Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Juma Kombo Hamad

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wingwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, nikushukuru kwa kunipa fursa hii na mimi nichangie mawili, matatu kuhusiana na hotuba ya Waziri Mkuu. Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu kwa kuanza kuchangia katika sehemu
ambayo mara nyingi tumekuwa tukiisemea au imekuwa ikizungumzwa humu kwenye Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Wazanzibari mara nyingi wamekuwa wakijiuliza hatma ya Mashekhe hususan kupitia Wizara ya Katiba na Sheria, lakini leo nimeamua kulizungumza hili kwenye hotuba hii ya Waziri Mkuu tukiwa na matumaini kwamba kilio hiki sasa kinaweza kikasikika. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni juzi tu kupitia Mahakama Kuu ya Zanzibar, Jaji wa Mahakama Kuu ya Zanzibar alinukuliwa kupitia vyombo vya habari akisema kwamba Mashekhe wale wameletwa huku kwa makosa na sasa wanatakiwa warejeshwe Zanzibar kwa namna yoyote itakavyokuwa. Kwa bahati mbaya sana hatukuona hata dalili ya namna ambavyo kuna ushughulikiwaji wa suala lile kuona kwamba Mashekhe wale sasa watarejeshwa Zanzibar na kama ni kuhukumiwa basi watahukumiwa Zanzibar. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, ni miaka minne sasa Mashekhe wale wako ndani, haijulikani tatizo ni nini isipokuwa kinachoonekana pale ni mihemko au hisia tu za kisiasa ambazo zimewafanya Mashekhe wale wanaendelea kusota ndani. Miaka minne imetosha, kama masuala ya upelelezi hayajakamilika kwa nini basi wasipewe dhamana wakaendelea kufuatiliwa wakiwa pamoja na familia zao na huku kesi ile inaendelea? Miaka minne ni mingi sana, naamini kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu ni kubwa, Waziri Mkuu ni mtu mkubwa katika Serikali hii, ndiyo msimamizi mkuu wa shughuli za Serikali anaweza akasikia vilio hivi vya Wazanzibari kuona kwamba Mashekhe wale ni sehemu ya Watanzania wanasikilizwa na wanaachiwa na wanaendelea kuwa huru pamoja na familia zao, hilo ni moja. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la pili, katika mambo ambayo tutayapitisha kupitia Bajeti ya Waziri Mkuu hii ambayo tunaijadili sasa ni pamoja na kujadili Fungu Namba 27 ambalo linagusa Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa. Ni jambo ambalo halikujificha, liko wazi kwamba Msajili wa
Vyama vya Siasa sasa ameamua kwa makusudi kabisa kuingilia na kupandikiza migogoro ndani ya vyama vya siasa. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nasema haya kwa sababu ofisi hii majukumu yake yamezungumzwa ndani ya sheria inayoongoza vyama vya siasa ya mwaka 1992. Moja, kusimamia kumbukumbu za vyama vya siasa; pili, kusajili vyama vya siasa ambavyo vimekidhi matakwa ya sheria hiyo;
tatu, ni kufuta chama cha siasa ambacho kimekwenda kinyume na taratibu hizo ambazo zimezungumzwa ndani ya sheria pamoja na majukumu mengine lakini haya matatu ndiyo majukumu makuu ya Ofisi hii ya Msajili wa Vyama vya Siasa. Kwa bahati mbaya sana Msajili wa Vyama vya Siasa leo amejipa majukumu mengine, sijui kayatoa wapi, madaraka haya sijui ameyatoa wapi ya kuona kwamba sasa ana mamlaka ya kuchagua chama cha siasa kiongozwe na nani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Watanzania wote wanafahamu, Watanzania wote wana akili timamu na wanafahamu kwamba Profesa Lipumba alijiuzulu Agosti, 2015 kwa kuandika barua ya kujiuzulu kabisa. Baada ya miezi kumi Profesa Lipumba anasema anarudi katika nafasi yake ya
Uenyekiti. Katika Katiba hii ya Chama cha CUF hakuna sehemu yoyote ambayo inatoa mamlaka kwamba mtu anapojiuzulu baada ya muda anaandika barua kwamba narudi kwenye nafasi yangu, hakuna. Ofisi ya Msajili wa Vyama vya Siasa ilipokea barua na minutes zote za vikao
kwamba sasa wanaokaimu nafasi ya Mwenyekiti ni hawa. Chama cha CUF kupitia Baraza Kuu la Uongozi kikaunda Kamati ya Uongozi ya Chama na kupeleka kila kilichotakiwa kwa Msajili wa Vyama vya Siasa kutambulisha kwamba sasa wanaoongoza majukumu ya Mwenyekiti ni hawa kwa muda wa miezi kumi. Baada ya miezi kumi Profesa Lipumba anaandika barua ya kurudi kwenye nafasi yake ya Uenyekiti, very shameful. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Jaji akaamua kwa makusudi kabisa kwa sababu eti anataka kuivuruga CUF kutambua kurudi kwa Profesa Lipumba bila kufuata sheria, kanuni, Katiba ya nchi, kwa matakwa yake akaamua sasa kupandikiza mgogoro ndani ya Chama cha CUF. Chama cha CUF hakina mgogoro.
