Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Anatropia Lwehikila Theonest

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru. Nichukue fursa hii kupongeza uamuzi uliouchukua, kiukweli tunaona mambo mengi yanaenda ndivyo sivyo napongeza sana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, narudi kwenye hotuba yetu ya Kamati, kwanza, na-declare interest ni Mjumbe wa Kamati ya Viwanda, Biashara na Mazingira, kwa hiyo mambo nitakayoyaongea hapa nayajua hasa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mujibu wa taarifa ya Wizara mpaka tunavyoongea tarehe 31 Januari, 2017 tukiwa kwenye robo ya tatu, Wizara imepokea fedha ya maendeleo kutoka kwenye bajeti ya bilioni 42, imepokea bilioni 7.6 sawa na asilimia 18.6. Naongea hayo tukiwa tumebakiza theluthi moja tu ya kumaliza mwaka, Wizara imepokea pesa ya maendeleo shilingi bilioni 7.6 nimesema hapa nimemwambia Waziri wa Viwanda mimi leo nitakutetea, una haki ya kuwa unapiga propaganda kwa sababu kiukweli hakuna chochote unachoweza kufanya bila kuwa na pesa, hakuna chochote unaweza kukifanya kwenye Wizara yako, kwenye idara zako bila kuwa na fund.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaongea nini kama tunakuja hapa tena na bajeti ambayo imekuwa na ongezeko la asilimia 16. Kipindi cha mwaka 2015/2016 pesa ya maendeleo ilikuwa ni bilioni 35, Watu mmekuja hapa mnajinasibu kwa Serikali iliyopita ilikuwa imelala, sasa tunaongeza bajeti, mmeongeza bajeti kwa asilimia 16, tumeenda kwenye bilioni 42, lakini tunavyoongea leo katika robo ya tatu ni bilioni 7.6 tu zimepelekwa kwenye Wizara kama fedha za maendeleo. Swali najiuliza, Are we still on the track? Bado tupo kwenye mpango wetu wa kuleta maendeleo?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu mtashangaa nitakachowaambia hiki. Mtukufu alivyokuwa katika ziara zake anahamasisha ujenzi wa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam na Hostel ambayo tunapongeza sana, alitoa ahadi kwamba atatoa shilingi bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa hostel za wanafunzi wa vyuo. Hatukatai, lakini tunarudi katika swali la msingi; hicho ndiyo tulichokuja Bungeni na kubajeti kwamba tunataka kufanya kama kipaumbele cha Taifa? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hizo hostel ambazo Mtukufu ameenda ametoa bilioni 10 kwa nyakati ambazo aliona zinafaa, lakini tupo tunaongelea Serikali ya viwanda, tunaongelea uchumi wa viwanda, bado wana bilioni 7.6 katika theluthi ya tatu. Tutamlaumu Waziri maskini ya Mungu, tutamsema sana lakini atafanya nini? Atasema nini? Turudi tuiulize Serikali bado tupo kwenye track? Bado tunataka kuendesha uchumi wa viwanda au zilikuwa ni story tu ambazo tulikuwa tunajinasibu kwa sababu ilikuwa Serikali mpya kwa hiyo tulitaka kuja na kitu kipya? Na kiukweli ndiyo hicho ninachokiona. Tulitaka kuja na kauli mbiu mpya japo kitu kilikuwa kile kile, business as usual na inaonekana katika money value. Tunaongelea mabadiliko yoyote, tunaongelea kutoka stage moja kwenda sehemu nyingine sasa tuko wapi? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo viwanda ambavyo Mheshimiwa Waziri anakuwa anafungua kila siku bahati mbaya sisi Kamati hatujui, ila kubwa zaidi ninachojua anafungua viwanda vya watu, viwanda vidogo vidogo vya watu binafsi kitu ambacho pia sio kibaya, lakini turudi kama Serikali yake sasa, Serikali inataka kufanya nini kama mkakati wa kuanzisha viwanda katika nchi yetu? (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, Katibu Mkuu alikuja kwenye kamati yetu anaeleza kile kilichoitwa mkakati wa kufufua viwanda. Akatueleza katika kipindi cha mwaka mmoja mwaka ambao tupo sasa 2017...
