Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, na mimi kwa haraka haraka lakini siyo kwa umuhimu, nianze kwa kuipongeza sana Kamati inayosimamia masuala ya UKIMWI na masuala ya mapambano dhidi ya dawa za kulevya inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Ndugulile na Makamu Mwenyekiti Dkt. Tiisekwa na Wabunge wote Wajumbe wa Kamati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati hii kwa kweli imeanza kazi vizuri na ninaomba niseme kwamba inatushauri vizuri sana. Kwa hiyo, naomba niwashukuru sana Wajumbe wa Kamati hiyo. Sitakuwa nimejitendea haki kama sitakumbuka mchango mkubwa uliotolewa na Mheshimiwa Dkt. Ndugulile na Mheshimiwa Ester Bulaya wakati wa kutungwa kwa Sheria Namba 5 ya mwaka 2015 ambayo imetupelekea katika azma ya Serikali ya kupambana na dawa za kulevya katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nichukue nafasi pia ya pekee kabisa kuwapongeza sana Wabunge wote ambao tulikuwa wote pamoja katika Bunge la Kumi la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Nakumbuka sheria hiyo ilikuwa ni sheria yangu ya kwanza nilipoteuliwa kuwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Waziri Mkuu, lakini Waheshimiwa Wabunge waliniunga mkono sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kweli sheria hii mpya ni sheria nzuri na imeweka adhabu za kutosha kabisa za kupambana na tatizo la dawa za kulevya katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa labda niseme yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo la dawa za kulevya katika nchi yetu ya Tanzania lina historia. Historia ya ongezeko la tatizo hili ilianza toka miaka ya 1990 na miaka ya 1990 Serikali imekuwa ikihangaika sana kuona ni namna gani itaweka mifumo ya kisheria na taratibu za kupambana na dawa za kulevya katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 1995 Serikali kupitia Bunge hili la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ilitunga Sheria Namba 9 ya mwaka 1995 lakini sheria ile ilikuwa na kazi ya kuratibu tu masuala haya ya tatizo la dawa za kulevya nchini na ilionekana kwamba sheria ile haina nguvu yoyote. Watu wakikamatwa, sheria ilikuwa haiipi Tume ya Dawa za Kulevya nguvu ya kupekua, kupeleleza na kushitaki. Kwa hiyo, tulikuwa tunaona kulikuwa na upungufu mkubwa sana katika Sheria ya mwaka 1995. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, dhamira ya Serikali ilianza kujionesha mwaka 2014. Mwaka 2014 tulifanya utafiti wa nguvu kazi katika nchi yetu ya Tanzania na tukagundua kwamba nguvu kazi ya vijana kwa miaka 14 mpaka 35 ni asilimia 56. Hiyo asilimia 56 ya nguvu kazi ya vijana ndio hao ambao wanaathiriwa na madawa ya kulevya katika nchi yetu ya Tanzania. Kwa dhamira ya dhati, mwaka 2015 ndipo tukaamua kuja na Sheria Namba 5 ya mwaka 2015; lakini sheria hiyo sasa ikaweka nguvu nyingine ya ziada; hiyo sasa ikawa na ajenda ya kudhibiti na kupambana na dawa za kulevya katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme jambo hapa, mchakato sasa wa kuunda hii mamlaka ambayo itafanya kazi yake vizuri ambayo inategemewa na Watanzania wengi, mchakato huu umefika mahali pazuri sana. Mwaka 2015 Serikali ya Awamu ya Nne, kazi kubwa Serikali hiyo ilifanya ni kutunga sheria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwaambie Waheshimiwa Wabunge, jamani mapambano haya ya dawa za kulevya ni ya kwetu Watanzania wote, yasichague mtu yeyote. Na mimi kwa dhati ya moyo wangu, nawaomba Waheshimiwa Wabunge, kila atakayeamua kupambana na jambo hili tuungane mkono pamoja kwani ni ajenda ya kitaifa inayotuhusu Watanzania wote. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, inaoneshwa hapa ni kama vile Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli na Serikali yake hawana nia ya dhati ya jambo hili, hapana. Mheshimiwa dada yangu Mheshimiwa Halima, namheshimu, amesema hapa kitu ambacho siyo sahihi.
