Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Zainab Athuman Katimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. ZAINAB A. KATIMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii ya kuweza kuchangia katika hoja iliyopo mezani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kuleta uchumi wa viwanda kuna mambo ya msingi ambayo Serikali inabidi iendelee kuweka msisitizo. Katika uchumi wa viwanda ni lazima Serikali iweze kuangalia kwamba kuna upatikanaji wa malighafi. Tunahitaji malighafi ya kutosha ili kuweza kulisha viwanda vyetu. Katika malighafi tunazungumzia upatikanaji. Kukiwa kuna viwanda lakini hakuna upatikanaji wa malighafi ya kutosha kulisha viwanda vyetu basi mwisho wa siku tunakuja kuona viwanda vyetu vinafungwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, labda tu nitoe mfano, viwanda vyetu vya sukari hapo awali vilikuwa vinafungwa kwa msimu fulani kwa sababu hakukuwa na malighafi ya sukari ambayo ingeweza kuzalisha sukari. Kwa hiyo, Serikali inabidi iweke msisitizo katika upatikanaji wa malighafi hizi. Na hata tukiangalia nchi ambazo ziliendelea na zimeendelea katika uchumi wa viwanda ilianza kwanza agrarian revolution yaani mapinduzi ya kilimo, yalianza yakaweza kuleta industrial revolution ambayo ni mapinduzi ya viwanda. Kwa hiyo, naomba Serikali iweze kuendeleza jitihada zake inazozifanya. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini si hivyo tu, tunahitaji malighafi ambazo ni za bei nafuu. Tukiwa tuna viwanda lakini malighafi zinazopatikana nchini ni za bei ya juu na zinatumia cost of production kubwa kuliko zinazotoka nje ya nchi, mwisho wa siku tunaona kwamba hata gharama ya uzalishaji wa mali ambazo zitazalishwa ndani ya nchi zitakuwa zina gharama ya juu zaidi kuliko mali zitakazoletwa kutoka nje ya nchi.
Kwa hiyo, ningependa pia Serikali iendelee na jitihada zake inazofanya kuhakikisha kwamba malighafi zinapatikana kwa bei nafuu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini si hivyo tu, tunahitaji ubora wa malighafi ambao utatokana na ubora tuseme kwa mfano wa mbegu. Kwamfano kama tunazungumzia viwanda vya kutengeneza, tuseme juisi, inahitaji kwamba kuwe kuna ubora wa hata yale matunda yanayopatikana Tanzania. Kwa hiyo je, mbegu zinazotolewa na mbegu zinazotumika zina ubora wa kuzalisha kwa kiwango kizuri cha kuweza kulisha viwanda vyetu? Hilo ni suala lingine ambalo Serikali inabidi iendelee kufanya jitihada zaidi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la mbolea, kuna suala zima la teknolojia inayotumika, je, teknolojia inayotumika Tanzania ni ya kizamani au inaendana na wakati, kwa sababu kutumia teknolojia ya zamani kunaleta gharama kubwa zaidi ya uzalishaji na mwisho wa siku hata mali zetu na viwanda vyetu vinakuwa haviendelei vizuri.
Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda pia kuzungumzia katika suala zima la upatikanaji wa mitaji. Upatikanaji wa mitaji au tuseme mikopo lakini upatikanaji wa mitaji hii kwa riba nafuu. Upatikanaji wa mikopo katika taasisi zetu za kibenki tujiulize, je, unaweza kuhimili uchumi wa viwanda? Je, financial institutions zinaweza kutoa mikopo kwa ajili ya wawekezaji wetu wa ndani kuweza kuwekeza katika viwanda vyetu? Na hiyo mikopo inayotoka na hizo fedha zinazotoka kutoka kwenye taasisi zetu riba zake zikoje, kwa sababu kuna taasisi za kifedha ambazo zinatoa mikopo, zinatoa fedha kwa riba hadi asilimia 25, je, huyu mwekezaji ataweza kweli kufanya biashara zake, ataweza kweli kuhimili matakwa ya kuendesha kiwanda chake na kikaweza kufanikiwa.
Kwa hiyo mimi napenda kuiomba Serikali kwamba ikae na wadau mbalimbali, viwanda na biashara na taasisi za kibenki, ili iweze kusaidia mchakato utakaoweza sisi kutunga sheria itakayoweza kuweka ukomo wa viwango hivi vya riba kwenye mikopo katika taasisi za kifedha. Kwa sababu tukisema tu tunaacha hivi ilivyo, taasisi za kifedha zinaweka riba za hali ya juu na mimi kama kijana najua vijana wenzangu wanajishughulisha katika shughuli za ujasiriamali na wanahitaji hizi fedha, wanakwenda kwenye taasisi za kifedha na wanapata fedha kwa riba kubwa sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja.