo ya Zanzibar, Serikali ya Muungano sasa imeridhia suala la mafuta na gesi kuondolewa katika orodha ya mambo ya Muungano. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ya Muungano imefanya busara ya hali ya juu sana, naipongeza sana. Jambo hili lina maslahi makubwa sana kwa Zanzibar na kwa Muungano, lakini inanisikitisha sana wapo miongoni mwetu ambao tumekuwa tukipigania jambo hili litolewe kwenye orodha ya Muungano ili Zanzibar iweze kutafuta mafuta na gesi kwa maslahi ya Zanzibar, sasa hivi tunaanza kuwa na kiguu cha nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaanza nasikia baadhi yetu wanasema oooh, suala hili limefanywa kinyume na misingi ya Katiba na hao tunaosema haya ni kule upande wa Zanzibar ambao tungepaswa jambo hili tuliunge mkono. Naiomba sana Serikali ya Muungano wa Tanzania tusivunjwe moyo na jambo hili, tuendelee mbele jambo hili lina maslahi makubwa sana kwa uchumi wa Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, nilipokuwa nikichangia bajeti ya Wizara hii hii mwaka jana, nilisema kuna haja ya uchumi mkubwa kusaidia uchumi mdogo. Mwaka huu, napenda niseme nimefarijika sana kwa kumsikia Waziri Mheshimiwa Makamba akitupa taarifa hapa kwamba kuna mradi maalum unaosimamia uvuvi wa ukanda wa Pwani ya Magharibi ya bahari ya Hindi. Mradi huu bila shaka una umuhimu mkubwa sana kwa uchumi wa Zanzibar. Kama tunavyojua Zanzibar inategemea sana uvuvi na kwa maana hiyo ikiwa asilimia 50 ya wananchi wa Zanzibar wanategemea uvuvi, bila shaka mradi huu utatoa mchango mkubwa sana. Tumeambiwa hapa kiasi cha milioni mia nne sabini na sita, zimepelekwa Zanzibar ili kusaidia wavuvi wadogowadogo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, namwomba Mheshimiwa Waziri kwa kupitia mradi huu, mradi wa usimamizi wa Ukanda wa Kusini Magharibi mwa Bara Hindi, ni vizuri ukaanzisha mradi maalum au mfuko maalum wa kusaidia wavuvi wadogowadogo. Nalisema hili kwa sababu fedha ambazo hivi sasa zinatolewa si haba, lakini si nyingi sana, kwa maana hiyo naomba Wizara hii, ama mradi huu unaweza kuwekwa chini ya mradi wa Mamlaka ya Uvuvi wa Bahari Kuu, ama unaweza kuwekwa chini ya usimamizi wa mradi huu nilioueleza. Mheshimiwa Waziri uamuzi ni wenu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hoja ninayoieleza hapa ni kwamba, kuna haja ya kupata fedha za kutosha kwa ajili ya kuwasaidia wavuvi wadogowadogo pia kwa ajili ya kuimarisha mazingira ya baharini. Kama unavyojua, kipindi kilichopita kiasi cha miaka miwili, mitatu hivi iliyopita, tulikuwa na mradi wa kuwasaidia wavuvi wadogowadogo pamoja na …
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MHE. SHAMSHI VUAI NAHODHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutamka rasmi kwamba naunga mkono hoja.