Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru na mimi nataka kuchukua nafasi hii kumpongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kumteua Kamishna wa Tume ya Kuzua Dawa za Kulevya. Hiki ndicho kilikuwa kilio cha Wabunge. Mheshimiwa Mwenyekiti, Wabunge walikuwa wanapiga kelele mambo ya nchi yaendeshwe kwa mujibu wa sheria na kwa sababu sisi ndiyo watunzi wa sheria ilikuwa ni muhimu kupiga kelele ili sheria iweze kufuata mkondo wake. Haikuwa dhamira ya Mbunge yeyote aliyesimama katika Bunge hili ku-challenge utaratibu uliokuwa unatumika na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, haikuwa dhamira ya Mbunge yoyote kubeza kazi ambayo ilikuwa inafanyika na Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam, lakini dhamira ya Wabunge ilikuwa kilio cha kufuata taratibu ambazo nchi imejiwekea. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, kama tukiruhusu Nchi hii ikiendeshwa kwa viongozi wake kuvunja sheria tutaichana chana vipande vipande nchi yetu. Tunayo Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi ambayo tunaamini viongozi wake. Waziri wa Mambo ya Ndani, Katibu Mkuu na wengine wote wanaendesha Wizara ile kwa taratibu ambazo zimewekwa. Kwa hiyo, lilikuwa ni jambo la kusikitisha kusikia Mkuu wa Mkoa anatamka kama vile yeye ni Arresting Officer, watu waende wakaripoti kwake. Kila mtu mwenye akili na fahamu sawasawa, lazima alikuwa anapaswa ashangae. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi ninachosema, Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam alichokifanya pamoja na kwamba dhamira yake pengine kwa viwango vyake ilikuwa sahihi, lakini viongozi wa nchi yetu wasipodhibiti vitendo vya Mkuu wa Mkoa wa Dar es Salaam Bwana Makonda na wengine wa aina hiyo, nchi hii inakwenda kupasuka. Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi ukasimama tu ukamtuhumu Askofu na Kanisa lake kwa sababu kumtuhumu Askofu ni kutuhumu Kanisa zima, ni kutuhumu wenye imani hiyo, ni kuleta fujo! Huwezi kumtuhumu mtu halafu ukasema kwamba tutampekua halafu tukigundua kwamba hana tatizo tutamuachia. Umeshamchafua, utamsafisha namna gani? DCI ndiyo ana mamlaka ya kufanya upelelezi katika Jeshi la Polisi na anasimamia makachero wote. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, naamini vita ya madawa ya kulevya imekuwa ikiendelea kwa miongo yote ya utawala wa nchi hii kwa hatua mbalimbali. Alikuja Waziri Kitwanga hapa akatuambia ana majina 550, nina imani Mheshimiwa Mwigulu halali na hajalala anaendelea kufanya kazi hiyo, anaendelea kufanya shughuli hiyo. Isije ikajengwa hoja kwamba sasa Makonda anafanya kazi kuliko Waziri Mwigulu. Waziri Mwigulu anafanya kazi hiyo, DCI anafanya kazi hiyo lakini kiherehere cha baadhi ya viongozi vijana watafanya kazi hii isiendelee sawasawa. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo makubwa sana ya kutia shaka. Iko tuhuma inajengwa na bila shaka mmekwishaisikia kwamba Mheshimiwa Makonda sasa ana utajiri mkubwa kuliko umri wa kukaa kwake madarakani. Tunasikia amenunua apartment pale Viva Tower ya shilingi milioni 600. Mheshimiwa Rais umeingia madarakani kwa ahadi ya kwamba unapiga vita rushwa, huyu anatuhumiwa kwa kununua apartment kwa shilingi milioni 600, siamini kama Rais utakaa kimya. Vilevile Makonda huyu huyu anatuhumiwa amempa zawadi ya birthday yake mke wake Benz ya dola 250,000 sawa na shilingi milioni 400, hatuwezi kukaa kimya lazima tuseme. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, huyu huyu Makonda, Rais amezuia safari za Mawaziri, safari za Wabunge lakini amekwenda Ufaransa na mke wake, ameingia kwenye ndege daraja la business class dola 7,000, yeye na mke wake wamekaa siku 21. Kwa nini tusifikirie kwamba kitendo cha Makonda kutangaza hadharani watu ambao nafikiri anawatumia ilikuwa ni mkakati wa kufanya wauza madawa ya kulevya wakimbie ndani ya nchi? Kwa sababu sasa hivi ni muuza madawa gani mjinga ambaye amebaki katika nchi hii? Maana yake ni kwamba Makonda amesaidia wauza unga kuondoka katika nchi hii. Kwa sababu inawezekana Makonda anashirikiana nao na ndiyo maana sasa ana utajiri huu mkubwa kiasi hiki. (Makofi)
Mheshimiwa MWenyekiti, rai yangu ni kuwaomba viongozi wa Jeshi la Polisi, Kamishna Siro leo ameibuka anasema Mbowe asipokuja tutamfuata. Siro unamfuata kwa summons ipi uliyompa? Mpe summons kwa mujibu wa sheria ili aende. Kwa sababu sasa hivi kuna kiherehere tu, kila mtu anajifanya anafanya mambo sijui kwa namna gani anavizia uteuzi au Siro unataka u-IGP? Lazima tuseme kwa sababu hakuna mtu ambaye anaunga mkono madawa ya kulevya. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, ngoja niwaambie Waheshimiwa Wabunge, mimi nina mtoto muathirika. Kwa hiyo, kama kuna mwenye uchungu, mimi nina uchungu kweli kweli, tena tangu darasa la nne lakini Makonda asivuruge vita hii, sisi tunataka hawa watu wakamatwe. Watu hawa hawawezi kukamatwa kwa kuropoka, hawawezi kukamatwa kwa kujisifu, hawawezi kukamatwa kwa majigambo! (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa viongozi, sisi tunataka succession ya uongozi, watu wazima tunaondoka vijana waingie. Mimi namshauri Rais, vijana anaoingiza madarakani aangalie busara yao. Tulizungumza hapa juu ya DC Mnyeti yule wa Arumeru, lakini leo kwenye mtandao kuna habari DC alikaa hotelini na Afisa Sheria wa Arumeru anamwambia Rais, bwana mkubwa alinipigia simu ananiambia usiwe na wasiwasi fanya kazi, hawa Wabunge wajinga tu – hee! Hapo ndipo tulipofikia Waheshimiwa Wabunge. Makonda anaenda kwa wafanyabiashara, anampigia Rais simu halafu anaweka loud speaker ili wafanyabiashara wasikie Rais anavyowasiliana naye. Wale wote waliokuwa wanashughulikiwa kwa kukwepa kodi leo ndiyo marafiki wa Makonda. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Boniphace Getere alisema hapa, tuache mambo ya CHADEMA na CCM, tujenge nchi. Wabunge tuwe wakali kusimamia sheria za nchi hii, kusimamia principles, nchi yetu isonge mbele. Kama kuna ukweli tuseme kwa sababu matatizo yakitokea CCM haitapona wala CHADEMA hatutapona. Nchi hii ikipasuka CCM haitapona, CHADEMA haitapona. Nchi hii ina hierarchy ya uongozi, haiwezekani Siro am-supersede DCI, haiwezekani, iko wapi, kwa sababu Jeshi linaenda kwa command! Sasa DCI anachunguza madawa ya kulevya, Siro anachunguza madawa ya kulevya kwa amri ya Makonda, DCI anashirikiana na Waziri, fujo! Jeshi likiwa na fujo linasambaratika. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu hiyo niseme tu kwamba sisi Watanzania kwa ujumla wetu tunajua madhara ya madawa ya kulevya, hakuna asiyejua! CCM mnajua, CHADEMA mnajua, Watanzania wote mnajua. Watoto wetu wanaathirika, watoto wetu wanakuwa na tabia za ajabu ajabu. Tushirikiane ili vita hii iweze kufanikiwa lakini vita hii isiende kwa majigambo ya mtu mmoja ambaye anajifanya yeye ni bora na anaweza kupigana hii vita peke yake, hawezi! Atawaacha wale wanaohusika wakikimbia halafu matokeo yake vita itaishia njiani. Nakushukuru.