Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Hamoud Abuu Jumaa

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kibaha Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. HAMOUD A. JUMAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote napenda kuchukua fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema kwa kuweza kunifikisha mahali hapa na mimi leo hii niweze kuchangia hoja hii muhimu iliyopo mbele yetu. Napenda vilevile kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kuandaa hotuba nzuri ya bajeti yenye mlengo chanya kwa mafanikio, maendeleo ya nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hotuba hii inatupa mwelekeo wa kazi za Serikali na makadirio ya fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na Ofisi ya Bunge, hakika ni mwelekeo mzuri na wa kupongezwa sana, kwani imezingatia Ilani ya Uchaguzi ya Chama cha Mapinduzi ya mwaka 2015. Nichukue
nafasi hii pia kumpongeza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa kufanya ziara maeneo mbalimbali na nimshukuru pia kwa kufanya ziara jimboni kwangu Kibaha Vijijini, ziara zake zimekuwa na tija kubwa sana kwa maendelo ya wananchi, na kufungua fursa mbalimbali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue pia fursa hii kuipongeza Serikali kwa hatua mbalimbali ilizochukua kwa maendeleo ya Taifa letu, hatua ya kuhamia Dodoma na kuwa Mji Mkuu wa nchi yetu ni hatua nzuri na ya kuthubutu, kwani maamuzi yalishafanywa hapo awali na ilikuwa bado
utekelzaji tu. Yatupasa kuunga mkono jitihada hizi na kuishauri Serikali kwa namna yoyote katika uboreshaji wa mkakati huu ambao tayari umeshaanza kwa Wizara mbalimbali kuhamia Dodoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ikumbukwe kila mpango huja na changamoto zake, vivyo hivyo katika mpango huu wa kuhamisha Makao Makuu ya nchi yetu kuja Dodoma unachangamoto mbalimbali, changamoto hizi ni pamoja na mipango miji, barabara na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Dar es Salaam na miji mingine leo hii tunaona kwa namna gani tulichelewa katika kupanga miji yetu na leo hii miji haijapangika, tumekuwa na changamoto mbalimbali ambazo ni wajibu wetu kuzichukua kama fursa na kuja nazo Dodoma na kuziboresha hivyo kuepuka makosa yaliyofanyika katika miji mingine hususan mji wetu wa Dar es Salaam hayana budi kutokutokea katika Mji wetu wa Dodoma. Mipango Miji ipangwe vizuri, kutengwe maeneo ya viwanda, makazi ya watu, ibada, vituo vya mafuta, shule, hospitali, viwanja vya michezo na kadhalika, pia barabara zitengwe maeneo makubwa na ya kutosha ili kuepuka bomoa bomoa za kila mara ambazo tumekuwa
tukizishuhudia katika miji mbalimbali, mji wa Dodoma uwe ni mji wa mfano na wa kihistoria, mitaro ya kupitisha maji (drainage system) iboreshwe kikamilifu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naipongeza Serikali yetu ya Awamu ya Tano kwa kufanikiwa kwa kiasi kikubwa mpango wa kutoa elimu bure wenye tija kubwa kwa wananchi wetu ili kila mtoto wa Kitanzania aweze kupata elimu. Uwajibikaji na nidhamu katika utumishi wa umma
umekua kwa kiasi kikubwa ikilinganishwa na hapo awali ingawa bado zinahitajika juhudi zaidi kufanywa na Serikali ili hii dhana ya uwajibikaji iwe endelevu na yenye tija zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, bado tuna changamoto ya upatikanaji wa huduma mbalimbali kwa wananchi. Napenda kuishauri Serikali yangu sikivu kuzichukua changamoto hizi kama fursa kwa kuboresha maeneo hayo kwa maendeleo ya wananchi wetu na Taifa kwa ujumla.