Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

Hon. Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji na Taarifa ya Mwaka ya Shughuli za Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa Kipindi cha Januari, 2016 hadi Januari, 2017

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa fursa hii lakini nianze kwa kuipongeza Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kwa namna ambavyo tumekuwa tukishirikiana kufanya kazi na kutekeleza majukumu yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti,pia nichukue nafasi hii kusema kabisa mapema kwamba naunga mkono maoni na mapendekezo yote yaliyotolewa na Kamati, nasema mapema kwa sababu pengine muda hautatosha.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa ziko hoja ambazo nitazipitia haraka haraka katika muda huu mfupi uliopo. Hoja ya kwanza, naona wazi kabisa kwamba Wabunge wote wanakubaliana juu ya umuhimu wa utalii nchini hata michango yao na hoja zote walizozitoa zimejielekeza hivyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kukumbushana tu ni kwamba kwa sasa hivi Pato la Taifa linachangiwa na utalii kwa 17.2% wengine wanasema 17.5% lakini tuna kazi ya kuendelea kuboresha kwa sababu mwaka 2020 tunatakiwa tuwe tumefikia 18.3% na mwaka 2025 tunatakiwa tuwe tumefikia 19.5%. Yapo mambo ambayo tumekumbushwa na Kamati kwamba tuyafanye vizuri na Wizara imeyachukua kwa ajili ya kwenda kuyafanyia kazi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, miongoni mwa mambo hayo kuboresha miundombinu, lakini nataka nikumbushe tu kwamba upande wa miundombinu sio kila miundombinu ya utalii inatekelezwa na Serikali. Ipo inayotekelezwa na Serikali ambayo ni ile ya kuelekea kwenye vivutio na ile ya ndani ya vivutio tutaelekeza nguvu katika maeneo hayo kwa kushirikiana na Wizara nyingine kama Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi kwa ajili ya kuboresha miundombinu lakini iko miundombinu kama ya hoteli ambayo haitekelezwi na Serikali. Kwa hiyo, kule tutashirikisha tu wadau na sekta binafsi ili waweze kuboresha miundombinu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kuboresha utalii wa ndani, tayari tumekwishaanza jitihada na jitihada zenyewe ziko katika kutangaza lakini pia katika kuweka mazingira ambayo yatawawezesha watalii wa ndani waweze kupata huduma ya usafiri kwenda haraka. Upande mwingine wa ku-facilitate utalii wa ndani ni upande wa malazi. Wapo Wabunge wametoa hoja hapa kwamba gharama za malazi ni ghali sana kule pengine Serikali ifanye utaratibu wa kupunguza gharama. Katika hifadhi karibu nane au tisa hivi tunazo tayari hostels ambazo zina gharama nafuu lakini pia tunazo nyumba za bei rahisi kwa ajili ya watalii wa ndani, lakini tutaendeleza jitihada hizi ili katika kila eneo ambapo kuna vivutio tuweze kuweka mazingira ambayo watalii wanaweza wakaenda wakiwemo watalii wa ndani na waweze kufanya utalii kwa gharama nafuu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo suala la kuboresha upande wa Ukanda wa Kusini. Upande wa Ukanda wa Kusini tayari tuna mradi unaitwa REGROW ambao unajielekeza katika kujenga circuit ya Kusini ya utalii na huku tunajielekeza katika hifadhi kama vile ya Kitulo lakini pia zile nyingine za Katavi lakini pia ukanda mzima ule. Hapa niishukuru Serikali kwa kufungua upande wa Kusini mwa nchi, baada ya kuwekwa barabara ya lami sasa unaweza ukatoka Makambako ukafika mpaka Mtwara kwa barabara ya lami. Barabara ile inaweza sasa ikatumiwa vizuri sana na watalii wanaotoka Kusini mwa Afrika wakitokea upande wa mpaka wetu wa Kusini mwa nchi wanaweza wakatumia barabara ile sasa na kuunganisha Kusini na Mashariki mwa nchi kwa ajili ya kuboresha utalii. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kuboresha bidhaa za utalii kwamba tuna utalii wa aina moja, nataka niseme tu kwamba tayari tumeshapitia fukwe mbalimbali za bahari na maziwa lakini kwa upande wa fukwe za bahari tumeshapitia fukwe karibu 74 lakini hizi fukwe zina ownership mbalimbali. Wenye hizo fukwe ni watu binafsi, mahali pengine ni Serikali, sasa bado tuko kwenye utaratibu wa kuhakikisha kwamba tunaboresha mazingira ambayo yatawezesha uwekezaji katika maeneo hayo ili tuweze kujielekeza kwenye maeneo mengine ya utalii ukiwemo utalii wa kiutamaduni na utalii wa kihistoria.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuzungumzia utalii ingawaje ni kwa kifupi tu nizungumzie kuhusu uhifadhi. Hakuna utalii bila uhifadhi. Suala la uhifadhi limejadiliwa hapa kwa hisia mbalimbali, Waheshimiwa Wabunge wengi sana wamezungumzia kuhusu changamoto mbalimbali za uhifadhi. Kwa sababu ya muda, mimi niseme tu kwa kifupi, niseme maoni yote yaliyotolewa na Waheshimiwa Wabunge, interest zote za wadau mbalimbali nchi nzima, maslahi ya mtu mmoja mmoja, maslahi ya vikundi mbalimbali yote yatazingatiwa lakini mwisho wa siku tutazingatia maslahi ya Taifa. Ni vigumu sana kukidhi haja ya maslahi ya mtu mmoja au kikundi wakati maslahi ya Taifa yanaangamia. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, kwa kifupi nikisema hivyo nikienda kujielekeza sasa kwenye zile changamoto za uhifadhi niseme tu kwamba maeneo yote na hii nachukua kutoka kwenye hoja na maoni ya Kamati kwamba hakuna utata kuhusu suala la mifugo yote kuondoka ndani ya Hifadhi za Taifa. Tulisema kwamba yako maeneo ambayo mipaka ya baadhi ya vijiji inaingia ndani ya hifadhi na yako maeneo ambapo baadhi ya vijiji viko ndani kabisa ya hifadhi. Sasa huko kuna changamoto ambazo ni za kisheria zimo ndani ya Serikali, tunazifanyia kazi, tutaweza kuja kupambanua kujua kwamba sasa vijiji vile ambavyo vina utata wa namna hiyo tupitie sheria kwa namna gani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, viko vivutio vikubwa muhimu sana kama Ngorongoro kwa mfano kutaja vichache. Ngorongoro umuhimu umeelezwa, lakini mimi niongezee tu kwamba hapo mwanzoni tulikuwa na umuhimu wa Ngorongoro kwa sababu ya Crater zile tatu, Ngorongoro Crater yenyewe, Empakai Crater na Olmoti Crater. Hata hivyo, hivi karibuni utalii wa historia umejumuisha eneo la Olduvai Gorge pamoja na zile nyayo za Laetoli. Haya mawili yamefanya kupandisha hadhi ya Hifadhi ya Ngorongoro kuwa kubwa zaidi na kwa hiyo dunia nzima sasa hivi inakwenda kuona umuhimu wa Ngorongoro zaidi ya vile ambavyo tulikuwa tunaona hapo mwanzoni. Sasa zile changamoto za mifugo kuingia ndani, watu kujenga ndani majengo pamoja na watu kufanya huduma zingine za kijamii zote hizo sasa hivi ni changamoto ambazo tunatakiwa kwenda…
(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)
MWENYEKITI: Ahsante.