Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa kwa kipindi cha Miaka Mitano kuanzia mwaka 2016/2017 – 2020/2021

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi hii nami kuchangia Mpango wa Pili wa Maendeleo wa Taifa wa Miaka Mitano. Pia nichukue nafasi hii kuipongeza Serikali ya Chama cha Mapinduzi hasa Awamu ya Tano, kwa mwanzo mzuri wa utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi hasa katika utumbuaji majipu na dhamira thabiti ya ukusanyaji mapato ambao unakwenda kujibu changamoto kubwa ambayo ilikuwepo kwa ajili ya ufinyu wa mapato Serikalini ambapo inatuonesha mwanga sasa miradi ya maendeleo itakwenda kwa maana ya fedha kupatikana kwa wakati na maendeleo kufika kwa wananchi.
Pia, nimpongeze Waziri wa Fedha na Mipango kwa Mpango mzuri aliouwakilisha leo wa miaka mitano ambao unaonesha mwanga wa Tanzania mpya ambayo Watanzania walikuwa wanasubiri mabadiliko tuliyowaambia watayapata ndani ya CCM. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nakubaliana kabisa kama alivyosema Mheshimiwa Waziri, nchi nyingi zimeendelea kwa kupitia mlango wa viwanda, nchi nyingi zimepiga hatua kwa maendeleo ya viwanda, lakini pamoja na maendeleo ya viwanda pia viwanda vinategemea maendeleo ya miundombinu kwanza, kwa sababu miundombinu ndiyo ufunguo wa maendeleo ya viwanda, pamoja kwamba maendeleo ya viwanda ndiyo ufunguo wa maendeleo ya uchumi, lakini bila miundombinu rafiki, miundombinu mizuri na wezeshi maendeleo ya viwanda yatakuwa yana walakini kupatikana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali yangu kwa sababu ili kuwe na maendeleo ya viwanda, lazima Serikali ije na mpango mzuri wa kuboresha hii miundombinu ukizingatia Mheshimiwa Waziri anasema miongoni mwa changamoto ambazo awamu ya kwanza haikuweza kutekeleza vema katika maendeleo mazuri ya miundombinu, kwa mfano, katika miradi mitano ile mikubwa ya mpango huu, lipo suala la Mkulazi, Kijiji cha kilimo lakini miundombinu kule siyo mizuri. Matokeo yake kama alivyosema Mheshimiwa Waziri, mradi ule unatakiwa kutekelezwa pamoja na ushirikishwaji wa private sector, sasa private sector nyingi zikienda kule kufanya ukaguzi zinashindwa kufika kwa wakati. Hivi ninavyosema sasa hivi mawasiliano yamekatika huko Mkulazi kwenyewe, tunakwenda miezi sita kipindi cha miezi mitatu hii ya mvua huwezi kwenda.
Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri ili kuwavutia hao private sector waje, katika kuutekeleza mpango huu kwa uhalisia wake ni vizuri kuboresha miundombinu ya Mkulazi ukizingatia barabara, mawasiliano, umeme pamoja na maji ili lile eneo liwe rafiki, na liweze kuwavutia wawekezaji wengi kwa ajili ya mradi huu ambao utakuwa unajibu changamoto nzuri kuhusu maendeleo ya kilimo katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili, naomba nichangie katika suala la kilimo. Kilimo ndiyo uti wa mgongo, kilimo ndiyo kinachangia asilimia 75 ya ajira ya Watanzania, kilimo kinachangia pato la Taifa zaidi ya asilimia 25, lakini pia kinachangia katika fedha za kigeni asilimia 30 na pia kilimo ndiyo source kubwa ya mapato katika Halmashauri zetu nyingi Tanzania...
MHE. KHATIB SAID HAJI: Taarifa....
MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kwanza unilindie muda wangu na pia taarifa yake siipokei, kwa sababu nilikuwa sisomi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nachangia katika umuhimu wa kilimo, lengo lilikuwa kwa sababu ya umuhimu wa kilimo kama nilivyosema, namwomba Mheshimiwa Waziri katika mpango wake anapokuja, ni vizuri akaongeza bajeti ya kilimo kutoka iliyopo sasa angalau ingefikia asilimia 10, kwa umuhimu wa kilimo katika nchi yetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika suala la kilimo, kilimo kinategemea ardhi na sasa hivi tumeona changamoto kubwa iliyopo hapa nchini ni migogoro ya ardhi, nilitegemea katika mpango huu, Serikali ingekuja na majibu ya kutatua changamoto hiyo, hasa katika kupima ardhi, kuzingatia matumizi bora ya ardhi, ili kila eneo lipate mmiliki na wale wananchi waweze kumilikishwa ile ardhi waweze kuitumia kwa ajili ya kupatiwa Hati Miliki kama Hati zile za Kimila, zinaweza zikawasaidia katika kujipatia mikopo katika taasisi za fedha na kuanza kulima kilimo cha kibiashara zaidi kama walivyojiajiri katika hicho kilimo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia, tatizo la kilimo katika nchi yetu hii siyo wakulima tu, tatizo kubwa ni miundombinu ya kilimo imeachwa nyuma. Ningeshauri Serikali iongeze bajeti ya kilimo katika miundombinu ya umwagiliaji, ili kilimo kiweze kuwa na uhakika wa mavuno na kiweze kuzivutia taasisi za fedha ili kuwakopesha wakulima badala ya sasa wanategemea mvua na ndiyo maana wakulima wanashindwa kukopesheka.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri hata pale Serikali ilipokuja na mpango wa kujenga maghala kwa ajili ya kuhifadhia mazao, pesa zile zingetumika zaidi kwenye miundombinu ya kilimo, hasa umwagiliaji. Nafikiri tatizo la maghala wangekopeshwa tu, taasisi za fedha wangeweza kutoa kwa sababu, vile ni vifaa wezeshi tu vya kuhifadhia ambavyo vinavutia hata taasisi za fedha kukopesha wakulima, tofauti na sasa hawawezi kuwakopesha wakulima kwa sababu hawana uhakika mkulima huyu kama atavuna au atafanyaje.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo, Serikali ingeelekeza zaidi kuwekeza kwenye miundombinu ya kilimo badala ya mambo mengine, nina uhakika kikiwepo kilimo cha uhakika hizi taasisi za fedha zote zitavutika kwenda kuwekeza kwenye kilimo kwa sababu wana uhakika mkulima atavuna. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, tukiwezesha katika mipango bora hii ya ardhi kupima, tukiwatengea wafugaji eneo lao, kuwatengenezea miundombinu na kuwaweka pamoja nina uhakika hata hawa wafugaji wataweza kukopesheka na wataweza kuendelea na itawavutia wawekezaji wa viwanda vya maziwa waje kuwekeza katika maeneo yale, badala ya sasa wanashindwa kuwasaidia hawa wafugaji kwa sababu wamekuwa wachungaji badala ya wafugaji na mtu anajua kwamba hata akiwekeza katika kiwanda cha maziwa hana uhakika wa kupata raw material ya maziwa kwa sababu hawa wafugaji ni wa kuhamahama.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la masoko ya kilimo, Mheshimiwa Waziri wa Viwanda hapa alizungumza neno la busara kabisa na ni ukweli, kwa sababu alizungumza vizuri akasema, ili bidhaa zetu za kilimo za viwanda ziweze kuuzika lazima bei zetu ziwe za chini, kuna watu wamembeza kwa sababu tunataka tulete siasa katika suala la kiuchumi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukweli uliopo haya mazao ya kilimo tunayolima, yaliyo mengi sisi siyo watumiaji tunategemea soko la nje. Soko la nje wauzaji siyo peke yetu, lazima lina ushindani