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kugusia suala zima la ukuaji wa uchumi nchini. Serikali imeainisha ukuaji wa uchumi kwa mwaka 2016/2017 unaonesha uchumi wetu unazidi kuimarika. Kwa takwimu za Ofisi ya Taifa ya Takwimu, ukuaji halisi wa Pato la Taifa ulifika 7.0% mwaka 2016, pongezi kwa Serikali ila kuna changamoto nyingi sana katika ukuaji wa uchumi kwa ujumla na ukilinganisha na uchumi wa mtu mmoja mmoja, wananchi wengi ambao vipato vyao ni vidogo na maskini wamekuwa wakiendelea kulalamika hali ngumu ya maisha, mifumuko ya bei za bidhaa muhimu kama chakula na kadhalika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, imekuwa ikiwaumiza sana wananchi na hivyo kutokuona umuhimu wa hizi takwimu za ukuaji ama nafuu ya maisha. Naomba kuishauri Serikali kuwajengea uwezo wananchi ili waweze kukabiliana na changamoto hizi wanazokumbana nazo, Serikali iweze kusimamia vyema mifumuko ya bei isiyokuwa na tija na yenye kumuumiza mwananchi wa kawaida. Serikali isimamie kikamilifu bei za mazao ya wakulima ambao ndio nguvu kazi kubwa hapa nchini, wauze mazao yao kwa faida ya bila vipingamizi vyovyote.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mfano mdogo ni Serikali ilipoamua kusimamia bei la zao la korosho na kufanikiwa kwa kiasi kikubwa kwa wakulima kuuza mazao yao kwa faida nzuri. Hivyo naiomba Serikali ifanye pia katika mazao mengine nchi nzima ili wakulima wetu ambao kitakwimu
ndio wengi waweze kufaidika na kilimo, waondokane na umaskini na kuona faida hizi za ukuaji wa uchumi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishazungumza sana na kuchangia humu Bungeni kwa umakini mkubwa na kuishauri Serikali kuwa viwanda ndio msingi mkubwa wa ukuaji wa uchumi na kumaliza kama si kupunguza tatizo la ajira. Naishukuru Serikali ya Awamu ya Tano ikiongozwa na Dkt. John Pombe Magufuli kuja na kipaumbele hiki cha Tanzania ya viwanda. Na mimi nasema Tanzania ya viwanda inawezekana kwa kuungana sote na kuunga mkono jitihada hizi kwa manufaa ya nchi yetu ili tuondokane na changamoto nyingi tunazokabiliana nazo za ajira kwa vijana wetu ni lazima tuwekeze katika viwanda kwani malighafi mbalimbali tunazo hapa hapa nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi nyingi tajiri kiuchumi duniani ni maamuzi ya uwekezaji wao katika viwanda kwa muda mrefu. Mkoa wetu wa Pwani una viwanda takriban 89, viwanda hivyo viko katika maeneo mbalimbali ya mkoa lakini mpango kazi wetu ni kuzidi kutafuta wawekezaji ili waje kuwekeza katika mkoa wetu hususan Kibaha vijijini kwani tuna maeneo makubwa yametengwa kwa ajili ya viwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna changamoto mbalimbali katika sekta ya viwanda hususan katika utoaji wa vibali vya mazingira. Nashauri vibali hivyo vya mazingira viwe vinatolewa kwa eneo zima ili kuepuka usumbufu wa mtu mmoja mmoja kufanya maombi ya vibali hivyo. Kibaha
Vijijini kama nilivyosema hapo awali tuna maeneo ya kutosha ambayo tayari yameshatengwa kwa shughuli husika. Niliishauri Serikali humu humu Bungeni kuhusu suala la bandari kavu iliyopo Kwala, bandari hii iwe maalum kuegesha magari yote (used), kwa maana kuziondoa yard za kuuzia magari (used) ambazo zimezagaa kila kona ya Jijini Dar es Salaam na hivyo kuwepo sehemu maalum ya mtu akitaka magari (used) anajua wapi pa kwenda hili limefanyika katika nchi nyingi sana zilizoendelea kama Dubai na kadhalika, huwezi kukuta kila kona ya mji kuna yard ya kuuzia magari. Hizi yard zimekuwa zikiharibu mandhari ya miji yetu na uchafuzi wa mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo hilo pia la bandari kavu kuwepo na upatikanaji wa spare tofauti tofauti za magari pamoja na mashine mbalimbali. Hiyo itapelekea kuondokana na maeneo ya mijini kutapakaa maduka ya spare hovyo kama ilivyo hivi sasa mtaa wa Shaurimoyo.
