Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Juliana Daniel Shonza

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Sheria Ndogo na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Haki, Maadili na Madaraka ya Bunge na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

MHE. JULIANA D. SHONZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote ninakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia katika Kamati yangu ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama nikiwa Mjumbe wa Kamati hiyo. Nianze moja kwa moja kuzungumzia namna ambavyo bajeti inaathiri utendaji katika Wizara hii. Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo Taarifa ya Kamati imejieleza, kwa muda mrefu sana Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Kimataifa imekuwa ikishindwa kutekeleza majukumu yake kulingana na bajeti ambayo imekuwa ikitengwa, haifiki kwa wakati na hata ile ambayo ni ndogo ambayo imekuwa ikitengwa kwa ajili ya Kamati hiyo imekuwa haitoshelezi. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ambavyo ripoti imesema ukienda kuangalia Balozi zetu zina hali mbaya. Balozi zetu katika nchi za nje kwa kweli zimechakaa, fedha za matengenezo hakuna. Kama haitoshi, inafika mahali kama Kamati tunaona kwamba sasa lile lengo la kuwa na hizi Balozi nje haina maana. Kwa sababu lengo mojawapo la kuwa na Balozi katika nchi za nje ni kuhakikisha kwamba tunakuza diplomasia ya kiuchumi, lakini ukiangalia uhalisia huo kwa sasa haupo, Balozi zetu zinashindwa kufanya kazi kutokana na kwamba fedha za maendeleo zimekuwa hazipelekwi. Mheshimiwa Mwenyekiti, wale watumishi ambao wanafanya kazi katika Balozi hizo wamekuwa ni watu wa kupewa mishahara, lakini wanashindwa kutekeleza yale majukumu yao ya kimsingi kutokana na kwamba fedha zimekuwa haziendi. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe ushauri juu ya hilo kwamba ni vema sasa kama Wizara, ikaangalia utaratibu hizi fedha ambazo zinatengwa kwa ajili ya Wizara hiyo zikaenda moja kwa moja kwenye Balozi kama ambavyo fedha za maendeleo zimekuwa zikienda katika Halmashauri zetu. Kwa kufanya hivyo naamini kwamba itarahisisha utendaji kazi wa hizo Balozi. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, kama haitoshi, hata shughuli za Kamati katika mwaka huu wa fedha 2016/2017 kwa kiasi fulani Kamati ya Mambo ya Nje, Ulinzi na Usalama tumeshindwa kutekeleza majukumu yetu kama ambavyo tunapaswa kutekeleza, hususan kwa suala la mambo ya nje. Sisi kama Wajumbe wa hii Kamati tunavyozungumzia kwenda kutekeleza majukumu yetu, mojawapo ni kwenda kutembelea hizi Balozi kuangalia kama zinatekeleza majukumu yao ya kukuza diplomasia ya kiuchumi. Ni wazi kwamba kama Kamati haijawezeshwa kutekeleza jukumu hilo, sasa inafika mahali sisi Wajumbe tunakuja kuchangia hapa Bungeni kwa vitu ambavyo tumeletewa ripoti ya kwenye makaratasi, kitu ambacho sio kizuri. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, napenda kushauri katika bajeti ijayo ya mwaka wa fedha 2017/2018 nashauri kwamba Wizara iweze kuangalia utaratibu mpya kwamba fedha ambazo zinatengwa ziende kama zilivyopangwa na siyo kama ambavyo imetokea katika bajeti ya mwaka 2016/2017 Wizara imetengewa bilioni nane lakini imeenda bilioni tatu. Haijafika hata nusu yay ale malengo ambayo, kama Wizara ilikuwa imejiwekea. Vilevile hata vyama vya kibunge; kuna vyama kwa mfano PAP, ilikuja kwenye Kamati yetu lakini wakasema sisi hatuna kitu cha kuwasilisha kwa sababu hatujaenda popote. Ninaomba sana suala hili la bajeti liweze kuzingatiwa. Kwa kufanya hivyo tutaongeza ufanisi katika Bunge kama muhimili. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba pia nizungumzie suala lingine kama Kamati tuliweza kutembelea magereza mbalimbali. Tumetembelea Gereza la Songwe, gereza ambalo linajishughulisha na shughuli za uzalishaji mali na wamekuwa wakifanya hivyo na kuweza kulisha magereza mengine. Tatizo kubwa ni kwamba wamekuwa hawalipwi fedha zao kwa wakati na hiyo inasababisha kuwavunja moyo na inawaondolea ile hali ya kuendelea kuzalisha zaidi. Nashauri Wizara iangalie katika bajeti ijayo basi waweze kuzingatia yale madeni ambayo gereza linakuwa linaidai Serikali yaweze kwenda kulipwa kwa wakati kama ilivyo. (Makofi) Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumzie pia suala la polisi. Siku zote polisi wamekuwa wakifanya kazi katika mazingira magumu, lakini niipongeze Serikali kwa sababu…
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuunga mkono hoja.