Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. January Yusuf Makamba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Bumbuli

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA MAKAMU WA RAIS, MUUNGANO NA MAZINGIRA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa fursa na mimi kuchangia hoja hii ya Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuipongeza Kamati na Mwenyekiti na Kamati nzima kwa kweli kwa ripoti nzuri waliyoiandika, kwa mapendekezo mazuri, lakini pia kwa ujumla kwa kazi nzuri wanayoifanya kuisadia Serikali wakati wote ambapo tumekuwa tunafanya nao. Kamati hii imesheheni wanamazingira, wanafahamu changamoto zilizopo na wamekuwa wanatusaidia vizuri sana katika kufanya kazi zetu. Nawapongeza na nawashukuru sana. (Makofi)
Waheshimiwa Wabunge, kwanza tumepokea mapendekezo ya Kamati, ni mazuri na mimi nayaunga mkono, lakini pia tumesikia michango ya Wabunge kuhusu masuala ya mazingira. Wabunge wote waliochangia kuhusu eneo hili wamesema hali ya mazingira nchini ni mbaya na mimi nataka niseme kwamba hali ya mazingira nchini ni mbaya sana, si tu ni mbaya, ni mbaya sana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, maji katika nchi yetu ni rasilimali kubwa, ukitazama mito, vijito, mabwawa, chemichemi, kila mwaka unaopita tunapata changamoto ya upatikanaji wa maji, kwenye ardhi rutuba inapungua, matumizi yasiyozingatia kanuni za masingira, misitu inateketea, mvua hazitabiriki.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kila mwaka hapa tunakutana kupanga maendeleo na kupanga maendeleo na kupanga fedha za maendeleo. Ile shughuli za kupanga maendeleo na kupanga fedha za maendeleo itakuwa haina maana kabisa kama hatutazingatia umuhimu wa kuhifadhi mazingira kwenye sekta zote. Ukitaja kilimo, hakiwezekani kuwa na manufaa kama hakizingatii mazingira. Afya, elimu, maji, utalii, hakuna sekta isiyoguswa na mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, maendeleo ya nchi yetu yana mahusiano moja kwa moja na hifadhi ya mazingira lakini pia hata uwezeshwaji wa wanawake (women empowerment) na yenyewe moja kwa moja ina uhusinano wa hifadhi ya mazingira. Tunapozungumza ukosekanaji wa maji unaotokana na changamoto ya mabadiliko ya tabia nchi wanaoathirika zaidi ni akina mama. Tunapozungumza suala la nishati ya kupikia, wanaotumia muda mrefu kwenda kutafuta kuni na hata wakati mwingine kuingia katika mazingira hatarishi huko porini ni akina mama na ndiyo maana sikushangaa kwamba Wabunge waliochangia kwa sehemu kubwa kwenye mazingira ni akina mama, Mheshimiwa Leah Komanya, Mheshimiwa dada yangu mpendwa sana Hawa Bananga, Dkt. Christine Ishengoma, Mama Mwanne Mchemba kwa sababu ni jambo linalowagusa akina mama sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kwamba tumepokea mapendekezo na tumeyakubali na tunapenda Bunge litusaidie kwa sababu Bunge ndilo linalogawa fedha, Bunge ndilo linaloamua fedha kiasi gani ziende katika maeneo gani. Waheshimiwa Wabunge, mkiamua ninyi kwamba Mfuko wa Mazingira katika mwaka ujao wa fedha uwe na shilingi bilioni 200 badala ya sifuri mnaweza kufanya hivyo. Sisi tulipanga katika bajeti iliyopita, tulijadiliana ndani ya Serikali lakini na hapa Bungeni kuhusu uwezekano wa mfuko wetu kupata vyanzo vya moja kwa moja kwenye tozo mbalimbali ili uweze kuwa na fedha nyingi zaidi ili mimi kama Waziri mwenye dhamana ya Mazingira nikipita kwenye majimbo nikiona unahitaji miche 10,000 niwe na uwezo wa kukupatia miche 10,000. Nikiona unahitaji kwa kupitia Mfuko wa Mazingira, vyanzo vya maji vitunzwe kwenye jimbo tuweze kufanya hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo napenda nirudishe changamoto hii kwa Waheshimiwa Wabunge kwamba tunaelekea kwenye bajeti na kama kweli tunaamini mazingira ni muhimu basi pale tuoneshe kwa vitendo kwamba Mfuko wa Mazingira upate vyanzo vyake vya moja kwa moja kama ambavyo mfuko wa barabara unapata vyanzo moja kwa moja, kama ambavyo Mfuko wa Nishati unapata vyanzo moja kwa moja na mifuko mingineyo, mtakuwa mmetusaidia na mtakuwa mmeisaidia nchi yetu sana. Kwa hiyo ndugu zangu bila fedha hifadhi ya mazingira ni jukumu la moja kwa moja la msingi la Serikali. Sekta binafsi inaweza kushiriki kwenye hifadhi ya mazingira lakini hatuwezi kubinafsisha hifadhi ya mazingira. Lazima sisi kama Bunge tupange fedha ili zitumike huko.