Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Dr. Shukuru Jumanne Kawambwa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bagamoyo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. DKT. SHUKURU J. KAWAMBWA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa fursa ya kuchangia hoja ya Mawaziri Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Utumishi wa Umma na Utawala Bora.
Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote naomba nichukue fursa hii kuipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa kazi nzuri ambayo inayoifanya katika sekta mbalimbali. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Rais kwa uongozi mzuri na kuhakikisha kwamba Taifa letu linasonga mbele.
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kuchukua fursa hii kuchangia hoja katika suala la elimu. Kwanza katika Sekta ya Elimu niungane na Waheshimiwa Wabunge ambao wameipongeza Serikali kwa kutekeleza mpango wa elimu bila malipo. Huu ni uthubutu mkubwa ambao umehitaji ujasiri kuweza kuutekeleza. Ni mpango ambao umewahusisha wananchi wetu wengi. Watoto wa kiume na wa kike wa Taifa letu hili jumla yao wanazidi milioni 10; milioni kama tisa katika shule za msingi na milioni mbili katika shule za sekondari, wote wakisoma bila ya malipo. Jambo hili limewafanya wanafunzi wa tabaka mbalimbali kuweza kushiriki katika elimu, lakini ni jambo ambalo limewapa imani na uhuru wananchi wetu wasio na uwezo wa kuwapeleka watoto wao katika shule na kuwafanya watoto wao waendelee na masomo yao ya msingi na sekondari.
Mheshimiwa Naibu Spika, hili jambo ni la ukombozi, elimu ni msingi wa maendeleo ya Taifa letu. Hatuwezi kufika mwaka 2025 kama Taifa la uchumi wa kati bila wananchi wetu kuwa wameelimika.
Mheshimiwa Naibu Spika, nia hii thabiti ya Serikali na juhudi hii ya Serikali katika kuelimisha Taifa hili, tunaiona pia katika bajeti. Inatenga bajeti nzuri kwa Sekta ya Elimu ambayo inaendana na mahitaji katika shule zetu. Hata hivyo, tunajua kwamba changamoto katika shule zetu za msingi na sekondari ni kubwa mno, kwa hivyo bajeti hii ambayo tunaijadili hivi sasa tunaihitaji mno iweze kufika katika Halmashauri zetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, mchango wangu ni katika wasilisho la bajeti ndani ya Halmashauri zetu. Katika Halmashauri ya Bagamoyo hili limekuwa changamoto moja kubwa sana na ili tufanikiwe katika elimu tafsiri ya bajeti lazima itekelezwe katika utekelezaji wa bajeti yenyewe ndani ya Halmashauri. Kwa mfano Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo katika mwaka huu wa fedha 2016/2017 imetengewa pesa maalum kwa ajili ya ujenzi wa nyumba za Walimu, jumla ya Shilingi milioni 200 lakini hivi sasa tunaingia quarter ya nne bado hatujapokea .
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini pia tuna fedha za MMES kwa ajili ujenzi wa nyumba za Walimu na kwa ajili ya usambazaji wa umeme katika shule za sekondari, jumla ni Sh. 466,000,000,000. Pesa hizo hivi tunavyoongea quarter ya nne bado hela hizi hazijaingia katika Halmashauri.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile fedha za LGCD, jumla Sh. 147,000,000 kwa ajili ya ujenzi na ukarabati wa miundombinu ya shule. Fedha hizi Sh. 147,000,000 mpaka tunamaliza quarter ya tatu tumepata asilimia 49. Kwa ujumla bajeti ya miradi ya elimu kwa mwaka huu wa fedha kwa
Halmashauri ya Bagamoyo jumla ya Sh. 814,000,000 tumepokea Sh. 72,000,000 ambayo ni chini ya asilimia 10.
Mheshimiwa Naibu Spika, sasa bila Serikali kusimamia utekelezaji wa bajeti katika Halmashauri zetu kwenye sekta ya elimu hatutoweza kufanikiwa katika elimu. Tutaizungumzia elimu na tutawapa matumaini wananchi wetu lakini mwisho wa siku pesa haikutoka hakuna kitu tutaweza kumudu. Sasa hivi tuna upungufu wa vyumba vya madarasa 291 katika Halmashauri yetu, ni fedha nyingi sana, lakini kama
tungeweza kupata pesa hizi za mwaka huu wa fedha maana yake hatua kwa hatua tungeweza kuanza kupunguza shida hii ya vyumba vya madarasa na miundombinu mingine muhimu ya kuwezesha elimu bora iweze kupatikana kwa watoto wa kike na kiume wa nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali yetu tutakapoingia katika bajeti hii ya mwaka 2017/2018, ihakikishe kwamba tunapomaliza mwezi wa Sita bajeti hii utekelezaji wake uwe kwa wakati na ukamilifu kufuatana na mafungu yale ambayo tumeyapanga. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ningependa kuzungumzia kuhusu huduma ya afya. Hospitali ya Wilaya ya Bagamoyo ni hospitali ya zamani sana, tangu tumepata uhuru tulikuwa na hospitali hii. Miundombinu yake ni chakavu, tuna upungufu mwingi; tunahitaji wodi za kulala wanaume, wodi za kulala wanawake, chumba cha kujifungulia na vifaa vya tiba, tuna upungufu pia mkubwa wa dawa katika hospitali ya Bagamoyo. Hata hivyo, hospitali hii inatoa huduma kwa wananchi wengi, Halmashauri ya Wilaya nzima ya Bagamoyo inaitegemea hospitali hii. Kwa maana kila mtu anapotoka kwenye zahanati, kata mbalimbali na vijiji mbalimbali tegemeo lake ni hospitali hii.
Mheshimiwa Naibu Spika, Halmashauri yetu ya Bagamoyo haina uwezo wa kuijenga upya au kuikarabati au kuijengea miundombinu inayohitajika katika hospitali ili iweze kutoa huduma inayofanana na mahitaji ya wananchi wa Halmashauri ya Wilaya ya Bagamoyo. Naisihi Serikali, katika bajeti hii ihakikishe kwamba inatupa uwezo Halmashauri ya Bagamoyo ili tuweze kuipandisha kufikia ngazi au huduma ambao inafanana na mahitaji ya wananchi wa Wilaya hii ya Bagamoyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, changamoto ya miundombinu na upatikanaji wa madawa ipo pia katika zahanati zetu. Naishukuru Serikali kwa hatua ambazo imeweza kuzichukua katika mpango wa RBF, lakini naomba iongeze juhudi katika suala hili la afya.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kuyasema hayo, nakushukuru sana na naunga mkono hoja.