Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. George Boniface Simbachawene

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibakwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijalia afya na kusimama mbele kwa kazi ya kujumuisha mjadala wa bajeti ya mwaka 2017/2018 juu ya bajeti ya mapato na matumizi ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuwashukuru Waheshimiwa Wabunge wote kwa ujumla wa pande zote mbili kwa michango yenu mizuri na muhimu ambayo ililenga kuboresha utendaji kazi wa Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge wa pande zote mbili wametoa michango yao; walioweza kuchangia kwa maandishi ni 47 na waliochangia kwa kuongea ni 34. Michango yao yote tumeizingatia na tumeijibu hoja kwa hoja katika jedwali hili la majibu ya hoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kwa kuwa michango ni mingi na waliozungumza ni wengi, pengine haitakuwa rahisi kuweza kutumia muda huu wa kuzungumza kumjibu kila mmoja alichokisema, lakini muamini tu kwamba kila mmoja alichokisema tumekizingatia na tutakizingatia wakati wa kutekeleza bajeti itakayopitishwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, rai yangu kwenu ni kwamba mtusaidie tuweze kupata fedha hizi tulizoziomba ili tuweze kutekeleza majukumu kama tulivyoainisha katika malengo ya Wizara, Ofisi ya Rais, TAMISEMI.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla ya kuanza kujibu hoja za Wabunge, nataka niseme maneno. Michango mingi imetolewa na Wabunge, pamoja na uzuri wa michango hiyo, iko baadhi ya michango ilileta hali ya kutokuelewana. Kutokuelewana huko kumetokana na lugha na pengine matamshi yanayotamkwa ambayo kimsingi, hata kama katika utaratibu unaambiwa tunakuja huku Bungeni kupewa ushauri kama Serikali, lakini unaona huo utayari wa kupewa ushauri haupo kwa sababu anayetoa ushauri tayari ana hukumu na kutumia lugha ambayo haiko sawa sawa kimaadili, lakini pia hata katika kanuni zetu za uendeshaji wa shughuli za Bunge. Ndiyo maana katika mjadala kulitokea kusimama kwingi na vurugu nyingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme tu, ukitaka kujua historia ya nchi yoyote lazima uangalie vipindi vyake vya utawala. Nchi hii toka tulivyopata uhuru Rais wetu wa kwanza alikuwa Mheshimiwa Julius Kambarage Nyerere ambaye naye katika wakati wake, hasa alipoamua kujenga Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea alipata shida kubwa. Walitokea wapinzani, walitokea waasi na mtakumbuka akina Oscar Kambona, akina Kasanga Tumbo; na mnakumbuka katika historia nini kilitokea kwa baadhi ya watu waliokuwa wapinzani wa misingi ya Ujamaa na Kujitegemea ambao leo hii hapa tunajivunia kwamba imeliweka Taifa hili salama. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipindi cha pili amekuja Mzee Mwinyi. Rais Mwinyi katika kipindi chake akafungua milango ya uchumi akaleta uchumi huria; na kwa maneno yake alisema unapofungua milango na madirisha basi nzi wataingia, matakataka yataingia, wadudu wataingia, hewa chafu itaingia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufungua milango ya uchumi akaonekana yeye ni mtu asiye na weledi wa uchumi, ni mtu ambaye amefungua kila kitu, mambo yanaenda holela, wakapatikana wa kulaumu na wakalaumu sana. Hata hivyo, kipindi hicho kikapita na leo hii tunakumbuka Awamu hizo zote mbili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amekuja Mkapa akaleta discipline ndani ya Serikali, akaboresha utumishi ndani ya Serikali, akaboresha heshima ya Serikali. Kwa kufanya hayo naye akaambiwa huyu ni Mkapa ameleta ugumu wa maisha na akalaumiwa sana. Kipindi hicho kikapita na chenyewe tunakikumbuka na tunakipongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, amekuja Kikwete ambaye amemaliza Awamu ya Nne, Rais mpole, mjuzi wa Diplomasia ameijenga nchi yetu kujulikana sana Kimataifa, amejenga uchumi na miundombinu, amefanya mambo makubwa akaambiwa ni Rais dhaifu, tena ni mpole aliyepitiliza hafai kuwa Rais; hapa hapa humu ndani na bahati nzuri waliosema wamo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo anapongezwa sana kwamba ni Rais mzuri hajapata kutokea, amefanya mambo makubwa, anakumbukwa kwa mema na makubwa aliyoyafanya na anakumbukwa na watu wa pande zote mbili na ushahidi ni namna alivyoshangiliwa juzi alipokuja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa stadi hii na mifano hii, leo hii kuweka mipango na mikakati ya baadhi ya wenzetu humu ndani ya kumdhalilisha na kumtukana Mheshimiwa Rais si jambo la kwanza; kumbe inawezekana akimaliza atapongezwa na kusifiwa. Kwa hiyo, ninachotaka kumwambia Mheshimiwa Rais wangu, haya yanayosemwa ni utaratibu wa kawaida wa miongo yote ya utawala wa nchi yetu, yeye aendelee, tunasonga mbele na sasa nchi inakwenda mbele katika uchumi wa viwanda. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi majuzi IMF na World Bank wiki iliyopita imezindua taarifa ya hali ya uchumi ya Tanzania na imepongeza uchumi wa Tanzania kwamba ni miongoni mwa nchi tano ambazo uchumi wake unakua kwa kasi na uko stable. Uchumi wa Tanzania kwa sasa uko very stable, unakua kwa asilimia saba nukta moja. Kwa Afrika inazidiwa na Côte d’Ivoire ambayo uchumi wake unakua kwa asilimia
saba nukta tisa. Kwa ukanda huu wa East Afrika hakuna nchi inayotukuta, sisi katika Afrika ni wa pili, katika sifa kama hii bado watu wanasema hawaoni kitu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini leo hii Rais huyu anazindua ujenzi wa reli ya treni ya standard gauge inayotaka kutupeleka sasa kwenye miundombinu ya usafirishaji pamoja na barabara zinazojengwa zilizounganisha mikoa yote na za lami sasa watu wanasafiri. Zamani ukisema unatoka hapa kwenda Moshi ni hadithi, leo hii kaka yangu Selasini akiwasha gari saa hizi, saa tatu yuko Moshi anakula nyumbani kwake chakula; haya ni maendeleo makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini Rais huyu ambaye sasa anajenga nchi na uchumi mkubwa unajengeka na unatupeleka kwenye viwanda, viwanda vingi vinafunguliwa bado wanasema hawaoni anachokifanya. Rais huyu anayesisitiza uwajibikaji, anaondoa rushwa, amesababisha Watanzania wanapata huduma nzuri wanapokelewa vizuri maana huko nyuma ilielezwa kwamba watumishi wa umma ni miungu watu, leo hii watumishi wa umma wamegeuka wanawahudumia Watanzania, wamegeuka wanawapokea vizuri. Ukienda hospitali unapokelewa na nesi vizuri unahudumiwa vizuri, wanasema Watanzania wamekuwa waoga, Watanzania ambao wamekuwa waadilifu na wanaona mambo yanavyokwenda vizuri, wanaambiwa wamekuwa waoga.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwahakikishie watumishi wa umma wa nchi hii kwamba, Serikali ya Awamu ya Tano chini ya Dkt. John Pombe Joseph Magufuli inafanya kazi nzuri na muiunge mkono; na sisi tunatambua changamoto mlizonazo watumishi wa nchi hii; kwa kuhakikisha kwamba mnafanya wajibu wenu bila kushinikizwa. Naamini kabisa matunda haya yanayopatikana yataivusha nchi yetu kutoka mahali ilipo na kufika mahali pazuri zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zimezungumzwa hoja nyingi lakini nianze na moja ambayo inakera hivi. Huwezi ukasema kitu bila kuwa na takwimu na bahati mbaya sana takwimu tunazileta sana humu. Kibaya zaidi ni kwamba kumbe mtu akiamua kukupinga hawezi kukubali hata takwimu utakazomletea hawezi kukubali chochote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeambiwa elimu ya Tanzania inashuka, lakini kinachoweza kutusaidia kujua kwamba elimu inashuka au inapanda ni matokeo ya wanafunzi wanaofanya mtihani. Kama kipo kigezo kingine labda ni baadaye lakini cha kwanza ni matokeo. Sasa nifanye ulinganisho, katika sekta ya elimu matokeo ya darasa la nne mwaka 2014, ufaulu ulikuwa ni kwa asilimia 64, leo 2016 matokeo ni kwa asilimia 93, watoto wamefaulu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, darasa la saba mwaka 2012 watoto walifeli sana, ilikuwa ni asilimia 33 ya ufaulu, leo hii ni asilimia 70. Matokeo ya kidato cha pili, mwaka 2012 ilikuwa asilimia 57, leo hii ni asilimia 91. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo ya kidato cha nne mwaka 2012 ilikuwa ni asilimia 45, leo hii ni asilimia 70 ya ufaulu. Matokeo ya kidato cha sita yanatisha ni karibu wanafunzi wote wamefaulu. Mwaka 2012 ilikuwa asilimia 88 tu ndio waliofaulu, leo hii ni asilimia 99 ndio waliofaulu. Ahsanteni Walimu wa Tanzania, tunawashukuru sana Walimu wa Tanzania. Ninyi ni wazalendo wa nchi hii, Walimu wa Tanzania ni wapenda maendeleo ya elimu ya nchi hii, tekelezeni wajibu wenu na Serikali inatambua mchango wenu; na wala ninyi sio waoga. Msijazwe upepo wa kuambiwa ni waoga, sidhani kama kwa mwoga huenda kilio. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini, Serikali tunatambua na ndiyo maana tumechukua hatua. Hadi sasa tumelipa madeni ya Walimu wote nchini bilioni thelathini na tatu, madeni yasiyo na mshahara. Kwa mwaka 2015/2016 – 2016/2017, tumelipa bilioni thelathini na tatu na tumelipa kwa takribani mikoa yote na madeni ambayo yamebaki yanadaiwa ni yale tu ambayo ni ya mshahara, lakini yale yasiyo ya mshahara yote tumeyalipa na tunahakikisha kwamba na madeni ya mshahara na yenyewe tutayalipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, elimu bila malipo imebezwa humu ndani sana na katika ubezwaji huo ni ubezwaji wa kupotosha. Serikali inatumia billioni ishirini na mbili nukta tano kila mwezi. Wakati fulani ili kumwandikisha mtoto darasa la kwanza ilikuwa ni lazima mzazi atoe kati ya Sh. 30,000/= mpaka Sh, 100,000/=, Serikali imesema marufuku, itagharamia gharama hizo za uandikishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inatoa ruzuku ya uendeshaji wa shule, wazazi hawachangishwi, Serikali inatoa chakula kwa shule za bweni, lakini Serikali inagharamia mitihani, ilikuwa wazazi wanalipia mitihani sasa hivi ni bure. Ilikuwa hakuna vitabu sasa hivi tunapeleka vitabu na tumegawa vitabu zaidi ya millioni sita, ukijumulisha vyote vya kuanzia elimu ya msingi na sekondari, vitabu vingi tumegawa na sasa uwiano wa mwanafunzi wa vitabu ni kitabu kimoja wanafunzi watatu. Kwa hiyo, tunakaribia kufika kwenye lengo la milenia lakini watu wanasema hakuna kinachofanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niwasihi Watanzania kwamba elimu yetu inaboreshwa na inatazamwa kwa ukaribu sana na Serikali na tutahakikisha kwamba pale ambapo Serikali ina wajibu wa kufanya mambo tutaendelea kuyafanya zaidi. Kwa sasa tunatumia billioni karibu ishirini na tano kwa kila mwezi kwa ajili ya kuondoa zile gharama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haimaanishi kwamba kwa kusema tu elimu bure na kuchukua gharama hizi zilizokuwa zinawaumiza wazazi na kusababisha udahili wa wanafunzi kupungua; leo hii kwa mwaka tumeandikisha wanafunzi wa chekechea na darasa la kwanza zaidi ya milioni moja na laki nne wakati lengo lilikuwa laki tisa. Haya ni mafanikio makubwa ambayo wazazi sasa wanawatoa watoto wao kwa sababu hakuna gharama za lazima wanazotakiwa kuzilipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mafanikio