Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Pia namshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya njema na kwa kutupa nafasi tena ya uhai katika maisha haya.
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesimama kuipongeza Serikali ya Awamu ya Tano kwamba sasa imetekeleza yale yaliyoamriwa tangu mwaka 1973 ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano kuhamia Dodoma. Nimeona kwa vitendo.
Mheshimiwa Rais alisema tarehe 25 mwezi wa Saba mwaka 2016, kwamba Waziri Mkuu atahamia Dodoma na Mawaziri na Makatibu Wakuu pamoja na Watendaji wengine. Jana katika uwanja wa mashujaa, Serikali ilisema mpaka sasa waliohamia Dodoma ni watumishi zaidi ya 2,000.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, naipongeza sana Serikali ya Awamu ya Tano kwa uamuzi huo. Tatizo nililonalo ni hili; wakati Mheshimiwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu anajibu hoja za Wabunge katika Bajeti ya Waziri Mkuu alisema kwamba Muswada wa Sheria ya Serikali kuhamia Dodoma utaletwa Bungeni hivi karibuni, lakini hakusema muda. Utaletwa Bunge hili; Bunge lijalo au Muswada huo utaletwa mwaka 2020? Hakusema.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wa Dodoma wanataka time frame kwamba ni lini Muswada wa Sheria wa Serikali kuifanya Dodoma kuwa Makao Makuu utaletwa Bungeni na kujadiliwa na Bunge hili? Jambo hilo ni muhimu sana kwa sababu hata ilipoamuliwa mwaka 1973, hakuna
Sheria iliyotungwa na Bunge hili mwaka 1973 na kuifanya Dodoma kuwa Makao Makuu ya nchi. Kwa sababu hatua imechukuliwa na Serikali ya Awamu ya Tano, sasa ni muhimu kupata time frame ya Muswada kuletwa Bungeni na kujadiliwa na Bunge hili na sasa iwe sheria kwamba Makao Makuu ya Serikali ni Dodoma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeomba Mji wa Dodoma kuwa Jiji. Hatua zote tumeshafanya, tumeshapitisha kwenye Baraza la Madiwani, tumeshapitisha DCC na vikao vya RCC, lakini mpaka leo agizo hilo au ombi letu halijatekelezwa.
Naiomba Serikali, vigezo vyote tumezingatia, kanuni zote tumezipitia, Serikali ione namna sasa ya kuifanya Dodoma kuwa Jiji na hasa ukizingatia ujio wa watu wengi na vigezo vyote vimetekelezwa kama agizo la Serikali lilivyosema. Sasa tunaisubiri Serikali itupe Jiji la Dodoma.
Mheshimiwa Naibu Spika, watu wengi wanahamia Dodoma na wengi wangependa kujenga na wawekezaji wengi wangependa kujenga katika Mji huu na hata viunga vya Dodoma kwa mfano Bahi, Chamwino na maeneo mengine, lakini bado tuna changamoto ya miundombinu.
CDA ambao wamepewa kazi ya kuhakikisha kwamba wanapanga Mji, hawana fedha za kutosha kupanga mji huu.
Mheshimiwa Naibu Spika, nadhani Serikali sasa iangalie Mji wa Dodoma kwa macho ya huruma na kwa kuzingatia kwamba wengi wanahamia na wengi wangependa kujenga, lakini CDA ambao wamepewa mamlaka ya kupanga Mji, hawana fedha za kutosha. Kwa hiyo, CDA wapate fedha za kutosha, washirikiane na Manispaa ya Dodoma kupanga mji huu tusiwe na squatter kama miji mingine ilivyo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma katika Bajeti ya Waziri wa TAMISEMI, mdogo wangu Mheshimiwa Simbachawene. Nimeona jinsi alivyoonesha maabara yaliyojengwa nchi nzima na akasema kwamba katika ukurasa ule wa 27 na akaonesha kwamba mpaka sasa tumekamilisha asilimia 27% tu ya majengo ya maabara. Katika Mkoa wangu kuna maeneo mengi ambayo majengo ya maabara hayajakamilika. Naomba Serikali yangu sikivu kwamba majengo yale sasa, Serikali ione namna ya kuyakamilisha na Walimu wa Sayansi ambao wameajiriwa kwa sasa wapate kuwafundisha watoto kwa vitendo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naamini kwamba hata mikoa mingine maabara hazijakamilika kwa asilimia mia moja. Kwa hiyo, katika Wilaya na Halmashauri zetu kama hakuna vifaa vya maabara vya kutosha, hakika wanafunzi hawatajifunza kwa vitendo. Tunatamani wanafunzi
wanaosoma sayansi wajifunze kwa vitendo.
