Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Margaret Simwanza Sitta

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Urambo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. MARGARET S. SITTA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii. La kwanza kabisa, kwa niaba ya familia yetu ya marehemu mzee Sitta, nachukua nafasi hii kuishukuru Serikali inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, Serikali nzima,
uongozi wa Bunge unaoongozwa na Mheshimiwa Spika, Waheshimiwa Wabunge, viongozi wa vyama kisiasa, viongozi wa dini, wananchi wote Tanzania kwa jinsi ambavyo walitufariji sana sisi familia ya marehemu Mzee Samuel Sitta; tunawashukuru sana, tunaomba ushirikiano mliotupa sisi uendelee. (Makofi). Mungu ibariki Tanzania, lakini pia tunamwomba Mungu aiweke roho ya marehemu Samuel Sitta mahali pema peponi, Amina.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia nichukue nafasi hii kumpa pole Mheshimiwa Spika na Waheshimiwa Wabunge kwa kifo cha mwenzetu, Mheshimiwa Dkt. Macha, tumwombe Mwenyezi Mungu aiweke roho ya marehemu Dkt. Elly Macha mahali pema peponi, Amina.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitazungumzia katika sekta tatu. Kwanza kabisa naomba nianze na Sekta ya Kilimo. Kwa niaba ya wananchi wa Jimbo la Urambo, nasema wazi kwamba huwezi kuzungumzia hali ya kiuchumi na maendeleo ya kiuchumi ya wananchi wa Urambo bila kuzungumzia suala la tumbaku. Nawapongeza Waheshimiwa Wabunge wote mnapoongea mkizungumzia suala hili kwa sababu ni muhimu
sana katika maendeleo ya wananchi wa Urambo. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, namshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa niaba ya wananchi wa Urambo kwa jinsi alivyochukua hatua mbalimbali katika kunusuru zao la tumbaku, nakushukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu. Pamoja na hatua mbalimbali ambazo Mheshimiwa Waziri
Mkuu amezichukua bado kuna maswali ambayo ningeiomba Serikali ichukue hatua za haraka kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza, kwa kuwa Bodi ya Tumbaku imevunjwa, je ni lini Serikali itaunda bodi mpya kwa sababu sasa hivi mwezi wa Nne ndiyo masoko ya tumbaku yanatakiwa yaanze? Pia, pamoja na kuunda bodi mpya, Serikali imejipanga vipi kuiimarisha Bodi mpya ya
Tumbaku ili iweze kufanya kazi zake kwa ufanisi zaidi hususan upatikanaji wa classifiers, wale ambao wanapanga tumbaku katika grades zinazotakiwa wakati wa kuuza tumbaku na msimu ndiyo huu mwezi wa Nne?
Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile ningependa Serikali itueleze, wakulima wana tozo nyingi, sasa hizi tozo Serikali imejipangaje kuziondoa ili mkulima naye anufaike na zao lake analolihangaikia mwaka mzima?
Mheshimiwa Naibu Spika, lakini wakati huo huo amri ilitolewa na Serikali ya kuvunja uongozi wa AMCOS mbili za Utenge na Nsenda, lakini msimu wa tumbaku umefika, lini Serikali itaondoa amri hiyo ili kuwe na uongozi katika AMCOS hizo waweze kushughulikia uuzaji wa tumbaku haraka iwezekanavyo kwa sababu kama nilivyosema mwezi wa Nne ndiyo wanaanza?
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la tumbaku, tunaiomba sana Serikali itilie mkazo hasa upatikanaji wa mbolea. Tunapoanza na mbolea kuchelewa kutakuwa na matatizo makubwa. Je, wakati huu ambapo Bodi ya Tumbaku imevunjwa nani atakayeshughulikia suala la upatikanaji wa mbolea haraka iwezekanavyo?
Mheshimiwa Naibu Spika, nirudi kwenye upande wa changamoto nyingine tuliyonayo, upande wa suala la maji. Sasa hivi sisi Urambo hatuna maji na kuna mpango ambao Serikali imeuandaa wa kupata maji kutoka Malagarasi, lakini utachukua muda mrefu, je, Serikali imejipangaje kipindi hiki ambacho mradi wa Malagarasi unaendelea, hawawezi kutuchimbia visima, hawawezi kutuchimbia mabwawa ili tutumie wakati tukisubiri mradi huu wa maji wa muda mrefu kutoka Mto Malagarasi? Kwa hiyo, tunaiomba Serikali ifanye hilo.