wa hali ya juu, kama bidhaa zetu zitakuwa na gharama kubwa wanunuzi wana nafasi kubwa ya kwenda nchi nyingine au kununua sehemu nyingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mchangiaji mmoja alizungumza hapa akasema wakulima hawana uhakika mwaka huu wanalima mbaazi bei imepanda, mwakani imeshuka analima ufuta! sababu kubwa haya ni mazao ya muda mfupi na kama mazao ya muda mfupi, mwaka huu Tanzania mkilima ufuta mkipata bei nzuri mwakani nchi nyingine nazo zinalima, matokeo yake supply inakuwa kubwa kuliko demand, ndiyo maana bei inashuka bei nyingine inapanda, sasa tukitaka tulete siasa katika mambo ya uchumi hatuendi. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono Serikali kwa mipango mizuri inayokuja nayo, Waziri wa Viwanda tuelezane ukweli na ndiyo maana nilishauri siku moja ni vizuri kukaundwa taasisi ya utafiti wa masoko ulimwenguni ili kutoa taarifa kwa wakulima wetu kuwaambia nini kinachohitajika ulimwenguni sasa hivi kilicho na bei nzuri badala ya kilimo cha historia, umezaliwa baba yako analima kahawa, analima mkonge, unataka ulime kitu hicho tu, wakati mwingine zao hilo halihitajiki huko kwa walaji. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia katika suala la migogoro ya ardhi. Kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri wa Ardhi kwa kazi kubwa aliyoifanya na mimi ni mnufaika mmojawapo. Alifika kijijini kwangu katika Kata ya Tununguo katika Kijiji cha Mliringwa na alichukua maamuzi hapo hapo baada ya kuona ubabaishaji. Aliweza kuirudisha kwa wakulima ardhi ya heka zaidi ya 3,500 kutoka kwa wawekezaji wababaishaji ambao waliipata kwa ujanja-ujanja. Nakuomba Mheshimiwa Waziri urudi tena, kama unavyoona Morogoro mkipita yote yale ni mapori, lakini siyo mapori ni mashamba ya watu. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna tatizo kubwa la mashamba pori, wenyewe wenyeji hatuna pakulima, kila shamba lina hati, lakini hayaendelezwi. Nakuomba sana urudi myahakiki, ili mturudishie tuweze kuendelea. Morogoro ilikuwa ndiyo hifadhi ya chakula, lakini kila mwaka uzalishaji wa chakula unapungua, sababu kubwa ni ardhi imeshikwa na watu ambao wameenda kukopea hela badala ya kuitumia kwa ajili ya uzalishaji mali. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, cha mwisho, naomba katika mpango ule wa Mkulazi, shamba namba 217 lenye hekta 63,000, mpango wa Serikali hekta zote 63,000 mnataka muwape Wawekezaji, heka 3,000 tu ndiyo mmetubakizia watu wa Mkulazi, watu wa Morogoro na Watanzania kwa ujumla, hizi heka 3,000 hazitoshi kwa Watanzania katika kijiji hiki cha mfano kinachotaka kujengwa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu na naishauri Serikali, tusiiuze hii ardhi kwa mgongo wa wawekezaji kwa watu wachache kama mpango unavyosema, heka 20,000 kwa mwekezaji mmoja wa miwa, heka 20,000 kwa mwekezaji wa pili wa miwa na heka elfu tano tano kwa maana ya 20,000 zilizobaki kwa wawekezaji wanne wa mpunga, halafu Watanzania tuliobaki au watu wa Morogoro heka 3,000.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali ni vizuri ardhi hii ikagawanywa mara mbili, nusu ikaenda kwa outgrowers kwa maana ya watu wa Mkulazi, Morogoro na Watanzania kwa ujumla waje wapate elimu ya kilimo cha kisasa pale kwenda kusambaza kwingine badala ya kuiondoa ardhi hii yote kuwapa wawekezaji huko mbele tunakokwenda kutakuwa ni kweusi, tusije kupata madhara kama wanayoyapata nchi nyingine, huko mbele vizazi vyetu vikaja kugombea ardhi na kuuana. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi hii na naunga hoja.