haya makubwa yanatokana na fedha hizi ambazo Serikali inagharamia, lakini mtu anasema uwepo wa elimu bure basi Mwalimu Serikali ilipie kila kitu, ihakikishe mtoto huyu amechukuliwa kutoka nyumbani kupelekwa shuleni, mtoto huyu amepewa kila kitu jamani, hii tafsiri ni ya upotoshaji ni tafsiri isiyowatakia mema Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwasihi wazazi wa nchi hii kwamba watoto ni wa kwetu lazima tushiriki kusaidiana na Serikali kuhakikisha kwamba wanapata elimu kwa sababu mwisho wa siku haipati faida Serikali peke yake bali hata sisi wazazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie sasa Sekta ya Afya. Sekta hii ina changamoto kadhaa na zimesemwa na Waheshimiwa Wabunge. Moja ni changamoto ya upatikanaji wa dawa. Kwa mwaka wa fedha 2016/2017, hadi mwezi Machi tumepeleka kiasi cha Shilingi bilioni 79.7 za dawa. Tulipofanya ukaguzi tumekuta baadhi ya Hospitali za Wilaya zina fedha za dawa zipo kwenye akaunti hawataki hata kuzitumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hawataki kuzitumia ili zibakie baki mle baadaye wajue cha kufanya, huu ni wizi tu. Hizo fedha zimetolewa kwa ajili ya dawa, ni lazima zinunue dawa na watu wapate dawa, lakini wananchi wakienda kule wanaambiwa dawa hakuna. Niseme, Waheshimiwa Wabunge sisi ndio Madiwani, tuko kule, tufike hatua hata tukague akaunti za Halmashauri, si kosa kwa sababu Mbunge unashiriki kwenye Kamati ya Fedha na kule kwenye Kamati ya Fedha ndiko mnakohoji mpaka akaunti kwamba zina fedha au hazina pesa.

Waheshimiwa Wabunge, msije kulalamika huku, sisi tunakwenda kukagua kwenye akaunti ambazo ninyi mko kule, tunakuta kuna fedha zimebaki, unamuuliza Mganga Mkuu hizi fedha zimebaki za nini, anajiuma uma tu. Kwa hiyo, tunawasihi Waheshimiwa Wabunge na Waheshimiwa Madiwani kusimamia kuhakikisha kwamba dawa zinapatikana, Serikali inapeleka fedha nyingi sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mwaka huu wa fedha Serikali imepanga kutumia Shilingi billioni 96.433 kwa ajili ya dawa; tunahakika ni dawa nyingi, lakini bado hapo hujazungumzia CHF, hujazungumzia Mfuko wa Afya ya Jamii ambao na wenyewe unaingiza fedha nyingi sana. Mnapowauliza hizi zilizopelekwa na Serikali waulizeni hata yale makusanyo yao, ambapo katika yale makusanyo yao asilimia 33 ni kwa ajili ya motivation, inatakiwa ilipe hata on call allowances. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ziko Wilaya zinafanya hivyo na nyingine hazifanyi. Niwaombe sana Waheshimiwa Wabunge na Waheshimiwa Madiwani tusimamie sana kuhakikisha kwamba rasilimali hizi zinatumika katika kuwahudumia wananchi wetu lakini tukibaki tunabishana na kuona ni sifa kusema hakuna dawa, Serikali hii imeshindwa, imefanya nini, tunapoteza maisha ya watu wetu bure kwa uzembe wa watu wachache ambao si waaminifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utaratibu wa upelekaji wa dawa sasa tunauboresha, tunataka sasa pesa hizi sasa zipelekwe mpaka kule kwenye vituo vya kutolea huduma kwenye zahanati, kwenye vituo vya afya, kwenye hospitali za wilaya na kwenye hospitali za mikoa. Hela zipelekwe kule, na tumeweka utaratibu ambao sasa kutakuwa kuna maafisa mahususi kwenye kila kituo cha afya na zahanati zinazozunguka kituo cha afya watakaosimamia ununuaji na upangaji wa dawa kuhakikisha kwamba zinapatikana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sasa utaratibu tumeuboresha zaidi kwamba MSD watakapopelekewa ile quotation ya dawa na Halmashauri husika watakapokuwa out of stock hawana hizo dawa, lazima watoe hilo jibu mara moja ili sasa hao waende wakanunue kwenye maduka mengine kwa sababu na yenyewe hiyo haikatazwi tena sasa.