NAIBU WAZIRI WA AFYA, MAENDELEO YA JAMII, JINSIA, WAZEE NA WATOTO: kuhusu utaratibu, Kanuni ya 68...
MHE. ANATROPIA L. THEONEST: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru. Nitakariri vizuri, Mtukufu Rais wakati anazindua majengo ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam aliahidi atatoa bilioni 10 kwa ajili ya ujenzi wa chuo. Sasa swali linakuja? Track na mchezo wetu na wimbo wetu hapa Bungeni ilikuwa ni viwanda lakini katika theluthi ya tatu ya viwanda yenyewe, Wizara husika imepewa tu, bilioni 7.6 ikiwa chini ya pesa alizotoa Mtukufu Rais alivyoshawishiwa na maendeleo ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam. (Makofi/Kicheko)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitapenda Waziri anikumbushe vizuri, kama bado tuko kwenye wimbo ule ule au tumebadilisha kauli na sasa tuko kwenye kitu kingine kama sera yetu ya Awamu ya Tano. Nimekwenda kwenye mkakati wa viwanda aliowasilisha Katibu Mkuu kwenye Wizara yetu ni kwamba; kwa Mwaka huu wa Fedha na pesa waliyoipata wameweza kufufua kiwanda kimoja tu, kwa mwaka mmoja. Kwa hiyo, kwa vile bado miaka minne, tutarajie kwa pace iliyopo tutaweza kuwa na viwanda vitano tu! Hii tunasema ni Serikali ya viwanda, sasa swali, je, kauli mbiu tulizokuwa tunaziimba za nchi ya viwanda zilikuwa sahihi au tulikuwa tunawahadaa Watanzania?
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama hiyo haitoshi, tumeuliza juu ya Sera, ni Sera gani tuliyonayo kama nchi? Bado tuko kwenye Sera ya Ujamaa na Kujitegemea, tuko kwenye Sera ya Ubepari? Bado hata sisi wenyewe hata kauli mbiu ya nchi yetu hatuelewi tuko sehemu gani. Hilo swali tumeliuliza katika Kamati yetu. Tunakuja hapa tunasema sisi kama Serikali tunaenda kuwekeza kwenye viwanda, sisi kama Serikali tuna uwezo wa kuwekeza kwenye viwanda?
Mheshimiwa Mwenyekiti, ameuliza Mbunge mwenzangu; tumejiuliza ni kwa nini viwanda vyetu vilishindwa katika Awamu zilizopita na bado tunajidanganya kwamba tuna uwezo wa kuwekeza kwenye viwanda. Tukae chini tujiulize, Sera yetu ni nini? Ujamaa na Kujitegemea au tunaacha watu binafsi wawekeze kwenye viwanda. Kama tunataka watu binafsi wawekeze kwenye viwanda tumejiandaa vipi kuondoa kero ambazo zimekuwa zinawasibu na kurudisha viwanda nyuma. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunakuja kwenye kero mbalimbali ambazo wafanyabiashara wanapitia. Tumeandaa mazingira gani mazuri ya kuvutia wawekezaji wakati hapa nchini wafanyabiashara na wawekezaji wadogo tunawaona ni wapiga deal tu, leo sasa imekuja kauli mpya, wanaonekana kama ndiyo wanafanya biashara haramu. Sera zetu ni zipi kuhusu wawekezaji, hilo ndilo swali la tatu tunalopaswa kujiuliza juu ya mazingira rafiki. Nitaomba muda wangu ulindwe kwa sababu kuna mtu aliutumia vibaya tena kwa makusudi! (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, mazingira rafiki ya viwanda. Kuondoa tozo mbalimbali, kuweka one stop center. Nimeongea hapa Bungeni na narudia leo, tuwekeni one stop center na sio one collection center, kitu ambacho tunacho leo ni one collection center. Unaenda pale unawakuta Idara mbalimbali lakini wapo hawawezi kutoa maamuzi. Mtu yupo kama representative na inapokuja kwenye kufanya maamuzi anasema ngoja nimpigie bosi wangu. Sasa tunachokitaka ni one stop center na sio one collection center kama ilivyo leo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama haitoshi; kuna titiri mbalimbali za utozaji wa kodi. Unaenda TBS unaenda, TFDA, unaenda OSHA na vitu vingine ambavyo vinafanya kazi zile zile more or less the same function na tunasema kwenye Kamati tunataka mpango mkakati wa ku-harmonize hizi taasisi, hizi regulatory authority – tuwe na vitu vichache ambavyo vinapunguza kero kwa wafanyabiashara.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama haitoshi na inayosikitisha zaidi, TBS wanalalamika, TFDA wanalalamika, wanavyotaka kuingiza mashine za maabara wanatozwa pesa nyingi sana kama tozo ya ile mizigo inayoingia nchini na tunaomba sasa tozo zile zitolewe au zipunguzwe ili waweze kuingiza mashine za kutosha kwa ajili ya kuleta ufanisi ili kupunguza pia gharama za kupima vile vitu ambavyo wanapima kama whatever!
