Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Rashid Abdallah Shangazi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia mwelekeo wa bajeti kwa Ofisi ya Waziri Mkuu kwa mwaka wa fedha 2017/2018.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianzie alipoishia Mheshimiwa Mhagama kwenye suala zima la kilimo. Naanzia hapo kwa sababu huyu ni pacha mwenzangu naye anaendesha kilimo cha tangawizi kama ambavyo mama yetu Mheshimiwa Anne Kilango amesema sasa ni zamu ya
tangawizi. Napenda kuliambia Bunge lako Tukufu kwamba kule Mlalo, Kata ya Mbaramo, Lunguza, Mnazi na lakini kule katika Jimbo la Madaba na Jimbo la Same Mashariki na Same Magharibi kule ndiko tangawizi inalimwa kwa kiasi kikubwa. Tena sisi tunalima ile tangawizi ambayo ni kilimo hai, tunatumia mbolea ya samadi ambayo inakubalika hata kimataifa. Kwa hiyo, kwa kuungana pamoja na mama yetu Mheshimiwa Anne Kilango naamini jambo hili litapiga hatua kubwa zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli kabisa hatuwezi tukawa na kilimo endelevu kama hatutawekeza kwenye kilimo cha umwagiliaji. Kwa mujibu wa takwimu zilizopo ni kwamba ni asilimia moja tu ya ardhi yote ya Tanzania ambayo ni kilimo cha umwagiliaji. Ina maana Serikali inapaswa kuja na mikakati madhubuti kuhakikisha kwamba sasa kilimo chetu kisitegemee mvua. Kutokana na mabadiliko ya tabia nchi mvua zetu zimekuwa sio za uhakika tena. Kwa hiyo, ni wajibu wa Serikali kuhakikisha kwamba tunawekeza miundombinu ya mabwawa katika maeneo mbalimbali ya Halmashauri zetu ili kilimo hiki kiende kutoa ajira iwasaidie Watanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sambamba na hilo wakati mwingine namshangaa Waziri wa Viwanda na Biashara kwa sababu viwanda anavyozungumza bado haviendi kutatua tatizo kubwa la ajira. Tunahitaji tupate viwanda ambavyo ni shirikishi, viwanda ambavyo vitasaidia kunyanyua soko la bidhaa za mazao. Tukiwa na viwanda vya vigae na malighafi hizi za ujenzi pekee bado wananchi hawa hawatakuwa na uwezo wa kununua hivyo vitu lakini bado hatutatatua tatizo la ajira. Kilimo pekee… (Makofi)
TAARIFA...
MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hiyo ni nzuri lakini mimi sikuwa nazungumzia kiwanda kimoja specific, nilikuwa nazungumzia kwa maana ya nchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hapa ninavyozungumza pale Tanga pana kiwanda kinaitwa AFRITEX kilikuwa kinatengeneza nguo, ni mwaka wa pili sasa kimefungwa.
Mheshimiwa Waziri kila anaposimama anazungumzia viwanda vipya, hivi vya zamani vinavyokufa anavisimamia kwa namna gani? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapozungumzia Kiwanda cha Nguo tunamaanisha kwamba wakulima wa pamba ndiyo watakaoweza kulisha pamoja na kupata soko kupitia viwanda hivi. Kiwanda cha AFRITEX pale Tanga kilikuwa kimeajiri watu zaidi ya 2,000 sasa hivi watu wale hawana ajira. Kwa hiyo, lengo langu ni kusema kwamba, pamoja na ajira za viwandani lakini pia ajira hizi zitokane na mazao yanayozalishwa na wananchi katika maeneo mbalimbali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia Kiwanda cha Rhino Cement palepale Tanga kina tatizo la kupata malighafi. Tatizo lile ambalo alikuwa anakumbana nalo Dangote, Tanga Rhino Cement pia wana shida hiyohiyo. Malighafi wanayopata kutoka kwenye makaa ya mawe kule haitoshi. Uwezo wa kiwanda ni mahitaji ya malighafi tani 20,000 kwa mwezi lakini hawana uwezo wa kupata tani hizo wanaendesha kiwanda mara moja kwa wiki na kiwanda kile wakisimamisha uzalishaji kwa siku moja ina maana ajira zaidi ya watu 700 zitatetereka. Kwa hiyo, pamoja na hiyo nia nzuri lakini tunaomba kwamba viwanda vilivyopo pia viweze kuimarishwa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kiwanda cha Chai