Kwa hiyo, nina hakika kwamba kama tutasimamia vizuri na Waheshimiwa Wabunge na Madiwani tutasimama vizuri nina hakika kwamba tatizo hili halitakuwepo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa watumishi. Ni kweli kwamba tuna upungufu wa wataalam wa kada mbalimbali, mahitaji ni tisini na sita elfu na ushehe hivi lakini waliopo ni arobaini na sita elfu na upungufu ni kama hamsini elfu. Changamoto hii ni kubwa, tuna shida ya ikama hiyo kwenye upande wa Walimu na kwenye upande wa Sekta ya Afya. Utaratibu wa Serikali ni kwamba tutaendelea kuboresha ikama hizi kadiri tutakavyokuwa tunapata uwezo wa uchumi kuweza kubeba ajira zinazotakiwa kuzitoa katika Sekta ya Umma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii tunavyozungumza wage bill ya nchi yetu sasa is almost seventy percent ya GDP. Unapokuwa na wage bill kubwa kiasi hicho halafu bado una upungufu wa watumishi muhimu kama wa afya na elimu lazima kuna tatizo mahali. Ama tumeajiri katika kada nyingine watu wasiohitajika kuwepo, ama tumefanya over employment katika maeneo ambayo si muhimu kwa Taifa kwa sasa. Kwa hiyo, iko haja ya kuangalia ndio maana Serikali sasa tunaangalia masuala ya miundo, nafikiri atakuja kuzungumza Waziri wa Utumishi ili tuweze kuona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachoweza kusema kwa sasa ni kwamba kwa watumishi wa afya tumepata kibali cha hawa Watumishi madaktari 258 ambao nina hakika hawa tutawapanga kwenye vituo vyetu vya kutolea huduma hospitali za wilaya na za halmashauri pamoja na vituo vya afya mara moja. Kuanzia siku ya Jumatatu hawa tutaanza kuwa-deploy na kuwapeleka huko na tunasubiri vibali zaidi vikitolewa ili tuweze kuwapeleka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye upande wa Walimu tumepata kibali cha ajira zaidi ya elfu nne na tumeweza kupeleka Walimu takribani elfu tatu na mia kadhaa hivi ambao tumewachukua wote wa masomo ya sayansi waliomaliza mwaka 2015. Hata hao tuliowachukua tumebaki na nafasi ya kibali ambapo hawajatosha. Tunaamini wengine waliokosa kwa sababu ya kukosekana kwa barua zao tumewaambia wazilete Wizara ya Elimu na zingine kama wakiweza hata TAMISEMI tutazipeleka kwa Waziri wa Elimu wazihakiki ili waweze kupata nafasi; wale waliokosa, ambao walimaliza mwaka 2015.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilizungumzwa hapa habari ya ujenzi wa miradi ya afya na elimu, unazungumzia zahanati, madarasa, matundu ya vyoo na kadhalika na kadhalika. Mwaka uliopita tulipata hela ile ya maendeleo isiyo na masharti, inajulikana kama Local Government Development Grant. Tulipata fedha ingawa haikuletwa kwa kiwango kizuri tumepokea kiasi cha bilioni hamsini na nane. Waheshimiwa Wabunge, mkumbuke kwamba fedha hii kwa miaka mitatu mfululizo ilikuwa haijawahi kutolewa na ndiyo ilipelekea maboma mengi kubakia kwenye maeneo yetu bila kumaliziwa kwa sababu fedha hii ndiyo ambayo huwa inatumika kumalizia maboma haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninayo furaha kuwajulisha kwamba katika Mwaka wa Fedha 2017/2018, kiwango hiki cha fedha kimeongezeka hadi kufikia billioni 256. Hizi shilingi billioni 256 zikisaidiana na utaratibu wetu wa kawaida wa nchi yetu ya Siasa ya Ujamaa na Kujitegemea, ambapo ni lazima wananchi washiriki katika shughuli za maendeleo yao, wakatoa nguvu zao, wakasogeza mchanga, wakasogeza mawe, wakanyanyua mabomba au hayo yaliyopo hizi fedha zina uwezo wa kutusaidia kumalizia kwa kiasi kikubwa na kwa hivyo tutaongeza zahanati, vituo vya afya, tutapunguza upungufu wa madarasa na nyumba za Walimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe rai kwa wananchi wa Tanzania kushirikiana na Mamlaka za Serikali zao za Mitaa kuhakikisha kwamba wanachangia nguvu zao ili kwa uchumi wetu ulivyo na kiwango hiki cha fedha kidogo kiweze kuwa na tija kwa kumaliza kero hii ya wananchi katika maeneo ya huduma za afya na elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ilizungumzwa issue ya mapato ya ndani. Kama maombi mengi yalivyokuwa yanatolewa na niishukuru sana Kamati kwa kupitia Mwenyekiti wetu Mheshimiwa Jasson Rweikiza, walishauri sana kwamba sasa ile fedha inayopelekwa kwa ajili ya maendeleo kuwa sera ile ya asilimia sitini na kwa arobaini, yaani sitini iende kwenye maendeleo na arobaini ibakie kwa uendeshaji ilikuwa inapelekea Halmashauri nyingine zisizokuwa na uwezo kushindwa kujiendesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imesikia na tumeibadilisha ile sera sasa tutazipanga hizi Halmashauri kutokana uwezo wake. Zile ambazo hazina uwezo zitapeleka asilimia arobaini tu kwenye maendeleo na asilimia sitini itatumika katika uendeshaji wa Halmashauri. Hapa itatusaidia sana kuhakikisha kwamba Madiwani sasa hawakopwi posho zao, lakini pia uendeshaji hata wa shughuli nyingine za kiutawala utawezekana ikiwa ni pamoja na usimamiaji wa miradi ukiondoa OC per se ambayo italetwa na Serikali Kuu, lakini pia hii own source ni sehemu ya OC. Kwa hiyo, hii nayo ikitumika vizuri, ikisimamiwa vizuri itatusaidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwenye Halmashauri zetu huwa tunaambiwa tu OC haijaja, lakini OC ni pamoja na own source, ikijumlishwa ndipo unaipata own source unapoipata OC total. Hii OC ndiyo inayoweza ikatumika hata kupunguza baadhi ya changamoto ndogo ndogo. Unamkuta Mkurugenzi anadaiwa na Mwalimu Shilingi 45,000 ya matibabu. Hivi kama una own source kwa nini usimlipe Mwalimu huyo akaondoka akaenda kufanya kazi yake? Tumeona mfano mzuri uliofanywa na Mkurugenzi wa Arusha, ndugu Kiamia. Nafikiri Wakurugenzi wote waige mfano huo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, haki za watumishi. Waheshimwa Wabunge wamezungumzia haki za watumishi. Tunalo tatizo kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa ambako Waheshimiwa Wabunge mpo, Madiwani mpo. Wapo Maafisa Utumishi ambao wanawatesa wenzao, hawataki kuwahudumia wenzao, wanataka wahudumiwe wao.

Waheshimiwa Wabunge, ninyi ndio mamlaka za utawala. Mwalimu au mtumishi anasema mke wangu yuko mahali fulani nataka kuhamia kwa mke wangu anakwambia sitaki hata kama ni ndani ya Wilaya moja, hata kama ni ndani ya mkoa mmoja. Hii haiwezekani lazima Sheria za Utumishi zizingatiwe. Walimu hawa wanayo haki ya kutoka sehemu moja kwenda nyingine lakini pia na kuishi na wenza wao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mtumishi anapoomba ahamishwe kwa sababu anamfuata mwenza wake utadhani it is a privilege, ni hiari, no, ni haki yake ya msingi. Kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge, tusimamie haki hizi za watumishi, na ninyi ndio mamlaka za utawala na nidhamu kwenye maeneo ya Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, unyanyasaji wa wananchi katika dhana ya uchumi wa viwanda, ujasiriamali na biashara ndogo ndogo. Hii habari ya kuwasumbua wamachinga, Mheshimiwa Rais alishatoa maelekezo. Wafanyabiashara ndogo ndogo hawa wakirasimishwa; alisema Mheshimiwa Mabula Mbunge wa Mwanza; wanaweza kuchangia makusanyo makubwa sana ya Halmashauri. Wanaweza kuchangia uchumi wa Taifa. Hata hivyo, wako wengine wanaona kama wafanyabiashara ndogo ndogo ni mkosi, nuksi, balaa, washughulikiwe na waondoke, hapana!