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge wengi wamezungumzia kuhusu tatizo la mkaa. Tumeamua sisi kama Serikali kwa kushirikiana na wenzetu wa Wizara ya Maliasili na Utalii kukabiliana na changamoto hii. Sasa hivi tutaleta mapendekezo; tozo kwenye kila gunia la mkaa ni shilingi 16,000 za TFS; labda Halmashauri inaweza na yenyewe inaweza ikacharge shilingi 2,000. Tunataka tuongeze kodi kwenye mkaa ili tuweze kupata fedha nyingi zaidi na tutapenda fedha hizo ziingie kwenye mfuko wa mazingira. Tungependa Wabunge mtusaidie tuamue na Waziri wa Fedha yuko na mazungumzo yanaendelea Serikalini; kwamba zile teknolojia ambazo zinasaidia uhifadhi wa mazingira basi zisamehewe kodi ili gesi iwe bei rahisi, majiko ya gesi yawe bei rahisi ili wananchi wa kawaida waweze kuyamudu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mradi wa maji Simiyu, Mheshimiwa Naibu Waziri amezungumza vizuri ila nataka niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba moja ya nyenzo ambazo tumeamua kuzichukua kama Ofisi ya Makamu wa Rais ni kutumia hii mifuko mikubwa ya kifedha ya kimataifa kupata fedha kwa ajili ya kukabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi lakini fedha hizo kuziingiza kwenye miradi ya maendeleo. Kwa mfano, kwa uhakika kabisa Mkoa wa Simiyu utapata shilingi bilioni 200 kwa ajili ya upatikanaji wa maji kutokana na Mfuko wa Mazingira wa Dunia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunataka kwenye maeneo yote yenye ukame kama Serikali tujenge hoja kwamba ukame ule unatokana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Kwa hiyo, fedha inazosaidiwa Tanzania kwenye kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi tuzipeleke kwenye maeneo kama hifadhi ya maji, kilimo cha umwagiliaji na kadhalika. Tukifanikiwa katika mwezi huu wa tatu unaokuja kupata fedha hizo shilingi bilioni 200 itafungua mlango wa kupata dola milioni 800 kwa ajili ya maji katika nchi yetu. Huu ni mradi ambao tunaufatilia kama Ofisi ya Makamu wa Rais na tutafanikiwa, tutakapofanikiwa basi wetu tutakuwa tumewapunguzia kero.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu ukataji wa miti na kilimo cha kuhamahama, nimesikia nilipata nafasi ya kufanya ziara ya mikoa kumi katika nchi yetu na baada ya Bunge hili tutazunguka katika mikoa yote siyo tu kukagua hali ya uharibifu wa mazingira bali kuchukua hatua wakati ule ule tutakapoona kuna uharibifu wa mazingira.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kule kwenye tumbaku Tabora, tumeamua sasa kupiga marufuku matumizi ya yale mabani ya zamani ya kienyeji ambayo yanatumia magogo mengi na kupelekea ukataji wa miti na misitu ya nchi yetu. Ningependa Bunge lako liwe ni Bunge la wanamazingira. Naomba tusaidiane sana, Waheshimiwa Wabunge mkiishika ajenda ya mazingira tutatoka, pamoja na kwamba inawezekana athari za uharibifu wa mazingira zisionekane papo kwa papo lakini madhara yake huko mbele yatakuwa maisha magumu sana kwa Watanzania. Kwa hiyo, tuna uwezo wa kuweka historia kama Bunge la kwanza lililoweka fedha nyingi zaidi kwenye hifadhi ya mazingira na kuyaokoa mazingira ya nchi yetu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuja hapa kila mwaka tunaomba fedha nyingi kwenye bajeti ya maji, lakini unaweza kuomba fedha na kujenga miundombinu ya maji kama hatukupanga fedha za kuhifadhi vyanzo vya maji tutakuwa tumepoteza fedha kwenye kujenga mabomba ya maji wakati kule maji yanakotoka hatujayahifadhi.
Kwa hiyo, katika shughuli zote ambazo tunazipanga katika Bunge hili mazingira ndiyo msingi wake na Serikali tunaishukuru sana Kamati kwamba jambo hili imeliona na inalishughulikia, tunategemea sasa spirit hii ya Kamati basi Bunge zima na yenyewe italichukua ili itakapofika wakati wa bajeti basi wote tuzungumze kwa kauli na sauti moja ili tuweze kuisaidia nchi yetu.(Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo nashukuru sana kwa fursa hii, naishukuru tena Kamati na ninawashukuru wote mliochangia kwenye hoja hii.