Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Hawa Abdulrahiman Ghasia

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Mtwara Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. HAWA A. GHASIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Nami ningependa kuchangia hoja. Niwapongeze watoa hoja wote na hivyo nianze kwa kuunga mkono hoja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la kwanza ningependa kuzungumzia suala la elimu na hasa masuala mazima ya ufaulu. Katika wilaya nyingi na mikoa mingi ambapo matokeo ya kidato cha pili na kidato cha nne yamekuwa siyo ya kuridhisha, asilimia kubwa uamuzi au hatua zilizochukuliwa ni kushusha vyeo walimu wakuu au wakuu wa shule. Mimi sidhani kama mwalimu peke yake anaweza akawa ndiyo sababu ya shule kufeli au kufaulu. Mimi napenda nishauri katika zile Wilaya ambazo kila mtihani uliofanywa zimekuwa za mwisho hebu tufanye utafiti wa kina tujue kwa nini wilaya hizo zimefanya vibaya. Haiwezekani kwenye Mkoa wangu Wilaya moja hiyo hiyo matokeo ya kidato cha nne wa mwisho, matokeo ya darasa la saba ya mwisho halafu tuone hatua ya kuchukua ni kushusha vyeo tu walimu, sidhani! Naomba tufanye tathmini ya kina ili tujue tatizo tuweze kuwasaidia na zile Wilaya na zenyewe zifanye vizuri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nirudi kwenye sekta ya afya na nianze kuzungumzia suala la uchache wa watumishi katika sekta ya afya. Kwa kweli hali ni mbaya, ukienda katika vituo vyetu vingi vya afya, hospitali majengo ni yanaridhisha, unakuta hospitali zetu sasa hivi nyingi ni safi, madaktari wanajitahidi hata wauguzi, kauli zinaridhisha lakini uchache wao unawaangusha. Katika baadhi ya Wilaya tunashindwa kutoa baadhi ya huduma kama upasuaji, kufungua baadhi ya zahanati, kwa sababu ya uchache wa watumishi. Niombe Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma, wakati tukiendelea na uhakiki basi kama tulivyofanya kwa sekta ya elimu na sekta ya afya nayo tuiangalie, hali ni mbaya hasa katika Mkoa wangu wa Mtwara ambao ninaufahamu. Nina vituo vyangu vya afya ambavyo vimeshindwa kuanza huduma za upasuaji kwa sababu hatuna watumishi wa kuweza kutoa huduma hizo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la vifo vya akina mama limezungumziwa sana hasa kutokana na changamoto za uzazi. Mojawapo ikiwa kuzalishwa na watumishi ambao kwa kweli hawana utaalamu. Niombe hivi vituo vya afya, mlishaanza kuvifanyia tathmini na kuvipa madaraja, zoezi hili likamilike nchi nzima ili vile vituo ambavyo havina uwezo wa kuzalisha akina mama waambiwe kwamba siku zako zikifika pale huwezi kusaidiwa, wajue ili ajiandae, ikiwezekana aende akakae karibu na eneo ambalo ataweza kusaidiwa. Kwa sababu kama atahitaji damu wakati wa kujifungua, kama atahitaji operation wakati wa kujifungua ndiyo kusema kama atakuwa eneo ambapo hakuna huduma hizi huyo mama ndiyo tumeshampa cheti cha kifo.