Mponde, ni mwaka wa tano sasa hakifanyi kazi kiko kule Bumbuli. Kwa taarifa yako Jimbo la Bumbuli lina kata 18, kata 15 zote wanalima chai lakini ni mwaka wa tano sasa kiwanda kimefungwa, wananchi hawana shughuli zozote za uzalishaji kule. Maana yake ni kwamba hata Halmashauri sasa haiwezi kupata mapato kwa sababu ndani ya Halmashauri yenye kata 15 zinazolima chai, leo chai ile haina soko kwa sababu kiwanda kimefungwa. Mheshimiwa Mwijage anafahamu, Ofisi ya Waziri Mkuu hili wanalifahamu, kwa sababu PPF na NSSF wamekwenda kule lakini mpaka sasa hivi hakuna matumaini. Mheshimiwa Mwijage, sisi ni wajomba zako kule, tunakuomba utunusuru katika hili, Kiwanda cha Chai Mponde kifunguliwe ili wananchi wapate ajira. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ni Kiwanda cha Sabuni cha Foma pale Tanga. Kiwanda hiki kimenunuliwa na mwekezaji Haruna Zakaria lakini amekifunga, kimepoteza ajira zisizopungua watu 1,000. Tunaomba Serikali ikae na mwekezaji huyu kujua kwa nini amekinunua kiwanda na amekifunga, kwa sababu mitambo ipo pamoja na nyenzo nyingine zote zipo pale lakini amefunga. Sasa inawezekana wakati mwingine ni mambo haya ya kodi lakini ni vizuri sasa Mheshimiwa Waziri mwenye dhamana akaenda kukutana na watu hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine niongelee suala la miundombinu ya barabara katika Mkoa wetu wa Tanga. Mkoa wa Tanga, Wilaya za Pangani na Handeni ni sehemu ambayo Mbuga ya Saadani pia inapatikana, siyo kwamba Saadani inapatikana kwa Wilaya ya Bagamoyo pekee. Ili tuweze kuimarisha utalii katika Mkoa wa Tanga, ambapo pia kuna Mbuga ya Hifadhi ya Mkomazi iliyopo katika Wilaya za Kilindi na Lushoto kwa upande wa Tanga, ni lazima sasa ile barabara ya kutoka Pwani - Pangani - Tanga iunganishwe na barabara ya kwenda Maramba – Bombomtoni – Mlalo - Same Mashariki iweze kunyanyuliwa. Hii barabara iko chini ya Wakala wa Barabara wa Mkoa, tunaomba sasa ianze kufikiriwa kuingizwa katika mpango wa kuwekewa lami. Sambamba na hilo, barabara ya kutoka Lushoto - Mlalo – Mnazi - Same kule Ndungu kwa mama yangu Mheshimiwa Anne Kilango pia lazima na yenyewe ifikiriwe kwanza kuwekwa lami. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nayazungumza haya kwa sababu uzalishaji mkubwa wa mazao ya mbogamboga na matunda katika Wilaya ya Lushoto unategemea sana barabara. Inawezekana kabisa kwamba kama kutanyesha mvua barabara ikasumbua ndani ya siku moja unaweza
ukamtia mtu hasara kubwa sana kwa sababu mazao haya yanaharibika kwa haraka. Kwa hiyo, mpango pekee ni kuhakikisha kwamba barabara hii inawekewa lami ili iweze kuwa na uhakika wa kufikisha mazao ya wananchi masokoni. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho niongelee suala la MIVAF. Tumetembelea miradi mbalimbali iliyoko chini ya Ofisi ya Waziri Mkuu kule Pemba na Unguja. Nishukuru kwamba MIVAF ni mradi ambao umesaidia sana lakini unakwisha mwaka huu mwezi Desemba. Niiombe Serikali, kuna tetesi kwamba andiko la miradi hii lipo kwenye Ofisi ya Wizara ya Fedha, tunaomba sasa wasisite waweze kuhakikisha kwamba wanasaini hii mikataba ili angalau tuweze kupata na MIVAF II. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, kule Jimboni Mlalo, tulipata mradi mmoja wa soko kupitia MIVAF lakini nasikitika kusema kwamba soko lile ni dogo sana. Sisi uzalishaji wetu wa viazi, Mheshimiwa Mhagama ni mkubwa sana, tunazungumzia takribani fuso 40 kwa kila wiki zinaingia Dar es Salaam. Bila Lushoto Dar es Salaam chipsi zitakuwa ni adimu sana. Kwa hiyo, tunaomba pamoja na mambo mengine lakini soko lile pale kwenye Kata ya Malindi ambalo limejengwa kwa fedha za MIVAF liongezewe uwezo liwe kubwa zaidi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja. Ahsante sana.