Mheshimiwa Naibu Spika, la tatu ni suala la afya. Ningeiomba Wizara ya Afya kwanza kwa kuanzia hebu ibane halmashauri kwa kushirikiana na viongozi wa halmashauri (TAMISEMI); kwamba ni jinsi gani halmashauri zimepanga fedha hususan kwa ajili ya kuokoa maisha ya mama na
mtoto? Kila siku wakati wa kujifungua hapa Tanzania tunapoteza akinamama 30. Je, Serikali kwa kupitia Wizara ya Afya imejipangaje ili kuhakikisha kwamba fedha mahususi zinapangwa kwa ajili ya kuokoa vifo vya akinamama na watoto?
Mheshimiwa Naibu Spika, wakati huohuo nichukue nafasi hii kuishukuru sana Serikali kwa kuchagua Jimbo la Urambo au Wilaya ya Urambo kuwa miongoni mwa wilaya ambazo zitapata fedha moja kwa moja kupelekwa kwenye vituo vya afya, zahanati na hospitali.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, nauliza moja tu; je, Serikali imejipangaje kuhakikisha kwamba zahanati zetu zinakuwa na watumishi waliotosha? Kwa mfano, sisi tuna zahanati 21, hamuwezi kuamini katika zahanati 21, 15 hazina maafisa tabibu, sasa wagonjwa wanaandikiwa matibabu na nani? Wakati huo huo upungufu ni asilimia 77, yaani ufanisi wa utumishi ni aslimia 33 tu. Sasa fedha zikipelekwa moja kwa moja kwenye zahanati na vituo vya afya nani anashughulikia fedha hizi?
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, natoa ushauri kwamba haraka iwezekanavyo tusaidiwe sisi wa Jimbo la Urambo kupewa wafanyakazi wa kutosha haraka sana ili waweze kutekeleza hili zoezi la kupeleka fedha moja kwa moja kwenye zahanati. Wewe fikiria mahali ambapo kuna
watumishi wawili nani anamwangalia mwenzake? Nani anatimiza wajibu wa kuhudumia wagonjwa? Nani anatunza fedha? Kwa hiyo la kwanza ni upatikanaji wa watumishi haraka iwezekanavyo lakini pili, tunaiomba Serikali iajiri wahasibu ili hizi fedha zitakazokuwa zinapelekwa kwenye
zahanati ziweze kutunzwa kadri iwezekanavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema, kutokana na uhaba mkubwa watumishi kwa asilimia 77 katika Jimbo langu, naamini na wenzangu wako kwenye matatizo ya hivyo hivyo. Mimi kama Mbunge wa Jimbo la Urambo naomba Wizara husika ituanzishie Chuo pale pale
kama ilivyo Nzega na kadhalika ambacho kitafundisha Watumishi wa kada ya kati ili na sisi tupate watumishi haraka iwezekanavyo kutokana na uhaba tuliokuwa nao.
Mheshimiwa Naibu Spika, pia Kanda ya Magharibi, ukichulia hasa Mkoa wa Kigoma na Tabora, hatuna Hospitali ya Kanda. Tunachukua nafasi hii kuiomba Serikali na sisi Mkoa wa Kigoma na Tabora tujengewe Hospitali ya Kanda kwa sababu inatubidi kuja Dar es Salaam au kwenda Mwanza wakati wenzetu wanazo karibu kadri iwezekanavyo. Kwa hiyo, tunaomba Serikali ifanye hivyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, vilevile nilikuwa nafikiria kwamba hili suala la upatikanaji wa Watumishi wa Afya, Serikali ilitilie maanani ndugu zangu. Kwa hali ilivyo, kama Serikali haitachukua mkakati maalum, tutapata shida sana kuhusu watumishi.
Mheshimiwa Naibu Spika, nafikiri suala la upungufu wa Watumishi wa Afya liangaliwe ipasavyo na nitashukuru sana. Kama viongozi wetu, Mawaziri mtakuja kwetu kule kama alivyofanya Mheshimiwa Waziri Mkuu kuja Tabora kuangalia suala la Tumbaku na Mawaziri husika naomba mje mwangalie uhaba wa watumishi tulionao kwenye Mkoa wetu wa Tabora kwa ujumla lakini pia Wizara Afya. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, nashukuru kwa kupata nafasi, lakini naomba sana, katika kujumuisha hapa, tupate majibu, lini tumbaku itapata uongozi wa haraka iwezekanavyo? Ile Bodi ya Tumbaku ipate uwezo wa kuajiri wafanyakazi wa kutosha ili masoko sasa yanayoanza mwezi huu yaende kama yalivyopangwa. Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi.