Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

Hon. Jerome Dismas Bwanausi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lulindi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Fedha za Ofisi ya Waziri Mkuu na taasisi zilizo chini yake pamoja na Mfuko wa Bunge kwa mwaka 2017/2018.

MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Spika, kwanza nianze kwa kutoa shukrani kwa kupata fursa hii kama mchangiaji wa kwanza kwenye hotuba ya Waziri Mkuu.
Nianze tu kwa kumpongeza Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli, kwa kazi kubwa anayoifanya na kuonesha uzalendo wa hali ya juu katika kuhudumia Taifa letu.
Mheshimiwa Spika, la pili, namshukuru sana mtoa hoja, Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa jinsi alivyotoa hotuba yake na jinsi alivyojaribu kuchambua maeneo mbalimbali yanayohusiana na shughuli mbalimbali za kiuchumi na kijamii katika nchi yetu.
Mheshimiwa Spika, labda niende moja kwa moja, lakini pia bila kuwasahau Waziri anayeshughulikia Bunge, Ajira, Kazi, Vijana na Watu wenye Ulemavu, Mheshimiwa Jenista Mhagama pamoja na Naibu wake, ndugu yangu pale Mheshimiwa…
SPIKA: Mavunde!
MHE. JEROME D. BWANAUSI: Mheshimiwa Mavunde kwa kazi nzuri wanayoifanya katika Wizara hiyo.
Mheshimiwa Spika, niende moja kwa moja kwenye kilimo na hasa kwenye ukurasa wa 23 wa kitabu cha hotuba ya Waziri Mkuu, alipozungumzia zaidi suala la stakabadhi ghalani. Nianze tu kwa kusema, kwa kweli Sheria ya Ushirika inabidi tuombe mamlaka zinazohusika zilete sheria ile tena, tuifanyie marekebisho kwa sababu sheria ya ushirika ina upungufu mwingi sana na kusababisha wananchi wetu
kupata athari mbalimbali katika kupata haki zao katika mazao yao.
Mheshimiwa Spika, nakubaliana kabisa na hoja ya Waziri Mkuu kwamba maeneo mengi, stakabadhi ghalani imeonekana moja kwa moja kuwa ndiyo ufumbuzi wa matatizo ya masoko katika mazao yetu mbalimbali, ikiwemo kahawa, chai, tumbaku, pareto, korosho na mengineyo.
Nitolee mfano zao la korosho; tatizo kubwa lililojitokeza kufanya wakulima wetu wasipate haki vizuri ni tatizo la vyama vya msingi na vyama vikuu wakati mwingine kufanya kwa makusudi kabisa hujuma ya kuiba fedha za wakulima.
Mheshimiwa Spika, nikitolea mfano, wananchi walipeleka zao lao la korosho kwenye maghala tangu Septemba mwaka 2016, lakini ninavyosema hivi sasa, kwenye Halmashauri yangu ya Wilaya ya Masasi kiasi cha zaidi ya sh. 1,200,000,000/= hazijalipwa kwa wakulima.
Mheshimiwa Spika, jambo hili linawakatisha tamaa wananchi na ndiyo maana nimesema ile Sheria ya Ushirika inabidi tuitazame upya, kwa sababu wenzetu wanaopata mamlaka kwenye vyama vya msingi na vyama vikuu wamegeuka kuwa miungu watu na kuona kwamba wao
wana uhuru uliopitiliza kana kwamba wanaishi kwenye himaya tofauti na Watanzania wengine.
Kwa hiyo, ombi langu kwa Ofisi ya Waziri Mkuu ni kwamba hebu iingilie kati kuona jinsi gani wananchi hawa wanavyoweza kupata haki zao, kwa sababu kwa kweli ni jambo ambalo wananchi hawalielewi, kwa sababu hakuna korosho zilizopo kwenye maghala lakini fedha zao
hazionekani zipo wapi.
