Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. John Peter Kadutu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ulyankulu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. JOHN P. KADUTU: Mheshimiwa Naibu Spika, ninakushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi niseme kidogo, leo sina maneno mengi wala mapepo hatuyatoi.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika utangulizi ninaotaka kusema nataka kuhubiri juu ya amani. Amani ni kitu muhimu ambacho hakuna mwenye dhamana zaidi ya Watanzania wote. Viongozi wa kisiasa, mwananchi mmoja mmoja tunapaswa kuilinda amani bila kujali itikadi zetu na bila
misimamo ya kimihemuko na ushabiki.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika siku za karibuni na hasa wanasiasa tumekuwa na matamko mbalimbali yanayoashiria kupoteza amani, vitisho mbalimbali vinatokea na matukio mbalimbali kama haya ya utekaji na mambo kadha wa kadha ambayo lazima kama Wabunge humu ndani tuyakemee kwa nguvu zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, mimi kwa miaka miwili na nusu iliyobaki, nasema iliyobaki kwa sababu mwaka 2020 sitagombea Ubunge, nitaendelea kuhubiri amani na baada ya kumaliza Ubunge nitaendelea na kazi ya kuhakikisha amani inaendelea kupatikana, hiyo ni njia sahihi ya kuwakumbusha Watanzania wote juu ya amani. Watu mbalimbali tumekuwa na matamko ambayo napata taabu sana. Kwa hiyo, nilitaka kuwakumbusha wenzangu juu ya umuhimu wa amani, kila mmoja anatamka anavyoweza na kila mmoja ana uhuru wa kutamka anayoweza lakini lazima tuwe na akiba ya maneno, tuwe na vifua vipana vya kuhifadhi maneno, lakini kutafakari athari za maneno tunayoyatamka.
Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kusema hayo sasa nichangie kidogo juu ya hotuba ya Waziri Mkuu. Watu wa Tabora na Jimboni kwangu Ulyankulu, Mheshimiwa Waziri Mkuu tunakupongeza sana kwa kazi nzuri ambayo umeifanya juu ya zao letu la tumbaku, Bodi ya Tumbaku, Bodi ya WETCU na kwa sababu umeahidi kwamba utakuja sasa kumalizia kazi hizo tunakukaribisha kwa niaba ya wenzangu wote tunakuunga mkono kwa hatua mbalimbali unazozichukua. Huu ushirika umekuwa na shida, ushirika ulivunjwa, ukarudi lazima sasa Serikali iwe karibu sana na ushirika na hasa hawa Warajisi wa Ushirika Mikoani, ni watu ambao wakati mwingine wanasaidia kuharibu nia njema ya ushirika na tukukaribishe tena Tabora na utusimamie vizuri hasa uanzishwaji wa vyama vyetu vya ushirika.
Mheshimiwa Naibu Spika, shukrani nyingine ni kwa niaba ya Wabunge wenzangu wenye ulemavu, nitoe shukrani kwa Katibu wetu wa Bunge na Sekretarieti yake kwa kuwa karibu na sisi Wabunge wenye ulemavu. Ofisi ya Katibu wa Bunge imekuwa ikiratibu mambo mbalimbali toka tukiwa na Mheshimiwa Possi na sasa tunakwenda vizuri, lakini tuombe tu Ofisi ya Katibu waweze kutekeleza ombi ambalo tulitoa kwamba Ofisi ya Utawala itengenezewe lift kuwawezesha Wabunge wenye ulemavu kuweza kufika kule juu kuliko na ofisi mbalimbali za Utawala, tuna imani Katibu wa Bunge atakuwa amelisikia, tunafanya kumkumbusha jambo ambalo tulilizungumza huko mwanzo.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala lingine Mheshimiwa Waziri Mkuu ni juu ya uanzishwaji wa maeneo mapya ya utawala. Ukiuchukua Mkoa wa Rukwa, Mkoa wa Katavi, Mkoa wa Tabora eneo lote lile lilikuwa Mkoa wa Tabora limeendelea kukatwa polepole na sasa bado Mkoa wa
Tabora ni Mkoa mkubwa kulikuwa Mikoa yote Tanzania. Lakini hapa katikati Serikali imekuwa inatoa maeneo sisi kazi yetu tunasikiliza tu, mara mmekata Mkoa gani mmewapa, lakini
Tabora hamtaki kuugawa Mkoa, kwa sababu ni Mkoa mkubwa bado tunahitaji Mkoa ugawanywe hata kama tuna azma ya kupunguza matumizi, Wilaya zetu ni kubwa, ukiichukua Wilaya ya Uyui peke yake inaweza ikakusanya Mkoa wa Kilimanjaro na Mkoa wa Tanga ikawa sawa na Wilaya ya Uyui. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ukichukua Wilaya ya Kaliua inaweza kuwa sawa na Mkoa pia wa Kilimanjaro na Tanga kwa pamoja. Kwa nini sasa tukazingatia tu kwamba tunataka kubana matumizi. Mheshimiwa Waziri Mkuu tuombe sana, Ulyankulu tumeomba Wilaya, tumeomba Halmashauri na jambo hili Mheshimiwa Rais wakati wa kampeni aliahidi kwamba siku tatu tu zingemtosha kutoa uamuzi sasa tuna mwaka mmoja na nusu bado tu hamjatafakari kutupa
Wilaya? Bila shaka ujumbe umefika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu nimalizie sitaki kuwa na maneno mengi na sitaki kumaliza dakika zangu zote, kwa niaba ya TFF nitoe shukrani kwa Serikali pamoja na TRA kwa kumaliza mgogoro ambao umekuwepo hata kama haujaisha moja kwa moja lakini
hatua iliyofikia kati ya Shirikisho la Soka nchini pamoja na TRA liko vizuri.
Mheshimiwa Naibu Spika, hapa katikati tuliona na kusikia kwamba TRA iliweza kuwateremsha vijana wetu mashujaa wetu wa Serengeti Boys kwenye basi kisa deni, mpaka pale mamlaka zingine zilipoingilia kati. Mchana huu nilikuwa nawasiliana na Ndugu Malinzi, Rais wa TFF ameniambia kwamba tuko vizuri pamoja na Serikali pamoja na TRA juu ya jambo hili. Kwa niaba ya wadau wote wa mpira na michezo kwa ujumla Mheshimiwa Waziri Mkuu tunakushukuru kuweza kulirahisisha jambo hili ili watu wafanye kazi yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, sitaki kumaliza dakika zangu na inanitosha. Wengine kwenye Wizara na Taasisi nyingine tutakutana mbele ya safari. Naunga mkono hoja.