Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Stella Ikupa Alex

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. STELLA I. ALEX: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Kwa sababu ya muda nitaenda haraka haraka. Nikiwa kama kijana, napenda na mimi niweze kuongelea kwa uchache kuhusiana na dawa za kulevya kwa sababu ni janga ambalo linaharibu ama linapoteza nguvu kazi ya Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja niiombe sana Serikali kuitengea hii Tume ya Udhibiti wa Dawa za Kulevya fedha za kutosha na kuipelekea ili iweze kufanya kazi yake vizuri kama inavyotakiwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niongelee suala la ulinzi kwenye mipaka yetu kwa sababu tunaona kwenye airport nyingi imeshadhibitiwa lakini bado kwenye mipaka yetu ulinzi hauko vizuri. Kwa hiyo, niiombe Serikali iimarishe ulinzi kwenye mipaka ya nchi yetu ikiwa ni pamoja na kupeleka vifaa vya kitaalamu ambavyo vitaweza ku-detect dawa hizi za kulevya kwa wale wanaopita kwenye hii mipaka yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, moja kwa moja niongelee suala la elimu hasa Bodi ya Mikopo ya Elimu ya Juu. Kwanza kabisa, napenda niishukuru Serikali kwa kuweka ulemevu kama ni kigezo kimojawapo cha utoaji wa mikopo ya elimu ya juu. Naomba nitoe mapendekezo yafuatayo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa watu wenye ulemavu kwa kuwa idadi ya watu wenye ulemavu ambao wanapata fursa ya kufika chuoni ni ndogo sana, hivyo niombe kabisa Serikali isitoe kama mikopo kwa watu wenye ulemavu bali itolewe kama ruzuku.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia niombe kwa habari ya elimu ya kuanzia shule ya awali mpaka kidato cha sita. Watu wenye ulemavu ambao wanapata fursa ya kwenda shule ni wachache sana na ipo ndani ya uwezo wa Serikali kuwapa elimu bure watoto wenye ulemavu kuanzia darasa la kwanza ama kindergarten mpaka kidato cha sita. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba niende ukurasa wa 45 wa Taarifa ya Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii. Ukurasa huu unaongelea mkakati wa kuongeza walimu. Naomba ninukuu; “Kamati imebaini kuwa, kuna upungufu wa walimu hususani wa masomo ya sayansi na hisabati, hali ambayo imekuwa ikiathiri kiwango cha elimu nchini. Kutokana na hali hiyo, Kamati inaazimia Wizara iandae mkakati maalum wa kuendeleza walimu wa masomo ya sayansi na hisabati ili kukabiliana na changamoto ya muda mrefu ya uhaba wa wataalamu hao katika masomo hayo.”
Mheshimiwa Mwenyikiti, mimi napendekeza kwamba kifungu hiki kisomeke kwamba; “Kamati imebaini kuwa kuna upungufu wa walimu hususani wa masomo ya sayansi, hisabati na elimu maalum hali ambayo imekuwa ikiathiri kiwango cha elimu nchini. Kutokana na hali hiyo, Kamati inaazimia Wizara iandae mkakati maalum wa kuendeleza walimu wa masomo ya sayansi, hisabati na elimu maalum ili kukabiliana na changamoto ya muda mrefu ya uhaba wa wataalamu hao katika masomo hayo.”
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa haraka haraka, naiomba Kamati ya Huduma na Maendeleo ya Jamii ijitahidi kutembelea shule…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante Mheshimiwa Ikupa.