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ni miradi ya kuchochea maendeleo. Tangu nikiwa mwanafunzi wa shule nasikia mnaongelea Liganga na Mchuchuma. Nataka Waziri atuambie, hiyo story mwisho lini? Hii Serikali inayotuongopea na Hapa Kazi Tu ina mipango mikakati gani ya kumaliza ujenzi wa viwanda vya Liganga na Mchuchuma kama vichochezi vya kiuchumi wa miradi mingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunachokiona leo ni Mtukufu Rais kama mlivyosema akifanya ziara sehemu fulani akaona kuna changamoto ya barabara anaagiza barabara fulani itengenezwe kitu ambacho sisemi kama ni kibaya, lakini lazima tujikite katika kujenga miundombinu ambayo ita-link viwanda, maeneo ya uwekezaji na itawezesha ufanyaji wa biashara na mazingira mazuri kwa maana ya miundombinu katika eneo husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kitu kingine ni kuongezeka kwa riba ya yale maeneo ambayo yalikuwa yametengwa kama maeneo ya uwekezaji, EPZA. Tunavyozidi kuchelewa kulipa fidia ya maeneo hayo ndiyo gharama ya haya maeneo yanavyozidi kupanda. Amesema Mwenyekiti wa Kamati ilianza ikiwa bilioni 60, mwaka jana ilikuwa bilioni 191 na yeye amemalizia kusema hajui mwaka huu tutaambia ni bilioni ngapi, who knows pengine itakuja bilioni 300! Swali ni je, bado tuko kwenye the same track ya kutaka kuwekeza? Nini vipaumbele na mawazo yetu juu ya kuwekeza?
Mheshimiwa Mwenyekiti, Katibu Mkuu anasema wanataka waanzishe EPZA, maeneo maalum ya uwekezaji. Sasa maeneo maalum ya uwekezaji yanazidi kubaki kuwa ndotoni kwa sababu uhalisia haupo, maeneo hayajalipiwa fidia, hakuna hata ndoto ya kupata pesa ya kulipia fidia halafu tunakuja hapa tunasema Serikali ya viwanda. Ni lazima tujipange upya na tuamue tunataka kufanya nini kama Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kama sisi hatuwezi kuwekeza kwenye viwanda, tuandae Sera, mazingira, mazuri ya watu wengine kuwekeza. Kuna watu wanaosaidia kuleta ushindani katika kuwekeza, mfano fair competition kuna taasisi mbalimbali ikiwa ni pamoja na Fair Competition Commission. Wanakuja kutuambia wana wafanyakazi 53 tu na sio hao tu kuna TBS, kuna wafanyakazi, kuna idadi chache sana ya wafanyakazi na wale wanapaswa kufanya kazi nchi nzima. Tunategemea wale watu wafanye kazi kwa miujiza na wanachodai ni kwamba hawapati vibali vya kuajiri…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)
MWENYEKITI: AhsanteMheshimiwa.