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba niweke sawa, mama yangu mmoja pale alifananisha mgogoro wa Chama cha CUF na ndoa ya mtu na mke wake, akasema kwamba mambo ya mtu na mkewe yanamalizwa chumbani. CUF haikuwa na mgogoro, mgogoro huo ulimalizika mapema Profesa kajiuzulu, Mkutano Mkuu wa Chama ukaitishwa, quorum ikaridhika kwamba Profesa kajiuzulu kama Katiba inavyozungumza, ya nini leo Msajili kufanya haya? Tena angalia sasa cha kushangaza, Msajili wa Vyama vya Siasa anatambua vikao vile na mkutano ule ulikuwa halali lakini anasema maamuzi yake ni haramu. Maana yake ni sawa na kusema nguruwe haramu, lakini mchuzi wake halali, hii haiingii akilini, kwa makusudi akaamua kufanya alivyofanya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi cha ajabu zaidi Msajili huyo wa Vyama vya Siasa alikuja kwenye Kamati, mimi ni Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria, kama Mjumbe wa Kamati ya Katiba na Sheria tulimuuliza sheria hizi umezitoa wapi? Nashukuru Kamati yangu imeandika kama miongoni mwa maazimio, ukurasa wa 30, Kamati pia inaagiza Ofisi ya vya siasa, si jukumu lake. Migogoro ya vyama vya siasa viachiwe vyama vya siasa, Msajili asiwe ni sehemu ya mgogoro wa chama cha siasa. Chama kina taratibu, sheria, Katiba na kanuni zake, leo iweje yeye apange? Ni ajabu! (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, juzi anatushangaza hapa sasa, anakuja kwenye Kamati anajitetea siku ya pili anasema anamtangaza kwamba sasa Sakaya ni Kaimu Katibu Mkuu. Sakaya alishasimamishwa uanachama, Sakaya alishasimamishwa uongozi, leo kwa sababu tu una mambo
yako unayatafuta unakuja …
Mheshimiwa Sakaya, Mbunge wa Kaliua, anamtambua kwamba eti ni Kaimu Katibu Mkuu wa Chama, aibu! Katibu Mkuu wa Chama yupo anafanya shughuli zake za kisiasa kama kawaida unashawishiwa, wewe umepanda shetani gani? Aliyekushawishi ni nani? Kakupandikiza nini? Kama kuna mtu anakusukuma au anakushawishi, wewe ni Jaji unapaswa uwe na heshima. Tunasema kama ana ndoto ya kufikiria kwamba Chama cha CUF kinakwenda kufa mikononi mwake, Chama cha CUF hakifi, kitaendelea kuweko imara na kitaimarika zaidi. Kama anahisi kwamba Chama cha CUF kinakwenda kufa basi hilo alisahau kabisa (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nizungumzie kidogo suala la utekaji. Nchi hii haiko salama tuseme kweli. Asubuhi watu wameomba miongozo umewakatalia ni suala la hatari. Kama unakumbuka kila siku zikienda mbele hali hii inazidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, ulinisimamisha kidogo naomba dakika yangu moja ambayo ulinisimamisha…
NAIBU SPIKA: Zilikuwa ni sekunde 10 ambazo zimeshaisha.
MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Naibu Spika, tulishuhudia Salma Said, Mwandishi wa DW alitekwa uwanja wa ndege...
NAIBU SPIKA: Haya ahsante sana Mheshimiwa.