Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa na Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nami nichangie hoja hizi mbili za Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI na Utumishi. Kwanza niwapongeze sana Mawaziri hawa wawili, Makatibu Wakuu, Naibu Makatibu Wakuu na Watendaji wote wa Wizara hizi kwa kazi nzuri walizofanya katika mazingira magumu sana ya upungufu wa ufinyu wa bajeti. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, TAMISEMI ni chombo kikubwa sana na TAMISEMI inatakiwa ipewe bajeti ya kutosha pamoja na Utumishi kwa sababu idara zote zipo TAMISEMI, ukitaka afya – TAMISEMI, maji – TAMISEMI, ujenzi – TAMISEMI.
Kwa hiyo, inatakiwa ipate fedha za kutosha ili waweze kutekeleza miradi mbalimbali. Hivi sasa kuna miradi viporo katika majimbo yetu kwa sababu fedha hazipo na zimechelewa kufika TAMISEMI. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili ambalo nataka kuzungumzia ni Jimbo langu la Mpwapwa hasa barabara za Mjini Mpwapwa. Mji wa Mpwapwa ulianzishwa tangu 1905, sasa una zaidi ya miaka 100 lakini hakuna hata barabara moja ambayo ina lami. Kwa hiyo, wakati umefika
sasa barabara za Mpwapwa Mjini zote ziwekwe lami ili ziweze kupitika bila wasiwasi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, barabara nyingine ninayotaka kuzungumzia ni barabara kutoka Gulwe - Berege - Chitemo - Mima - Egoji - Sazima mpaka Seruka. Barabara hii ni mbaya sana, Mheshimiwa Waziri wa TAMISEMI anaifahamu, ni barabara mbaya inapitika kwa shida. Tangu
mwaka jana nimeomba Serikali itenge fedha kwa ajili ya barabara hii ili ifanyiwe marekebisho makubwa, lakini mpaka sasa haijatengenezwa. Halmashauri ya Wilaya ya Mpwapwa haina uwezo wa kukarabati barabara hii kwa sababu uwezo wao ni mdogo. Naomba sasa TAMISEMI ikabidhi barabara hii TANROADS ili iwe chini yake na iweze kufanyiwa matengenezo makubwa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ni kuhusu tatizo la maji vijiji vya Mima, Iyoma pamoja na Bumila. Nashukuru sana Serikali imechimba visima vitatu, imechimba kisima vijiji vya Mima, Iyoma pamoja na Bumila. La kushangaza sasa ni zaidi ya miaka nane visima hivyo
havijawekwa pampu, mabomba wala matenki kwa ajili ya kusambaza maji. Naiomba Serikali visima hivyo viwekwe pampu na kusambaza maji katika vijiji hivyo. Wananchi wa maeneo hayo wana shida kubwa sana ya maji. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine ninalotaka kuzungumzia ni posho za Madiwani. Madiwani posho wanayopata ni kidogo. Bahati nzuri mimi nimewahi kuwa Diwani na Mwenyekiti wa Halmashauri miaka kumi na tano. Mwaka 2012 TAMISEMI waliunda Tume ya kushughulikia maslahi ya Madiwani na iliongozwa na Mheshimiwa George Malima Lubeleje na ikaitwa Tume ya Lubeleje. Bahati nzuri nilifanya kazi nzuri sana pamoja na wajumbe wangu mpaka Madiwani wakakongezwa posho. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini posho ile waliyoongezewa sasa ni zaidi ya miaka mitano, sita haijaongezwa. Udiwani wa zamani ilikuwa ni vikao tu, lakini Udiwani wa sasa lazima Diwani usimamie miradi. Ikianza kujengwa shule Diwani ushinde pale, ikianza kujengwa zahanati Diwani ushinde pale mpaka jioni na posho yao ni ndogo sana. Kwa hiyo, nashauri waongezewe posho ili waweze kutekeleza majukumu yao. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Madiwani wanaitwa ni civic leaders. Kwa nini waitwe civic leaders? Maana katika uchaguzi tunakwenda mafiga matatu, Diwani, Mbunge na Rais lakini baada ya uchaguzi hawa Madiwani tunawaweka pembeni, anabaki Mbunge pamoja na Rais. Kwa nini waitwe civic leaders? Kuna Sheria ya Political Leaders Retirement Benefit, nashauri kama inawezekana sheria hii irekebishwe ili
Madiwani waingizwe katika sheria ile nao wajulikane kama ni viongozi kama sisi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya hawakuwemo kwenye sheria hiyo, walikuwa kama watumishi wa Serikali. Mwaka 1999 nikiwa Mwenyekiti wa Kamati ya Bunge ya Kudumu ya Katiba, Sheria na Utawala tulirekebisha sheria sasa hivi Mheshimiwa Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya wapo kwenye sheria hiyo. Kwa hiyo, kazi ya Mkuu wa Mkoa na Mkuu wa Wilaya ni contract ya miaka mitano, akimaliza miaka mitano analipwa mafao yake, basi kama atateuliwa tena na Rais anayekuja ni jambo lingine. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, jambo lingine nimpongeze sana Waziri wa Utumishi ndiye anayesimamia TASAF na MKURABITA. Tumetembelea Mikoa kama nane kwa ajili ya kuangalia utendaji wa TASAF, wanafanya kazi nzuri sana. Kila Halmashauri ya Wilaya ina Mratibu wa TASAF, ina mratibu wa MKURABITA, hawa ndio walioandikisha kaya maskini, walijua kabisa wanaandikisha kaya maskini lakini leo nashangaa kusikia kwamba walikosea na kuna wengine kati ya walioandikishwa wana uwezo wanatakiwa warejeshe hizo fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi najiuliza mwenye kosa ni nani kati ya aliyeandikisha na kuthibitisha kaya maskini na aliyeandikishwa? Inakuwaje leo unamwambia kwamba hapana wewe una uwezo urejeshe hizi fedha? Naomba Mheshimiwa Waziri kwa kushirikiana na TASAF mlijadili hili suala, lakini TASAF inasaidia kaya maskini kwa sababu watu wanaboresha maisha yao, wanajenga nyumba, wanasomesha watoto na wanapeleka watoto kliniki.
(Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu MKURABITA mradi wa kurasimisha mali, mashamba yanapimwa na wananchi wanapata hati miliki, wanakwenda kukopa benki. Zamani zile hati miliki zilikuwa hazitambuliwi na vyombo vya fedha lakini nashukuru sana Serikali imeshauri mabenki kama CRDB, NMB wamekubali wanazitambua hati miliki za kimila. Kwa hiyo, wananchi wanapata mikopo, wanajenga nyumba bora
na wanasomesha watoto. Kwa hiyo, naipongeza sana Serikali na nashauri MKURABITA na TASAF iendelee.
Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana, huo ndiyo mchango wangu, naunga mkono hoja kwa asilimia mia moja.