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachosema sisi ni kwamba mamlaka hizi ndizo ziwapangie maeneo mahsusi ya kufanyia shughuli zao. Maeneo mengine kwenye miji mingine ukienda wanapangwa vizuri hata wakati wa masaa fulani wanafanya ile biashara yao, ikifika kwa mfano saa moja watu wanaondoka, wanapanga biashara zao vizuri, wako kwenye maeneo mazuri na asubuhi baada ya saa nne, au saa tano wanaondolewa vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nimeambiwa na yule Mbunge rafiki yangu Raza kwamba kule Dar es Salaam wanawafukuza. Mheshimiwa Raza nitalishughulikia, hii si sawa. Hatuwezi kuwa na nchi ambayo ina watu wote wanataka kuwa na uchumi rasmi. Duniani kote, watu wasio na uchumi rasmi ndio wengi kuliko wenye uchumi rasmi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo hili tumelifahamu lakini Halmashauri zote nchini zitenge maeneo mahsusi kwa ajili ya uwekezaji wa watu hawa wadogo wadogo. Ukiwa na Wilaya yako, hata kama ni wilaya si mji, ukawapangia wale washonaji, wanaosindika mafuta, ukaandaa eneo mahsusi, ukapeleka umeme, ukapeleka maji, ukapeleka barabara ni dhahiri eneo hilo litakuwa eneo la kiutalii, hata mtu akienda kwenye wilaya hiyo ataenda kutembelea eneo hilo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge, tuko huko, rasilimali zile ni zetu. Tuwaelekeze Wakurugenzi kuhakikisha kwamba wanatenga maeneo haya na kuyapatia miundombinu ili wafanyabiashara wetu wadogo wadogo hawa tukawaweke kule kwenye maeneo mahsusi si kama wanavyokaa kwenye barabara, kwa sababu pia na wao lazima wafahamu kwamba wako wananchi wengine wenye haki pia za kutumia maeneo ambako wao wanataka kufanyia biashara ambapo pia si sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya mipaka. Migogoro iko ya aina nyingi, iko migogoro ya mipaka ya mikoa, vijiji, wilaya, iko migogoro mingi sana. Kwa ujumla tuna migogoro zaidi ya 288 inayohusiana na mipaka ya vijiji na Hifadhi za Serikali; za misitu au za Taifa za utalii. Migogoro hii ni 288, lakini tunayo migogoro mingine takriban 56 ya mipaka na tunayo migogoro mingine takriban 18 na migogoro inayohusiana na ujenzi wa Makao Makuu ya Wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge, niwasihi, sisi ndio tuko kule. Sisi katika Serikali tumeamua kujipanga na Wizara ya Ardhi, tumetengeneza task force ambayo inaipitia migogoro hii yote na tumeihakiki migogoro hii yote, tunataka ifike hatua tuje tufanye maamuzi ya
pamoja. Kwa hiyo, niwasihi sana kwa sasa tushiriki katika kuhakikisha kwamba tunatuliza migogoro hasa ya wakulima na wafugaji. Waheshimiwa Wabunge na sisi wanasiasa kwa ujumla tusiwe chachu ya kuhakikisha kwamba migogoro hiyo inakua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia limezungumzwa hapa suala la Utawala Bora, kwamba iko migongano ya mamlaka kati ya ma-DC, ma-RC, ma-DED, na Madiwani kuna migongano. Waheshimiwa Wabunge, kwanza hawa wote wanaotajwa wapo kwa mujibu wa Sheria na uwepo wake hauwi choice ya mtu mwingine, they are all supposed to be there, kwa hivyo hakuna namna ni lazima waelewane. Sasa kuelewana msingi wake mkubwa ni sheria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya na mengine, najua tutapata fursa wakati wa mafungu. Naomba niwashukuru sana Waheshimiwa Wabunge na naomba kutoa hoja.