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nilitaka kulichangia ni tafiti zinaonesha maeneo ambayo wanaume wanafanyiwa tohara maambukizi ya UKIMWI yako chini sana kuliko maeneo ambayo hayafanyiwi tohara ambapo maambukizi ya UKIMWI yako juu sana, na hivyo hivyo maeneo ambayo tohara haifanyiki maambukizi ya kansa ya shingo ya kizazi pia yako juu. Niiombe Wizara ya Afya hili suala la tohara kwa wanaume lisiwe la hiari liwe la lazima. Kwa sababu kama tafiti zote zinatuambia maeneo mengine wanaume ambao hawajatahiriwa maambukuzi wako zaidi ya asilimia 21 kuliko wale ambao wametahiriwa. Kwa nini tusiseme ni lazima? (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninawaomba, ile Mikoa ambayo wanatahiriwa, lile tendo wasiite suna, maana yake mtu anasema anakwenda kutahiriwa unaita suna, kitu kama ni suna maana yake siyo lazima, niwaombe kwa wale wanaotahiriwa tuseme faradhi ili kila mtu ahamasike. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jana wote tulikuwa Morena, tumeambiwa haya, siyo kama nimeyatoa kichwani, ni taarifa zilizotolewa na Shirika la Afya Duniani, Wizara ya Afya wanazo. Tupeleke taarifa sahihi, kuhusu suala la tohara kwa wanaume. Tutawanusuru akina mama wetu tutapunguza maambukizi ya virusi vya UKIMWI.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaiomba Wizara ya Afya, tunazo hospitali zetu za Kanda, Kanda ya Kaskazini tunayo KCMC, Kanda ya Magharibi au ya Ziwa tunayo Bugando na Kanda ya Nyanda za Juu Kusini tunayo Hospitali ya kule Mbeya, Kanda ya Kusini peke yake ndiyo imebaki ambayo haina Hospitali ya Rufaa ya Kanda, ujenzi umeanza lakini ni wa kusuasua. Nikuombe Mheshimiwa Waziri, tusaidie katika hilo, gharama ya kumsaidia mgonjwa mmoja kuja hospitali kutibiwa kwa kumsafirisha kwa ndege kutoka Mtwara, Precision Air inafika mpaka shilingi milioni 12. Mimi mwenyewe nimesafirisha kijana ambaye alipata ajali ya gari kwa shilingi milioni nane kwa ATC, kutoka Mtwara kwenda Dar es Salaam, ni wangapi wanaweza gharama hizo? Kwa hiyo, tuwaombe wenzetu wa Wizara ya Afya mkamilishe ujenzi wa Hospitali ya Kanda ya Kusini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazo Hospitali za Rufaa za Mikoa, naomba tuzifanye ziwe kweli Hospitali za Rufaa za Mikoa. Unakwenda Hospitali ya Rufaa ya Mkoa unakuta ina oxygen machine moja, wakija wagonjwa wawili mmoja anakuwa kwenye mashine mwingine hata kama anahitaji ile huduma hawezi kupata. Tuombe muweke MRI, muweke CT Scan, X-ray machines, angalau hata kwa Kanda. Kwa sababu tunazungumzia suala la ugonjwa wa kansa ya kizazi ndiyo ugonjwa ambao unaua sana akina mama, lakini huduma hiyo inapatikana hospitali ya Ocean Road peke yake, na ugonjwa huo mgonjwa akiwahi unatibika. Kwa hiyo, niombe basi huduma hii ipelekwe angalau kwenye Kanda. Hivi ni wangapi wenye uwezo, unatoka Rukwa, unatoka Kagera kwenda Dar es Salaam na kila dozi inapokuja uende, kwa kweli, ndiyo kule utatibiwa bure, lakini mara nyingi gharama za kwenda kule huwa wanajigharamia. Kwa hiyo niombe kwa kweli hili lifanyiwe kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala hili la kuweka vifaa MRI, CT Scan na X ray machines siyo lazima Serikali ifanye, tunaelewa kwamba Serikali haina uwezo wa kugharamia kila kitu na tunaona unapokwenda kwenye hospitali pale Muhimbili kama mashine haifanyi kazi unaambiwa ukapime nje, kwa nini msiingie ubia mkafanya PPP, hizo mashine wakaja kuziweka kwenye hospitali zetu?
Mheshimiwa Mwenyekiti, niwaombe Wizara ya Afya mshirikiane muingie ubia, vitu kama MRI, CT Scan, X-Ray, kila baada ya miaka mitano teknolojia inabadilika na hatuwezi kwenda na kasi hiyo, lakini akiweka mtu binafsi ikipita muda wake unamwambia hamisha leta nyingine inayoendana na teknolojia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.