Mheshimiwa Spika, niende kwenye suala la tozo kama alivyozungumzia Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba Serikali mwaka huu imepania kuhakikisha kwamba inaondoa baadhi ya tozo kwenye mazao mbalimbali ya biashara yakiwemo tumbaku, chai, kahawa pamoja na korosho.
Bahati nzuri mimi ni miongoni mwa wanaotoka kwenye maeneo yanayolima zao la korosho; Masasi ni Wilaya ya pili kwa uzalishaji ukiachia Tandahimba. Kwa kweli tunampongeza sana Rais pamoja na Waziri Mkuu kwa jinsi ambavyo wameshiriki katika kufanya zao la korosho kwa
mwaka huu liweze kufikia kilo moja sh.3,800/=. Naamini kabisa Serikali ikiendelea kukaza uzi korosho zinaweza kuwa na uwezo wa kuuzwa sh. 5,000/= kwa kilo katika misimu ijayo.
Mheshimiwa Spika, naomba sana katika tozo zile ambazo Mheshimiwa Waziri Mkuu amezisema, lakini napenda kwa mfano tozo ya magunia ambayo kwa kweli inatozwa kwa wakulima, nadhani iondolewe pamoja na zile nyingine ili kumfanya mkulima aweze kupata unafuu zaidi.
Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningetaka niliseme, ni juu ya masuala ya umeme. Bahati nzuri ameelezea Mheshimiwa Waziri Mkuu katika hotuba yake kwamba Serikali ina nia nzuri ya kusambaza umeme, lakini napenda sana ieleweke kwamba wananchi wa Mikoa ya Mtwara na Lindi kwa sababu ambazo hata Mawaziri wanazijua kwamba maeneo haya yaliachwa kupewa huduma za umeme tangu mwanzo kwa sababu kulikuwa na tetesi kwamba Mkoa huu wa Mtwara na Lindi ulikuwa uhudumiwe na kampuni ambayo ilianza pale kusambaza gesi. Kwa hiyo, baadaye Serikali iliamua kusitisha makubliano yale na TANESCO kuendelea kuhudumia mikoa hii.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tatizo ambalo lipo ni kwamba maeneo, vituo au Wilaya za Mkoa wa Mtwara na Lindi hazina magari. Hata magari yaliyoletwa hivi karibuni, hayakusambazwa tena katika mikoa hii vizuri na kufanya utendaji wa kazi katika Mkoa wa Mtwara na Lindi hasa Wilaya ya Masasi kuwa mgumu sana kiutendaji kwa sababu hawana usafiri. (Makofi) Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naiomba sana Serikali
ione kwamba eneo hili linahitajika kutazamwa vizuri zaidi. Naipongeza suala la REA Awamu ya Tatu, kwamba linazinduliwa katika mikoa, lakini nataka tu nitoe angalizo kwa Serikali kwamba kama Mkoa wa Mtwara na Lindi haukutazamwa vizuri, unaweza ukajikuta maeneo mengine
yote nchini yamemaliza vijiji vyake, lakini Mtwara na Lindi vikabaki kwa sababu kule hatukuwahi kupata ile phase one
na wala zile fedha za MCC kwa ajili ya umeme hazikupatikana.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tukienda kwa uwiano ulio sawa, basi mikoa hii bado itabaki nyuma. Kwa hiyo, naomba sana hata katika usambazaji umeme, katika maeneo ambayo umeme ulipita muda mrefu, utakuta maeneo ya Mkoa wa Mtwara na Lindi bado maeneo mengi
sana umeme umepita lakini wananchi hawajanufaika.
Mheshimiwa Spika, lingine ni suala la reli. Naomba sana hii reli ya kutoka Mtwara kwenda Mchuchuma na kama Mheshimiwa Nape alivyokuwa analalamika kwamba maeneo mengi yamewekwa ‘x’ lakini hatuoni zile juhudi za hasa za kuhakikisha kwamba kweli reli hii inataka ijengwe
hivi karibuni.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.