Hatua hii ikikamilika watu watajua wakitaka magari yaliyotumika yote ama spare zote basi wanakwenda Kwala Kibaha Vijijini na kufanya manunuzi. Itasaidia kuwa na sehemu moja tu ambayo utapata hitaji lako ama gari au spare.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwenye hili, Serikali tayari imeshaonyesha nia kwa kutenga maeneo kama ilivyo jimboni kwangu. Kilichobaki ni utolewaji wa elimu na uhamasishaji kwa sekta binafsi kuziona fursa hizi na kuzifanyia kazi. Hatua hii ikishakamilika Serikali itapata fursa ya kuanzisha njia ya treni kutoka Dar es Salaam mpaka Kibaha kuwarahisishia wananchi watakaokuwa wakienda bandari kavu hiyo. Serikali kupata fedha za uendeshaji, vilevile Mkoa wa Pwani hivi sasa umekuwa na watu wengi sana. Kupatikana kwa usafiri wa treni hiyo kutawasaidia watu wengi sana kutatua changamoto ya usafiri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kilio changu cha muda mrefu ni miundombinu ya barabara na mambo mengine mengi, ila kuna hii barabara ya Makofia, Mlandizi na Mzenga ina miaka sita sasa tunazungumzia ujenzi wa barabara hii. Wananchi wamekuwa wakipata shida sana katika shughuli zao za kila siku kutokana na hii barabara, shughuli zao za kiuchumi zimekuwa zikizorota. Naiomba Serikali hii sikivu sasa katika bajeti hii wakamilishe ujenzi wa barabara hii. Wananchi wale na wao waone faraja na kuanza kutumia barabara nzuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika bajeti hii tunaomba fedha zitengwe na barabara hiyo iweze kukamilika. Hata hivyo, niipongeze Serikali kwa jitihada kubwa zinazoendelea kuzifanya kwa kuleta miradi mikubwa ya barabara za juu makutano ya TAZARA, daraja jipya la Salender, ujenzi wa barabara Dar es Salaam – Chalinze kiwango cha express way bila kusahau ujenzi wa barabara za juu (interchange) kwenye makutano ya barabara ya Ubungo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizi ni hatua muhimu za kimaendeleo katika kukabiliana na changamoto ya msongamano wa magari. Vilevile Mji wa Mlandizi kutokana na kukua kwa kasi, kuna uhitaji wa makutano ya barabara ili kurahisisha watumiaji na kuufanya uwe wa kisasa zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa jitihada kubwa inazochukua katika kulinda na kufuatilia sekta nzima ya madini. Hatujachelewa bado na jitihada zilizoanzishwa na Mheshimiwa Rais ni mwanga tosha kwa sasa. Kazi imeanza na kama kulikuwa na upotevu wowote wa madini yetu au ukwepaji wa kodi sasa kila kitu kitakuwa wazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampongeza Mheshimiwa Rais kwa kuunda Tume Maalum ya kufuatilia suala zima katika sekta ya madini. Kama tutaitumia vizuri, basi Taifa litanufaika sana na kupata maendeleo katika nyanja mbalimbali hapa nchini. Madini ni kitu ambacho hakipatikani kila sehemu au nchi madini ni bidhaa adimu sana, hivyo tukifanya maamuzi katika utulivu wenye tija basi hatua stahiki zichujuliwe na hizo
changamoto tuzichukue kama fursa na kusonga mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tusimamie madini yetu yote kwa uadilifu mkubwa, zaidi madini ambayo hayapatikani sehemu yoyote duniani zaidi ya hapa kwetu tuyape thamani na kuyasimamia kwa faida ya Taifa letu ili pato la kodi liweze kuongezeka na kuleta maendeleo kwa wananchi. Vivyo hivyo, tuwawezeshe wachimbaji wadogo wadogo kwa kuwatolea kodi kwa vifaa watavyoagiza ili kuwapa motisha katika kazi zao za uchimbaji. Tuwathamini wazawa ambao ni wachimbaji wadogo kwani wametengeneza ajira hivyo kutokuwapa kipaumbele wao na kuwapa wageni tunawakatisha tamaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya wafugaji na wakulima imeendelea kuibuka maeneo mbalimbali nchini na chanzo cha migogoro hiyo ni ardhi ambayo imekuwa ikigombaniwa. Naipongeza Serikali kwa jitihada zake katika kutatua na kupambana na migogoro hiyo, ila naishauri
Serikali kupitia watumishi wake, maafisa mifugo kuanza kutoa elimu kwa wafugaji kufanya ufugaji wa kisasa ambao hauhitaji kuwa na kundi kubwa la ng’ombe ambao baadaye madhara yake mfugaji anashindwa kuwa na chakula cha kujitosheleza na hivyo kupelekea migogoro kuibuka, kutoa elimu kwa wafugaji kulima nyasi zao wenyewe na kuzihifadhi vizuri ili kipindi cha kiangazi waweze kuzitumia nyasi hizo. Kufanya hivyo kutapunguza sana hii migogoro na kurudisha hali ya kuaminiana na kupendana baina ya wakulima na wafugaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa muda mrefu sasa umepita tangu kuomba kuwekewa kivuko cha kuvukia watu na usafiri, Ruvu Station, Soga, Mpiji, Kwala, Magindu, kukosekana kwa vivuko hivyo kunapeleka wananchi kuwa katika hali ya hatari sana kwani maeneo hayo hayana alama