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna shida katika Wilaya yetu ya Bahi. Mimi ni Mbunge wa Mkoa, kwa hiyo, Wilaya zote za Dodoma ni zangu. Tuna shida kubwa katika Wilaya ya Bahi na Wilaya ya Bahi tunategemea kwamba hata wawekezaji na hata ofisi nyingine za Serikali zinaweza
kujengwa katika maeneo ya Bahi, lakini pale hatuna Hospitali ya Wilaya. Kituo cha Afya kilichopo kinalaza wagonjwa nane tu. Tulileta maombi maalum kwa Serikali kwamba hospitali ile tena iko njiani, Kituo cha Afya kile kipewe huduma zinazostahili, tupewe theatre ndogo. Wanawake wanaotaka kujifungua, kama wana matatizo wanaletwa Dodoma Mjini, kilometa 65. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tumeleta maombi maalum kwa Serikali yetu. Naomba sasa kwa ajili ya wananchi wa Bahi; ni miaka kumi sasa tangu Wilaya ile itengwe lakini mpaka leo hawana hospitali ya Wilaya, lakini hata Kituo cha Afya kilichopo basi kiimarishwe ili kiweze kuwahudumia
wananchi wa Wilaya ya Bahi. Afya ya Mtanzania ni muhimu, afya ya mwanamke na mtoto ni muhimu, lakini hatuna hata theatre ndogo pale. Naiomba Serikali ilifikirie sana jambo hilo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna shida pale Bahi ya maji. Tumeleta maombi maalum kwa Serikali kwamba itusaidie maji. Maji ya pale Bahi hayastahili kwa matumizi ya mwanadamu. Naomba sana Serikali ikawasaidie wananchi wa Bahi, maji ya pale yana chumvi mno na Bahi kuna madini ya uranium. Kwa hiyo, naiomba Serikali iwasaidie wananchi wa Bahi kwa kuwaangalia kwa jicho la huruma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nimesoma kitabu cha bajeti ya Waziri wa Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, ukurasa wa 39. Nimeona ajira ambazo zimetolewa kwa mwaka huu unaokwisha, ajira 9,721. Siyo mbaya, kwa sababu wamepewa Maaskari Polisi, Uhamiaji na kadhalika; lakini tuna shida kubwa ya wahudumu wa afya katika maeneo yetu. Wahudumu katika Vituo vya Afya na Zahanati zetu. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Dodoma pamoja na wafanyakazi kuhamia kwa wingi, hospitali ya Ben Mkapa inapunguza, wagonjwa wanakwenda Hospitali ya Mkoa, lakini pale kuna wahudumu 51, kati ya wahudumu 751. Kuna upungufu mkubwa sana. Nilitegemea kwamba Waziri wa
utumishi angeliangalia hili kwa macho ya huruma. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, tuna upungufu wa Watendaji wa Mitaa. Tuliambiwa kwamba kada hii tunaweza kuwaajiri, lakini tunawaajiri vipi kama hatuna bajeti? Naisihi tena, Serikali yangu sikivu iweze kuwapa mamlaka Halmashauri zetu pamoja na fedha. Kuwapa mamlaka siyo neno, lakini fedha za kuwalipa hawa Watendaji wa Mitaa na Watendaji wa Kata watazitoa wapi? Naomba hili litazamwe.
Mheshimiwa Naibu Spika, posho ya Madiwani imezungumzwa sana na Waheshimiwa Wabunge. Linatuhusu kwa sababu na sisi ni Madiwani. Madiwani ndio wasimamizi wa miradi ya maendeleo katika maeneo yetu. Posho yao ni ndogo mno. Madiwani wakumbukwe. Wao ndio wasaidizi wetu, wao ndio wanaosimamia miradi yote ya maendeleo; tukiwasahau hatuwatendei haki. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nichangie kuhusu Zahanati ya Hamai. Tuliomba fedha kwa ajili ya kituo hicho
Mheshimiwa Naibu Spika, naunga hoja mkono.