Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Felister Aloyce Bura

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Masuala ya UKIMWI na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Huduma na Maendeleo ya Jamii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. FELISTER A. BURA: Mheshimiwa Mwenyekiti, namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kunipa nafasi ya kusimama katika Bunge lako Tukufu, lakini nikushukuru wewe pia kwa kunipa nafasi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nipongeze Kamati zote mbili kwa kazi nzuri walizofanya. Wamefanya kazi nzuri kwa muda mfupi sana, lakini wamefanya kazi kubwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunapopitisha bajeti hapa kila Wizara tunapitisha bajeti zake tukiamini kwamba fedha zitakwenda kwenye Wizara hizo kwa wakati muafaka. Lakini kwa Taarifa ya Kamati ya Maendeleo ya Jamii, nimesikitika jinsi mtiririko wa fedha ulivyo na hasa katika Wizara ya Afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania milioni 45 tunategemea kuhudumiwa na Wizara ya Afya kuhusu huduma ya afya. Wazee wanaitegemea Wizara ya Afya, wanawake, watoto, vijana, kwa hiyo, milioni 45 fedha zinapopelekwa asilimia 21 kwa muda wa miezi sita ina maana Watanzania hawana pa kukimbilia na hasa wale ndugu zangu ambao wanaishi vijijini na hawana uwezo wa kujitibu na hawana bima ya afya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasikitika kweli ninaposema hili kwa sababu tunapata matatizo tunapokwenda vijijini, unamkuta mtu anaumwa na anaumwa kweli kweli na hana fedha, na zahanati au kituo cha afya jirani yake hakuna dawa. Kwa hiyo, mzigo unakuwa kwa Mbunge ambaye amekwenda kutembelea pale au mzigo unakuwa kwa Diwani aliyeko eneo lile.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niombe sana kwamba tunapopitisha bajeti hapa basi fedha ziende kwa wakati. Utakuta mwezi wa tano au wa sita ndipo Wizara ya Fedha inapeleka fedha katika Wizara mbalimbali na mwisho wa mwaka unapofika fedha zinarudi nyingi tu Wizara ya Fedha kwa sababu fedha zimepelekwa muda umekwisha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna deni la MSD tangu Bunge lililopita; tangu mwaka wa jana wakati tunapitisha bajeti tuliomba sana kwamba deni la MSD lilipwe ili MSD wawe na uwezo wa kununua dawa na kuzisambaza mikoani, lakini hili deni linapungua kidogo kidogo mno.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimuombe Waziri wa Fedha afya za watanzania ni muhimu kwa hiyo, deni la MSD lilipwe ili MSD wawe na uwezo wa kuagiza dawa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia na Watoto na Wazee fedha za maendeleo wamepelekewa asilimia 21, nimeshangaa kweli. Mwaka jana tulipitisha bajeti tukiomba fedha kwa ajili ya kukarabati Hospitali ya Rufaa ya Mirembe; wanaotibiwa pale wana ugonjwa wa afya ya akili, wameshawapiga manesi na madaktari wengi tu pale, lakini mpaka leo hospitali ile haijakarabatiwa. Hospitali ile ilijengwa tangu mwaka 1926, kwa hiyo, miundombinu ya hospitali ile imechakaa kweli; wauguzi na madaktari hawatoshi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilitegemea kabla ya mwezi wa kumi na mbili Wizara itakuwa imepeleka watumishi wa kutosha, lakini mpaka leo watumishi ni wale wale, wauguzi wakiingia asubuhi ni mpaka jioni saa moja ndipo wabadilishane na posho za overtime hazilipwi kwa wakati. Na mimi simlaumu Mheshimiwa Ummy kwa sababu hana fedha. Posho za wauguzi hazilipwi, fedha za safari na za likizo hazilipwi kwasababu Wizara haina fedha. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jamani tuwakumbuke Wizara ya Afya. Naona tunawatetea sana walimu lakini hata wauguzi na waganga hawana watetezi, watetezi wao ni sisi. Pamoja na walimu, wauguzi na waganga nao wanateseka; hawana nyumba, overtime na fedha za likizo hazilipwi kwa wakati, na wao watizamwe kwa jicho la huruma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Rais John Pombe Magufuli alipomteua mdogo wangu Ummy Mwalimu kuwa Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Watoto na Wazee alijua umahiri wake katika kazi, na mimi nampenda kwa sababu anafanya kazi nzuri. Mheshimiwa Ummy nakupenda kwa sababu unafanya kazi nzuri, lakini nina tatizo moja, najua huna fedha lakini takwimu ambazo zimeoneshwa hivi karibuni zinaonesha kwamba kati ya wanawake wajawazito 100,000 wanawake 556 wanapoteza maisha.
