Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi jioni hii ya leo ili na mimi niweze kuchangia hotuba hii ya Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Spika, kama ilivyo ada, naomba nijielekeze moja kwa moja kwenye hotuba hii nikilenga kwanza hii Taasisi ya Uvunaji wa Misitu (TFS). Kama ambavyo unafahamu 60% ya Wilaya ya Liwale inazungukwa na misitu, kwa hiyo, uchumi mkubwa wa watu wa Liwale unategemea sana maliasili za misitu pamoja na wanyama. Kwa hiyo, naomba moja kwa moja nianzie huko.
Mheshimiwa Spika, namwomba Waziri Mkuu au Wizara inayohusika walete hapa marekebisho ya Sheria ya TFS. TFS kutupatia sisi Halmashauri 5% ya uvunaji wa mazao ya misitu kwa kweli ni kutokututendea haki. Ukienda kuangalia Liwale jinsi magogo yanavyovunwa pale, miti inavyohama na faida wanayoipata Wanaliwale wale kwa 5%, tena hiyo 5% yenyewe namna ya kuipata ni kwa shida kwelikweli. Naomba hii sheria iletwe hapa irekebishwe, 5% ni ndogo sana.
Mheshimiwa Spika, vilevile naomba niuelekeze mgogoro wa Hifadhi ya Selou pamoja na Wanakijiji wa Kikulyungu kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu. Kwa nini nauelekeza mgogoro huu kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu? Ni kwa sababu kwenye Wizara husika naona mgogoro huu umeshindikana.
Kwa hiyo, naomba moja kwa moja kwa nafasi hii niuelekeze mgogoro huu kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu pengine tukapata msaada ili wale wananchi wa Kikulyungu wakaepukana na adha wanayoipata leo hii ya kupigwa vibaya na Askari wa Wanyamapori.
Mheshimiwa Spika, baada ya hapo naomba nijielekeze kwenye upande wa takwimu. Sensa ya mwaka 2012 kwa kweli sisi Wilaya ya Liwale imetuathiri sana. Imetuathiri kwa maana ya kwamba, imeonesha wakazi wa Wilaya ile ni kidogo sana. Nitoe mfano ufuatao. Wilaya ya Liwale kwenye Basket Fund tunapata Sh.8,000,000/=, Wilaya ya Nachingwea Sh.18,000,000/=, Wilaya Kilwa Sh.17,000,000/ =, Wilaya ya Ruangwa Sh.21,000,000/=. Basket Fund, Liwale 350, Ruangwa bilioni 1, Kilwa milioni 600, Nachingwea milioni 800 lakini sisi hii idadi tuliyonayo sio kweli kwamba Wilaya ya Liwale yenye Kata 20 ina watu 92, siyo kweli, hii takwimu sio sahihi.
Mheshimiwa Spika, nashindwa kuwaelewa hawa watu wanaosimamia hizi takwimu. Katika Mkoa wa Lindi, Hospitali pekee inayoona wagonjwa wengi kwa mwezi ni Hospitali ya Wilaya ya Liwale lakini ndio hospitali pekee inayopata mgawo mdogo. Naomba nilielekeze hili kwenye Ofisi ya Waziri Mkuu ili liweze kupatiwa ufumbuzi.
SPIKA: Mheshimiwa Zuberi Kuchauka, kuna taarifa.
TAARIFA...
MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Spika, ahsante. Napokea taarifa yake kwani haijapingana na nilichokieleza lakini bado narejea palepale, kama takwimu za hospitali zinaletwa kila mwezi kwamba katika Mkoa wa Lindi hospitali inayoona wagonjwa wengi ni ya Wilaya ya
Liwale. Sasa ni mwenye akili gani timamu hiyo hospitali inayoona wagonjwa wengi akaipa mgawo kidogo? Napata wasiwasi. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba nijielekeze kwenye upande wa hiyohiyo takwimu inatuathiri vilevile kwenye mgawo wa wafanyakazi kwa maana ya ikama ya wafanyakazi. Ikama ya wafanyakazi kwa upande wa elimu, ikama ya wafanyakazi kwa upande wa afya, tuna matatizo sana. Mpaka leo hii ninavyoongea kwenye Bunge hili Tukufu, Liwale hatuna daktari bingwa, tuna uhaba wa madaktari, tuna uhaba wa walimu wa sekondari, lakini ukiuliza unaambiwa kwamba wale waliopo ndio wanafanana na idadi ya watu walioko kule wakati sio kweli. Naomba hizi takwimu zirekebishwe, kama ripoti unaletewa ya idadi ya wanafunzi iweje sasa ushindwe kuitumia ripoti hiyo uende mwaka 2012? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naingia kwenye vyama vya ushirika. Vyama vya ushirika naomba iletwe sheria hapa ili tufanye marekebisho, vyama vya ushirika wawekewe masharti namna ya kuajiri wahasibu. Tumepata matatizo sana mwaka huu, kwenye Chama Kikuu cha Lunali hawajawahi
kupatiwa fedha kama mwaka huu lakini wamevurunda mpaka sasa hivi vyama vya ushirika wameshamaliza pesa lakini wakulima hawajapata hela. Sawa, wale viongozi wa vyama vya msingi tutawapeleka Mahakamani watafungwa au watafilisiwa lakini bado mkulima aliyepeleka korosho yake mwezi wa 10 mwaka jana mpaka leo hajapata hela. Kufungwa au kupelekwa Mahakamani kwa huyu mtu mkulima yule imemsaidia nini?
Mheshimiwa Spika, leo hii mwezi wa Nne tunaandaa mashamba lakini mtu amepeleka korosho mwezi wa 10 mpaka leo hajapata pesa. Ombi langu ni kwamba, Sheria ya Vyama vya Ushirika iletwe hapa, tuwaundie sheria ili ajira za vyama vya ushirika ziendane na taaluma. Kwa sababu
tatizo kubwa tulilolipata safari hii ni watu hawana taaluma ya uhasibu. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, nijielekeze kwenye Sera ya Wazee. Sera ya Wazee imetungwa nafikiri tangu mwaka 2003 lakini mpaka leo Sheria ya Wazee haijawahi kuletwa kwenye Bunge hili, sijui mmekwama wapi? Naomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge hapa ndani sisi wote hapa ni wazee watarajiwa. Tunapolichelewesha hili tunajichelewesha sisi wenyewe na waathirika wakubwa ni sisi, leo vijana, kesho ni wazee.(Makofi)
Mheshimiwa Spika, napenda kuwapongeza sana wenzetu Zanzibar pamoja na uchumi wao kuwa hafifu lakini wamewakumbuka wazee angalau hata kuwapa Sh.200/=. Leo hii Tanzania Bara tumenyamaza, hata hiyo Sh.10,000/= tuliyoambiwa watapewa mpaka leo haijulikani, tutafikaje huko hata sheria yenyewe haijaletwa hapa? Naomba sana Sheria hii ya Wazee iletwe hapa ili tuone wazee sisi watarajiwa huko mbele tumejiwekea akiba gani?
Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa napenda nizungumzie kuhusu bajeti. Watu wengi sana wamezungumzia kuhusu upelekaji wa fedha kwenye miradi ya maendeleo, kwenye OC, siyo mzuri. Jamani, hapa tatizo siyo upelekaji, hela hakuna! Mimi sidhani kama Serikali wana
pesa halafu hawapeleki! Tuseme kweli kwamba pesa hizo hazipo, makusanyo hayo hayapo! (Makofi)
Mheshimiwa Spika, naomba Waziri wa Fedha anieleze pengine mimi kwa sababu ya elimu yangu ndogo sielewi. Hizi figure hizi zinazokuja hapa kila mwaka ambazo hata 50% tunashindwa kuzifikisha zina maana gani? Kuna tofauti gani leo hii tukasema kwamba hii bajeti yetu ni ya
shilingi trilioni 18 badala ya kuweka 30? Shilingi trilioni 18 tunaweza tukaifikia! Kwa nini tunaweka shilingi trilioni 31 ambayo mwisho wa siku hata shilingi trilioni 20 hatufiki! Kuna sababu gani? (Makofi)
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naomba Waziri mwenye dhamana anisaidie ili na mimi nipate uelewa ili siku nyingine nisije nikasimama tena hapa nikauliza kuhusu jambo hilihili. Kwa nini tunaletewa hizi figures kubwa kubwa ambazo hazina mwisho?
Mheshimiwa Spika, mwisho kabisa naomba niongelee walimu. Kuna tatizo kubwa sana la matokeo. Matokeo ya elimu mwaka huu, kwa mfano kama Mkoa wa Mtwara, Mheshimiwa Spika shahidi, Mkuu wa Mkoa ametimua watu, amepunguza watu lakini mimi nasema hii siyo solution, solution ni kuangalia maisha ya walimu.
Mheshimiwa Spika, walimu wetu tumewasahau na kama tumesahau walimu na elimu nayo tunaisahau. Ahsante sana. (Makofi)
SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa Kuchauka. Tupelekee salamu kule Liwale Mjini pale Makunjiganga, Nangano, Kimambi unapoelekea Kilwa, Kikulyungu unapoelekea Nachingwea, Mtawatao kwenye mpunga, Ndapata unapopakana na Selou, Barikiwa. Liwale sio ya kwako peke yako bwana. Mheshimiwa Kakunda.