Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Ridhiwani Jakaya Kikwete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Chalinze

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza nianze kwa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia afya njema na kunipa nafasi leo hii ya kuzungumza. Pia nimpongeze sana Mheshimiwa Mama Salma Kikwete kwa kuapishwa kuwa Mbunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Kwa kipindi kirefu sana amekuwa anahangaika na masuala yanayohusu watoto, hasa yatima, wasio na uwezo na akina mama. Nina uhakika kabisa kwa kupata nafasi ya kuwa Mbunge, Mheshimiwa Rais amefanya jambo jema sana kwa makundi haya na sasa watapata mtetezi wa kweli ambaye anayaishi yale atakayokuwa anayaongea. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, namwombea pia kwa Mwenyezi Mungu Rais wetu apewe afya njema sana aendelee kuhudumia Taifa hili ambalo linamhitaji sana kipindi hiki kuliko muda mwingine wowote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, pia namwombea heri mzee wangu, Mzee Chrisant Majiyatanga Mzindakaya ambaye anaugua pale Dar es Salaam, Mwenyezi Mungu ampe afya njema na apone mapema ili aendelee kuwa mshauri katika maisha yetu sisi vijana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, napenda sana pia niwape pole wananchi wenzangu wa Jimbo la Chalinze na Halmashauri ya Chalinze hasa kwa tatizo kubwa lililotupata ndani ya siku mbili au tatu, kutokana na mvua kubwa ambazo zinanyesha sasa katika maeneo yetu.
Tumeshuhudia barabara zikikatika, tumeshuhudia magari yakisimamishwa, safari zinasimama lakini baya zaidi ni uharibifu mkubwa wa miundombinu na nyumba zetu ambao umetokea katika Halmashauri yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nampa tu taarifa Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba hapa ninaposimama leo hii kuzungumza, zaidi ya kaya 150 hazina mahali pa kulala wala hazijui zitakula nini kutokana na tatizo kubwa la mafuriko lililokumba eneo letu lile. Ninachomwomba yeye pamoja na Serikali ni kuangalia njia za haraka zitakazofanyika hasa katika kile chakula cha msaada ili wananchi wangu wa Halmashauri yetu ya Chalinze wapate chakula kwanza wakati tunajipanga kuona mambo mengine tunayafanya vipi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia kipekee kabisa, naomba sana wananchi wenzangu wa Jimbo la Chalinze kwamba Mbunge wao niko pamoja nao sana na katika kipindi hiki kigumu mimi baada ya kumaliza kuchangia leo hii, nitarudi tena kukaa nao na kushauriana nao. Pia tumeomba tukutane kama Madiwani kupitia Kamati yetu ya Fedha ili tuweze kuona tunaweza kuchanga kipi au kutoa kipi katika Halmashauri yetu ili kukabiliana na hali hiyo ngumu
ambayo wananchi wenzangu wanaikabili. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sasa nirudi katika mchango wa Bajeti ya Ofisi ya Waziri Mkuu na nitapenda nianze na eneo la maji na viwanda. Mheshimiwa Waziri Mkuu, tunatambua kwamba Serikali yetu imeweka msisitizo mkubwa sana katika kuhakikisha kwamba viwanda vinajengwa katika eneo hili la Tanzania na katika kipindi hiki kifupi tumeshuhudia mabadiliko makubwa sana katika ujenzi wa viwanda. Waziri Mkuu mwenyewe anaweza kuwa shahidi na Serikali inaweza kuwa shahidi juu ya jinsi wananchi wa Jimbo la Chalinze au wananchi wa Halmashauri ya Chalinze walivyotoa maeneo yao kwa ajili ya kujenga viwanda. Viwanda takriban sita vikubwa vimekwishaanza ujenzi ndani ya Halmashauri yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na viwanda hivyo vinavyojengwa, tatizo kubwa sana lililokuwepo ni upatikanaji wa maji. Tulizungumza na hata juzi alipokuja Waziri Mkuu kufanya ziara katika Halmashauri yetu, aliona juu ya shida kubwa ambayo wananchi wanavyokabiliana na maji lakini pili alipata taarifa ya kina juu ya viwanda vile ambavyo vinaweza vikashindwa kuanza kutokana na matatizo ya maji. Tumezungumza mengi, lakini kubwa zaidi tulimwomba Waziri Mkuu kupitia Wizara ya Maji atoe kibali kwa wale wawekezaji wanaojenga kiwanda kikubwa cha tiles pale Pingo ili waweze kupata access ya kutumia maji ya Ruvu na siyo maji
ya Wami ili waweze kujenga kiwanda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kutoa maji Ruvu mpaka kwenye kiwanda pale Pingo ni kilometa zisizopungua 16; lakini kutoa maji Wami mpaka Pingo ni kilometa zaidi ya 26. Tunachoangalia hapa ni upatikanaji rahisi wa maji hayo na ninashukuru kwamba Waziri Mkuu alinikubalia. Nimeona niseme hapa leo kwa sababu hii ni mikakati ambayo ikiingizwa kwenye bajeti itakaa vizuri. Tunachosubiri kutoka kwake ni kusikia neno kwamba kibali kile kimetoka na kwamba ujenzi wa miundombinu hiyo umeanza. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini siyo hili tu, maji haya yatasaidia pia hata wananchi wa Mji wa Chalinze kwa namna moja au nyingine kwa sababu makubaliano yetu siyo tu maji yaende kwenye kiwanda, lakini pia yaende mpaka pale Chalinze Mjini ili kupunguza tatizo la maji tunalokabiliana nalo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia, kiwanda kikubwa kingine kinachojengwa kule Mboga cha kuchakata matunda nacho kinahitaji maji. Tumezungumza na Mheshimiwa Waziri Mwijage, tunamshukuru kwa jinsi alivyo tayari kukabiliana na changamoto hiyo, lakini pia kinachohitajika zaidi ni ule Mradi wa Maji wa Wami ukamilike mapema ili maji yapate kupelekwa pale na wananchi wa Chalinze wapate kazi, wananchi wa Tanzania wapate matunda kwa Serikali ya Chama cha Mapinduzi katika kipindi hiki cha miaka mitano hii inayoanza mwaka 2015 mpaka 2020. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo, nije katika jambo la vita ya dawa ya kulevya. Katika vita ya dawa za kulevya tunashuhudia mamlaka mbili zenye nguvu tofauti zikifanya kazi moja. Mimi ni mwanasheria, katika utafiti wangu au ujuzi wangu wa sheria, haiwezekani kazi moja ikafanywa na vyombo viwili na ndiyo maana katika mgawanyiko wa kazi hizi, mambo yanagawanyika kutokana na mihimili na kutokana na ofisi. Leo hii tunashuhudia, wako watu wanaitwa na Bwana Siro lakini pia wako watu wanaoitwa na Bwana Sianga. Matokeo yake sasa haieleweki, kumekuwa na double standards katika treatment ya watu hawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninachokiomba kwa kuwa natambua Sheria ya Dawa za Kulevya inayompa nguvu Bwana Sianga ya kuita, kukamata na kufanya inspection, hiyo sheria pia inaingiliwa na Jeshi la Polisi. Naomba Mheshimiwa Waziri Mkuu atakaposimama hapa awaeleze
ni jinsi gani vyombo hivi viwili vinaweza vikatenganisha utendaji ili kutoharibu mlolongo mzima wa upelelezi na upatikanaji wa watuhumiwa hawa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia, Mheshimiwa Waziri Mkuu alikuja kule kwetu na akaenda katika mbuga yetu ya Saadani, ameona jinsi mambo yanavyokwenda na ameona hali ilivyo. Naomba sana Mheshimiwa Waziri Mkuu, wakati anakuja kufanya majumuisho ya hotuba yake azungumzie vizuri juu ya jinsi gani tunaweza ku-promote utalii katika mbuga yetu ya Saadani, lakini pia azungumzie ni jinsi gani Serikai imeweza kukabiliana na vile vilio vya wananchi wanaozunguka mbuga yetu ya Saadani juu ya matatizo ya migogoro ya mipaka iliyopo baina ya mbuga yetu na makazi au vijiji vilivyo jirani hapo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, vilio vimekuwa vikubwa sana, vimefika kwenye Ofisi ya Mbunge, lakini pia vimefika kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu na Waziri Mkuu mwenyewe ameshuhudia watu wakigaragara kumzuia asitoke katika mbuga ya Saadani kwa sababu ya taabu kubwa wanayoipata hasa wenzetu hawa wanaosimamia mbuga wanapoamua kuchukua sheria katika mikono yao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hilo pia, niendelee kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa hatua kubwa anazozifanya. Sisi tulikutana naye, niliongea naye na baada ya kuzungumza naye, siku tatu baadaye akaja Waziri Mkuu kuzungumza juu ya kero ambazo zinawakabili
wananchi wa Chalinze. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba yangu na kwa niaba ya wananchi wa Chalinze, namshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa jinsi alivyomwepesi kukabiliana na changamoto. Katika wepesi huo, naomba niishauri Serikali malalamiko mengine ambayo yanahitaji majawabu kama siyo majibu ya haraka ili kuondoa hizi sintofahamu walizonazo wananchi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nawaomba sana, hakuna sababu ya mtu kama Mheshimiwa Waziri Mwigulu kuendelea kukaa kimya wakati wananchi wanalalamika juu ya hali ya kiusalama katika maisha yao. Mimi binafsi naishauri Serikali yangu kwamba unapojibu jambo lolote lile unatoa hali ya wasiwasi na wananchi wanapata… (Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MHE. RIDHIWANI J. KIKWETE: Mheshimiwa Mwenyekiti naunga mkono hoja.