Mheshimiwa Waziri ninajua una uwezo wa kuja na mkakati madhubuti kabisa kuhakikisha kwamba hivi vifo vinapungua. Tusiwafanye watoto wetu wasichana wakaogopa kuzaa kutokana na vifo. Ninaomba sasa leo ukijibu hoja za Wabunge useme mkakati ambao umeandaa kwa ajili ya kupunguza vifo vya wanawake na hata vifo vya watoto. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali inahamia Dodoma lakini kwenye Taarifa ya Kamati inaonesha kwamba Hospitali za Rufaa tulizonazo hazina watumishi wa kutosha; Hospitali ya Benjamin Mkapa kati ya watumishi 751 wapo 51 tu. Kama uhakiki wa watumishi umekamilika basi waajiriwe; hao wanaotoka Dar es Salaam wanaiacha Muhimbili kule wanaacha Hospitali za Rufaa kule Dar es Salaam wanakuja dodoma, tuna hospitali moja tu hapa ya General. Lakini Hospitali ya Benjamin Mkapa ambayo ina vifaa vya kutosha vya kazi, hakuna watumishi, watumishi 700 wanahitajika pale na wale wanatibu wagonjwa wa ndani na wa nje; wagonjwa wa Dodoma na wa nje ya Dodoma.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakuomba kama uhakiki umeshamalizika basi waajiriwe wafanyakazi wa kutosha pale Benjamin Mkapa, Hospitali ya Mirembe na Hospitali yetu ya Mkoa ili kuhakikisha kwamba huduma inayoendelea kutolewa pale iwe ya kuridhisha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niungane na msemaji, Mbunge aliyepita kuhusu ugonjwa wa kansa. Mimi kwa miaka mitatu nimepoteza ndugu watatu kwa ugonjwa wa kansa. Lakini hatujajua ugonjwa wa kansa unaambukizwaje, na tunatakiwa kujikinga vipi, na unasambaa au hausambai? Si mimi tu, wako wananchi wengi wa Tanzania ambao wanatamani kupata elimu kuhusu ugonjwa wa kansa. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kusema habari ya viroba vilivyojaa madukani. Vijana wetu hasa waendesha bodaboda asubuhi anapiga viroba vitatu na ndio maana ajali za pikipiki haziishi, viroba sasa viuzwe kwenye bar, tuache kuviuza madukani. Kwa sababu wengine wataogopa kuingia kwenye bar. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze pia kuhusu elimu. Sisi Kamati yetu ya PAC tulitembelea Chuo cha Ufundi Arusha; tuliona kazi kubwa ambayo inafanywa na kile chuo, wamebuni mambo mengi sana, wametengeneza mashine za kilimo cha kumwagilia, wamechukua kiwanda cha kuzalisha umeme kule Kikuletwa Wilaya ya Hai lakini hawana fedha. Pamoja na juhudi kubwa na kuwafundisha vijana namna ya kujitegemea, wavulana kwa wasichana wanajifunza mambo mengi sana pale lakini hawana fedha. Ninakuomba Waziri wa Elimu kiangalie kile chuo kwa jicho la huruma sana. Pamoja na kwamba tuna VETA lakini wanafunzi wanaweza wakatoka VETA wakaenda wakajifunza mambo makubwa sana pale Arusha Technical College.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kuna malalamiko kwamba wanafunzi ambao hawastahili kupata mikopo na wanapata mikopo wanaweza wakarudishwa majumbani. Ninaomba hili Waziri wa Elimu aliweke wazi kwa sababu wanafunzi wetu wapo wengi vyuoni, lakini hawajui hatima yao. Tumeambiwa uhakiki bado unaendelea, hatujui uhakiki utakamilika lini, na je, kama watapatikana ambao hawastahili kupata mikopo itakuwaje, watarudishwa majumbani au Serikali itaendelea kuwahurumia na wakaendelea na masomo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, wako watoto wa maskini wengi tu,wengine walikuwa na wafadhili wakasoma shule ya sekondari private school lakini anapoanza chuo mfadhili anamuacha. Mwingine baba au mama alikuwa na uwezo kipindi hicho lakini amebaki yatima hawezi kulipa chuo kikuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Waziri aliangalie hilo kwa umakini na wanafunzi wasirudishwe kwa kuwa hawastahili kupata mikopo kwa kuwa wameshaanza kusoma. Naunga mkono hoja.