yoyote. Kwa kuwa kikwazo kwa wananchi kufanya shughuli zao za kila siku pindi wanapotaka kuvuka ama kuvusha vitu mbalimbali. Naomba katika bajeti hii sasa tupewe kipaumbele kwa maeneo hayo kuwekewa vivuko, vilevile kuna uhitaji mkubwa sana kwa maeneo tajwa hapo kuwa na vituo vya treni ili kuwarahisishia wananchi hawa pindi kukiwa na vituo kutakuwepo na fursa mbalimbali maeneo hayo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, changamoto ya mawasiliano bado imekuwa kubwa hapa nchini kwetu. Jimboni kwangu Kibaha Vijijini ni wahanga wa changamoto hii kwani kuna maeneo mengi hakuna kabisa mawasiliano ya simu kwa kuwa hakuna hata kampuni moja ya simu inayopatikana maeneo hayo. Dutumi, Mpelamumbi, Miyombo, Gwata, Msua hakuna mawasiliano kabisa. Tunaomba minara ya Tigo, Vodacom na Airtel, hakika kwa wananchi wangu hii imekuwa ni kero ya muda mrefu sana. Hata hivyo, naipongeza Serikali kwa hatua yake nzuri ya
kukamilisha kituo kimoja cha kuhifadhia taarifa na mifumo ya Serikali (Government Data Centre) na Serikali haina budi kuzihamasisha Ofisi za Serikali kutumia mfumo huu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Awamu zote nilizokuwepo humu Bungeni, nimekuwa nikilisema hili la Kituo cha Afya Mlandizi kupandishwa hadhi. Sifa na vigezo tunavyo. Mheshimiwa Rais wa Awamu ya Nne na Awamu ya Tano walitoa ahadi ya kukipandisha hadhi kituo hiki na kuwa
hospitali. Lakini Awamu ya Nne imepita bila kituo hiki kupandishwa hadhi. Sasa tuko Awamu ya Tano, naomba ahadi hii sasa itekelezwe kwani Mheshimiwa Rais akitoa ahadi, kinachofuata ni utekelezaji kwa mamlaka husika. Hivyo, mimi na wananchi wangu tungeshukuru sana katika
bajeti hii maombi yetu ya muda mrefu na ahadi za Marais wawili zilitekelezwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, nimeona bajeti ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba imeongezeka kutoka shilingi bilioni 31 mwaka 2015/2016 hadi shilingi bilioni 251 mwaka 2016/2017. Ni jambo jema na la kupongezwa ila rai yangu kwa Serikali na mamlaka husika kumekuwa na changamoto za upungufu wa dawa katika vituo vyetu vya afya, zaidi dawa kuchelewa kufika kwa wakati. Naamini kwa ongezeko la bajeti basi changamoto hizi hazitakuwepo tena na kuleta nafuu kwa wananchi kupata dawa kwa wakati na kuwaondolea usumbufu wa kukosa dawa pindi wanapoandikiwa dawa hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mahakama yetu ya Kibaha Vijijini ina changamoto mbalimbali ila kubwa zaidi ni jengo. Jengo lake haliko katika hali nzuri. Katika michango yangu kila mwaka humu Bungeni, mbali na jitihada zangu binafsi za kuonana na Waziri mhusika nimekuwa nikilizungumzia takriban miaka sita bila matumaini yoyote. Naomba Serikali katika bajeti hii basi ituangalie kwa jicho la huruma na sisi tupate jengo la Mahakama. Napenda pia kuikumbusha Serikali kufikisha fedha za bajeti kwa wakati katika Halmashauri zetu kwani bajeti inapita lakini fedha zinachelewa na kuzorotesha shughuli za kimaendeleo. Fedha zikifika kwa wakati na miradi ya kimaendeleo itawafikia wananchi kwa wakati.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kumalizia, napenda kugusia kidogo suala zima la vita dhidi ya dawa za kulevya. Hili ni janga kubwa kitaifa na duniani kote. Dawa za kulevya zimekuwa zikiwaathiri hasa vijana wetu, nguvu kazi ya Taifa. Ndoto za vijana hawa zimekuwa zikisitishwa na kujiingiza katika kutumia dawa hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, napenda kuchukua fursa hii kuipongeza na kuishukuru Serikali ya Awamu ya Tano kwa kuonyesha dhamira ya dhati kabisa ya kupambana na vita hii. Kwanza kwa kuteua watendaji wakuu watakaosimamia Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya. Mamlaka hii ina nguvu ya kukamata, kupeleleza na kushtaki watuhumiwa wanaohusika na biashara ya dawa za kulevya. Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.