Waheshimiwa Wabunge, bajeti kwa ajili ya kutengeneza mamlaka hii mmeipitisha. Tumepitisha bajeti ya shilingi bilioni 2.3 kwa ajili ya kwenda kuunda mamlaka hii itakayopambana na dawa za kulevya nchini. Bajeti hiyo hatujaweka fedha ya maendeleo, kwa sababu unawapaje hawa watu fedha ya maendeleo? Unataka wakatekeleze nini…
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: ...badala ya kuwapa OC ya kwenda kufanya kazi…
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo bajeti, hiyo tumeitenga na tunategemea bajeti hiyo itaenda kufanya kazi.
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikuambie kwamba chini ya Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli tayari kanuni za sheria hizi tumeshazikamilisha na zipo tayari. Chini ya Serikali ya Dkt. John Pombe Magufuli, muundo wa mamlaka hii ya kupambana na dawa za kulevya iko tayari. Muundo umeshakamilika. (Makofi)
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachosubiri ni uteuzi wa Kamishna ambaye ataongoza mamlaka hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nieleweke, kuteua Kamishna ambaye atashughulika na jambo hili siyo jambo la lelemama. Ni lazima atafutwe mtu mwenye maadili anayeweza…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niseme. Narudia kusema, ni lazima atafutwe kiongozi anayeweza kuwa na maadili ya kutosha ya kupambana na tatizo hili…
T A A R I F A....
WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba tu ulinde dakika zangu. Ninachokisema hapa sitaki kusema kwamba Mheshimiwa Halima Mdee haja-quote taarifa ya Kamati. Nilichokuwa nalieleza Bunge hili, sisi kama Serikali, wakati tunaelekea kuunda mamlaka mpya yenye nguvu ya kudhibiti, hatukuona haja ya kuweka fedha ya mradi wa maendeleo. Tunaipaje Tume fedha za maendeleo ambapo sisi tumeweka shilingi bilioni mbili kwa ajili ya OC ya kuratibu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninachotaka kusema, taarifa ya Kamati hiyo anayoi-quote Mheshimiwa Halima, lakini mimi kama Waziri mwenye dhamana, najua Tume hii wakati inajibadilisha kwenda Mamlaka, tumeitengea shilingi bilioni 2.5 ili iweze kutengeneza Mamlaka na kufanya kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waheshimiwa Wabunge tuelewane. Narudia kusema, ninampongeza Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuonesha nia ya dhati…
Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli alisema wakati anafungua Bunge hili, alionesha nia ya dhati ya kupambana na dawa za kulevya katika nchi yetu ya Tanzania.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninasema ndiyo maana hii Sheria ya Namba 5 ya mwaka 2015, yale yote ambayo yanatakiwa yafanyike kwa mujibu wa sheria yameshatekelezwa yote. Bajeti kwa ajili ya mamlaka hii mpya itapangwa katika bajeti ya mwaka 2017/2018 na hiyo ndio nia ya Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. (Makofi/Kelele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema mapambano dhidi ya dawa za kulevya ni ya Watanzania wote na sisi wote tuungane pamoja, tuhakikishe kwamba vita hii tunakwenda nayo pamoja. (Makofi/Kelele)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwenye tatizo la UKIMWI katika nchi yetu ya Tanzania. Tumejipanga. Tumegundua kwamba ufadhili wa fedha za UKIMWI unazidi kwenda chini. Tumepitisha sheria mwaka 2016 ya kuanzisha Mfuko wa UKIMWI; na mfuko ule Serikali tumeutengengea shilingi bilioni 1.5 mpaka sasa. Naomba Waheshimiwa Wabunge mwamini Serikali ina nia ya dhati ya kuwakomboa Watanzania dhidi ya mapambano pia ya tatizo la UKIMWI katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, dawa za kulevya hazikubaliki na tutaendelea kuratibu na kupambana na dawa hizi tukiongozwa na Rais wetu, Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.